Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

FIQHI-UTANGULIZI

Faida
MAANA YA FIQ-HI KATIKA LUGHA NA SHERIA

Fiq-hi ni neno la kiarabu lenye maana mbili. Maana ya kwanza ni ya kilugha na ya pili ni ya kisheria. Katika lugha ya kiarabu neno "fiq-hi" maana yake ni kufahamu na kujua.

Fiq-hi kwa mtazamo wa sheria ni fani ya elimu inyoshughulikia na kusimamia utekelezaji wa sheria, kanuni na na taratibu za Uislamu katika maisha ya kila siku kwa ujumla fiq-hi ni sheria zinazoyatawala maisha ya Muislamu katika nyanja zote za maisha, kuanzia elimu, ibada, uchumi, ulinzi na usalama, ndoa, mirathi na kadhalika.

MISINGI YA FIQ-HI

Misingi ya fiq-hi ni chimbuko la elimu hii yaani mahala ambamo elimu hii imechukuliwa. Elimu ya fiq-hi imejiegemeza katika misingi mikuu minne kama ifuatavyo:

Qur-ani
Hadithi(sunnah)
Ijmaa,na
Qiyaasi

Hii ndio misingi na tegemeo la elimu hii ya fiq-hi.

Maana ya kila msingi

QUR-ANI

Qur-ani Tukufu ni kitabu kilichokusanya maneno matukufu ya Mwenyezi Mungu alichoshushiwa Mtume wa mwisho, Nabii Muhammad kupitia kwa Malaika Jibril ili kiwe ni sheria na muongozo kwa wanadamu wote.

HADITH(SUNNAH)

Hadithi (sunnah) ni tafsiri sahihi na ufafanuzi kamili wa Qur-ani Tukufu uliotolewa na Bwana Mtume kwa njia ya vitendo, maneno na "Iqraari"."Iqraari" ni kitendo cha Bwana Mtume kumuona mtu akitenda jambo fulani, kisha Mtume asitoe maelekezo yoyote ya kukemea au kukataza. Ukimya huu wa Mtume hutafsirika kuwa jambo lile linafaa kwani Mtume hawezi kulinyamazia jambo baya.

IJMAA

Ijmaa ni kongamano na makubaliano ya wanazuoni wa kiislamu baada ya kuja Mtume juu ya jambo au suala ambalo halikuelezwa kwa uwazi ndani ya Qur-ani au hadithi

QIYAASI

Qiyaasi ni mizani ya kulipima jambo au suala ambalo halina ufafanuzi ndani ya Qur-ani au hadithi na jambo au suala lililotajwa ndani ya Qur-ani au Hadith, kwa kulingana sababu.

Kwa ufupi hizi ndizo maana nyepesi na za awali za misingi hii minne ambayo ndio chimbuko la elimu hii ya sheria ya Kiislamu, elimu ya fiq-hi.

FAIDA YA FIQ-HI

Umuhimu na faida itokanayo na elimu hii ya fiq-hi unajidhihirisha katika maisha ya kila siku ya Muislamu, jamii na ummah mzima wa Kiislamu. Fiq-hi humsaidia Muislamu kujua:-

  • Maamrisho ya Mola wake, akayafuata ikawa ni sababu ya kupatia mafanikio ya Duniani na Akhera.
  • Makatazo ya Mola wake, akayaepuka ikawa pia ndio sababu ya kusalimika na maafa ya Duniani na Akhera.
  • Namna ya kutekeleza lengo la kuumbwa kwake ambalo ni ibada. Vipi na jinsi gani atamuabudu Muumba wake katika maisha yake yote.
  • Uhusiano wake na Mola wake, uhusiano wake na wanadamu wenziwe, uhusiano wa taifa na taifa jingine.
  • Halali na haramu. Fiq-hi ndio humbainishia ni lipi halali kutenda, kusema au kula na ni lipi haramu kutenda, kusema au kula.
  • Hukumu za makosa mbalimbali. Fiq-hi humuongoza Muislamu kutoa hukumu na adabu za makosa mbalimbali kuanzia yale madogo mpaka ya jinai.

Hizi ni baadhi ya faida zipatikanazo katika fani hii ya fiq-hi, kwa kuziangalia na kuzizingatia utaona na kufahamu kuwa Uislamu hauwezi kutekelezeka bila ya kuwa na elimu hii na hapo ndipo unapoonekana umuhimu wa fiq-hi.

HUKUMU YA SHERIA KATIKA FIQ-HI

Baada ya kuona faida na umuhimu wa fiq-hi hatuna budi kujua hukumu ya sheria katika elimu hii. Kila elimu katika Uislamu ina hukumu yake, elimu ya uchawi kwa mfano ni haramu kujifunza, elimu ya udaktari ni fardhi ya kutoshelezeana ndani ya mji, kama hakuna mwenye elimu hiyo ndani ya mji mzima basi wakazi wote wa mji ule huwa na madhambi.

Elimu ya fiq-hi ni fardhi kwa muislamu kujifunza kwani kwa kupitia elimu ndiyo huweza kutekeleza maamrisho ya Mwenyezi Mungu. Lakini ufaradhi huu unatofautiana baina ya mtu na mtu. Kwa mwengine huwa ni fardhi ya lazima kujua vipengele fulani na kwa mwengine huwa ni fardhi kifaaya.

FARADHI YA LAZIMA:

Kujifunza, kuijua na kutumia elimu hii ya fiq-hi inakuwa ni faradhi ya lazima kwa kila Muislamu mwanamume na mwanamke katika mambo ya ibada ya kila siku, kwa mfano sala na funga. Kujua kutoa zaka, au kujua jinsi ya kuhiji wakati hana uwezo si fardhi ya lazima bali ni faradhi kifaaya, ama kwa mwenye uwezo ni fardhi ya lazima kujua elimu hizo.

Kwa mantiki hiyo hiyo, mwenye kufanya biashara ni fardhi ya lazima kujua vipengele vya kufanya biashara ndani ya fiq-hi ili biashara yake iwe kwa mujibu wa sheria ya kiislamu, na kama hajafanya hivyo atakuwa na makosa mawili, kosa la kwanza ni kutojifunza hukmu ya uislamu ndani ya kazi yake na kosa la pili ni kutokufanya biashara yake kwa mujibu wa sheria kwa hivyo fahamu.

FARADHI YA KUTOSHELEZEANA

Elimu hii inakuwa ni faradhi ya kutoshelezeana katika masuala ya mirathi, elimu ya ukadhi, elimu ya kutoa fat-wa na elimu nyingine zinazofanana na hizo. Sasa ikiwa ndani ya mji hakuna anayejua masuala ya mirathi, wakazi wote huwa na madhambi kwa kutojifunza elimu hiyo.

Huu ndio mgawanyo wa hukumu ya sheria kuhusiana na fani hii ya elimu ya fiq-hi.

HUKUMU ZA SHERIA YA KIISLAMU

Jambo lolote lile katika maisha ya kila siku ya Muislamu linaangukia kwa mujibu na mtazamo wa sheria katika mafungu yafuatayo ya hukumu:-

Faradhi/Wajibu
Sunnah
Haramu
Mubah
Makuruuh

Hizi ndizo hukumu tano zinazoitawala sheria ya kiislamu, na ifuatayo ni maana na ufafanuzi mdogo wa kila hukumu:-

FARADHI/WAJIBU

Faradhi au Wajibu ni jambo ambalo mtu baleghe, mwenye akili timamu amelazimishwa na sheria kulitenda. Mtu mwenye sifa hizo tulizozitaja akilitenda la faradhi kama vile swala, funga n.k. kwa kumtii Mola wake hupata thawabu na akiacha kutenda bila ya udhuru wowote unakubalika kisheria anastahiki kupata dhambi na adhabu ya Mola.

SUNNAH

Sunna kwa mtazamo wa fiq-hi ni kinyume cha faradhi. Kwa hivyo basi sunnah ni jambo ambalo sheria haikumlazimisha mtu kulitenda bali imempa khiyari kutenda au kutotenda. Mfano wa sunnah ni kama vile kuanza kutoa salamu, kuwapa sadaka masikini, kufunga Al-khamisi na Jumatatu na kadhalika. Atakayelitenda jambo la sunnah atalipwa thawabu na atakayeacha hatopata dhambi wala kuadhibiwa.

HARAMU

Haramu ni kila jambo ambalo sheria imekataza kabisa kulitenda kama vile kuiba, kusema uwongo, kunywa pombe na kadhalika. Mtu aliye baleghe na mwenye akili timamu akilitenda lililoharimishwa kwa kuvunja amri ya Mola atastahiki kupata dhambi na adhabu na akiacha kutenda haramu kwa kufuata amri ya Mola atapata thawabu.

MUBAAH

Mubaah ni jambo ambalo sheria haikulazimisha mtu kulitenda na wala haikumkataza kulitenda. Mfano wa mubaah ni kama vile kuvaa nguo nzuri mno au kula vyakula vizuri vizuri. Hapana thawabu wala dhambi ndani yake.

UZINDUSHI:

Mtu akitenda jambo la Mubaah kama vile kula na akatia nia ya kupata nguvu ya kufanya ibada, atapata thawabu na kinyume chake akinuia kwa jambo hilo hilo la Mubaah kumuasi Mwenyezi Mungu basi atapata dhambi.

MAKURUUH:

Makuruuh ni kila jambo ambalo linachukiza kulitenda kwa mtazamo wa sheria. Hastahiki mtu kupata adhabu ya Mola kwa kulitenda bali akiacha atapata thawabu.

 


JIFUNZE : Dini ya Uislamu inatoa mwongozo kwenye kila kipengele cha maisha, kutokutumia mwongozo huu ni kumuasi Mola wetu aliyetuumba na haiwezekani tukaamua ni yepi ndani ya dini tufuate na yepi tuyaache kwani tutakuwa hatuna tofauti na mayahudi na uma zilizotangulia ambao walitekeleza waliyoyapenda na kuacha wanayoyachukia na wakashushiwa laana ya Mwenyezi Mungu na siku ya kiyama watapata adhabu kali.


Forum | Guestbook | Tuandikie |