Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

MAMBO YALIYO HARAMU KWA MWENYE JANABA

 

Mtu akipatwa na janaba kwa maana ya janaba kama tulivyoeleza katika maelezo yetu ya awali yanamuharimikia kwa mujibu wa sheria mambo yafuatayo:-

  1. Kuswali swala ya fardhi au ya sunnah. Hili ni kwa mujibu wa kauli ya Mwenyezi Mungu Mtukufu: "ENYI MLIOAMINI! MSIKARIBIE SWALA, HALI MMELEWA MPAKA MYAJUE MNAYOSEMA WALA HALI MNA JANABA ISIPOKUWA MMO SAFARINI (mnapita njia) MPAKA MKOGE…" [4:43]

Muradi na makusudio ya neno SWALA katika aya hii ni MAHALA PA KUSWALIA (msikiti) kwa sababu kupita njia hakupatikani ndani ya swala. Ikiwa mwenye janaba anakatazwa kupita msikitini, basi kukatazwa kuswali ni aula zaidi.

Amepokea Imam Muslim kutoka kwa Ibn Umar- Allah awawiye radhi- amesema : Hakika nimemsikia Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie- akisema "Haikubaliwi swala bila ya twahara".

Twahara iliyotajwa katika hadithi ni pamoja na twahara ya hadathi ndogo na janaba (hadathi kubwa). Hadathi hii inafahamisha uharamu wa kuswali kwa mwenye hadathi zote hizo; hadathi ndogo na hadathi kubwa(janaba).

  1. Kukaa msikitini. Ama kupita njia tu bila ya kukaa si haramu. Haya yanafahamika kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu : "…WALA HALI MNA JANABA, ISIPOKUWA MMO SAFARANI(mnapita njia)…". Yaani msiikurubie swala wala mahala pa kuswali (msikiti) mtakapokuwa mna janaba bila kukurubia kwa nia ya kupita njia, huku hakukukatazwa. Naye Mtume wa Mwenyezi Mungu amesema: "Msikiti si halali kwa mwenye hedhi wala mwenye janaba". Abu Daawoud
  2. Kutufu Al-Kaaba , twawafu ya nguzo/fardhi au ya sunna. Hii ni kwa sababu twawafu iko katika daraja ya swala, kwa hiyo nayo imeshurutizwa twahara kama ilivyo kwa swala. Haya ni kwa mujibu wa kauli ya Bwana Mtume –Rehema na Amani zimshukie- aliposema: "Kutufu al-Kaaba ni swala, isipokuwa kwamba Allah amekuhalalishieni kuzungumza ndani yake (twawafu), basi atakayazungumza na asizungumze ila la kheri". Al-Hakim
  3. Kusoma Qur-ani. Amesema Nabii Muhammad Rehema na Amani zimshukie: "Asisome mwenye hedhi wala mwenye janaba chochote katika Qur-ani". Tirmidhiy

ANGALIA: Inajuzu kwa mwenye janaba kuisoma Qura-ani moyoni bila ya kuitamka kwa ulimi, kama ambavyo inavyomjuzia kuutazama Msahafu bila kuushika. Kadhalika inamjuzia kusoma dhikri/nyiradi za Qur-ani kwa kukusudia ile dhikri na sio Qur-ani yenyewe. Dhikri ya Qur-ani ni kama vile mtu kusema:
(RABBANAA AATINAA FID-DUN-YAA HASANATAN WAFIL AAKHIRATI HASANATAN WAQINAA ADHAABAN-NAAR)[2:201] kwa kuikusdua aya hii kama dua. Na kama vile kusoma anapokipanda kipando (chombo cha usafiri)
("SUB-HANNAL-LADHIY SAKHARA LANNA HAADHA WA MAA KUNNAA LAHU MUQRINIYN") [43:13] kwa kuisudia hii dua na sio dhati ya Qur-ani yenyewe. Allah ndiye mjuzi mno.

  1. Kuugusa au kuubeba /kuuchukua msahafu au karatasi/kataa la msahafu au ngozi/jalada lake au kuuchukua msahafu ukiwa ndani ya mfuko au sanduku. Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu: "HAPANA AKIGUSAYE ILA WALE WALIOTAKASWA" [56:79]

Bwana Mtume –Rehema na Amani zimshukie- anatufasiria aya hiyo kwa kusema : "Asiiguse Qur-ani ila aliye twahara ". Daaruqutuniy na Maalik.

ANGALIA: Inajuzu kwa mwenye janaba kuubeba msahafu ukiwa pamoja na mizigo au ndani ya nguo sandukuni na wala hakuukusudia kuubeba ule msahafu bali mizigo/nguo. Kadhalika inamjuzia kuvichukua vitabu vya tafsiri ya Qur-ani iwapo ile tafsiri ni nyingi kuliko Qur-ani. Allah ndiye mjuzi mno wa lililo la sawa na haki.

ii) HEDHI

A/. MAANA YA HEDHI

Hedhi katika lugha ya kiarabu, maana yake ni KUCHURIZIKA. Ama hedhi kwa mtazamo wa sheria ni DAMU YA MAUMBILE yaani damu hii ni sehemu/ni katika jumla ya maumbile ya mwanamke, mwanamke kaumbwa hivyo kwa lengo maalum. Damu hii kutoka ndani kabisa ya tumbo la uzazi kila mwezi baada ya mwanamke kutimiza kwa uchache umri wa miaka tisa

B/. DALILIYAKE

Dalili na ushahidi juu ya kuwa hadhi huwajibisha josho la kisheria ni Qur-ani Tukufu na sunnah(hadithi). Ama katika Qur-ani ni kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu : "NA WANAKUULIZA JUU YA HEDHI , WAAMBIE HUO NI UCHAFU. BASI JITENGENI NA WANAWAKE WAKATI WA HEDHI (zao). WALA MSIWAKARIBIE MPAKA WATWAHARIKE. WAKISHATWAHARIKA BASI WAENDEENI KATIKA PALE ALIPOKUAMRISHENI ALLAH…"[2.222]

Ama dalili yake katika sunnah ni kauli ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie kumwambia Fatmah Bint Abiy Hubayshi Allah amuwiye radhi-: "Itapokujia hedhi , basi acha kuswali na itakapomalizika (kutoka) basi ikoshe damu (twaharisha) na uswali" Bukhaariy na Muslim.

B/. MUDA WA HEDHI

TunAkusudia kwa ibara (Muda wa hedhi) kile kipindi ambacho mwanamke hutumika yaani huwamo hedhini. Kipindi hiki tunaweza kukigawa katika sehemu tatu,kama ifuatavyo:-

  1. Kipindi kifupi;
  2. Kipindi kirefu na
  3. Kipindi cha ghalibu (ada)

KIPINDI KIFUPI – Hii ndio muda wa chini kabisa wa kutoka damu ya hedhi hiki ni kipindi cha masaa ishirini na nne (24). Hii inaamaanisha kuwa mwanamke anaweza kuingia hedhini mchana na usiku wake tu, kisha damu ikakatika

KIPINDI KIREFU-Huu ndio muda wa juu kabisa wa kutoka damu ya hedhi. Hiki ni kipindi cha siku kumi na tano (15), mchana na usiku

KIPINDI CHA GHALIBU- Huu ndio muda wa ada na desturi kwa wanawake walio wengi, yaani wanawake wengi hutumika katika kipindi hiki. Huu ni muda wa siku sita au saba

Muda wa chini wa twahara, yaani kipindi cha chini ambacho mwanamke anakuwa katika twahara ni siku kumi na tano(15). Hakuna ukomo (limit) wa wingi wa twahara kwani inawezakana kabisa mwanamke asipate hedhi kwa muda wa mwaka, miaka miwili au miaka kadhaa na hili limethibiti kwa majaribio

Mwanamke atakapoiona damu chini ya kipindi kifupi cha hedhi yaani chini ya masaa ishirini na nne au aliiona damu baada ya kule kipindi kirefu cha hedhi, yaani baada ya siku kumi na tano, damu hii itazingatiwa kisheria kuwa ni damu ya ISTIHAADHA na sio damu ya hedhi

C/. NINI ISTIHAADHA?

Istihaadha ni damu ya ugonjwa damu hii hutoka katika mshipa ulio ndani kabisa ya tumbo la uzazi. Damu hii hutengua udhu lakini haiwajibishi josho kama ilivyo kwa damu ya hedhi. Kadhalika damu hii haitoi fursa ya kuacha kuswali na kufunga. Mwanamke mwenye maradhi haya ya Istihaadha anatakiwa aioshe damu na afunge utepe mahala itokapo, kisha atawadha na halafu aswali. Imepokelewa riwaya kutoka kwa Fatmah Bint Abiy Hubaysh –Allah amuwiye radhi –kwamba yeye alikuwa akitokwa na istihaadha. Bwana Mtume –Rehema na Amani zimshukiae- akamwambia: "Ikiwa ni damu ya hedhi, basi itakuwa ni damu nyeusi ijulikanayo. Itakapokuwa hivyo, basi acha kuswali, ikiwa ni nyingine basi tawadha na uswali, hakika si vingenevyo huo ni mshipa ". Abu Daawoud.

D/. MAMBO YALIYO HARAMU KWA MWENYE HEDHI

  1. Kuswali- kwa ushahidi wa hadithi hiyo ya Fatmah Bint Abiy Hubaysh tuliyoitaja hapo katika Istihaadha.
  2. Kusoma Qur-ani na kugusa na kuuchukua msahafu kwa ushahidi tulioutaja katika yakiyo haramu kwa mwenye janaba (namba 4 na 5)
  3. Kukaa msikitini si kupita njia kwa ushahidi uliotajwa katika yaharamikayo kwa mwenye janaba (namba 2). Miongoni mwa dalili zinazoonyesha kuwa nafsi ya kupita hakukuharamishwa, mbali na ushahidi uliopita ni hii riwaya iliyopokelewa na Imam Muslim kutoka kwa Bi: Aysha –Allah amuwiye radhi- amesema: Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliniambia: "Niletee mswala msikitini" Nikamwambia: Mimi nimo hedhini.akaniambia. "Bila shaka hedhi yako hiyo hunayo mkono mwako ".
  4. Kutufu Al-Kaaba kwa ushahidi uliopita katika yaliyoharamishwa kwa mwenye janaba (namba 3). Imepolewa na Bi Aysha-Allah amwiye radhi –amesema :Tulitoka hali ya hatujidhani ila ni wenye kuhirimia hija, tulipofika sehemu iitwayo sarafu nikaanza kutokwa na hedhi. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie- akaingia kwangu na il-hali nikilia akaniuliza: "Una nini, umeigia hedhini?" nikamjibu: Naam. Akaniambia : Hakika hili ni jambo ambalo Mwenyezi Mungu amewaandikia (amewafaradhishiya) mabinti wa Adam (wanawake). Fanya/tekeleza ibada azifanyazo hujaji isipokuwa usifanye twawafu katika al-kaaba". Na katika riwaya nyingine "mpaka utwahirike".
  5. Kupita msikitini kwa sababu damu ni najisi na ni haramu kuuchafua msikiti kwa najisi na uchafu mwingineo. Ikiwa mwanamke atajiaminisha kutokuuchafua msikiti, basi anaweza kukatiza na kupita msikitini
  6. Kufunga, haijuzu kwa mwenye hedhi kufunga swaumu ya fardhi au ya suna, haya ni kwa mujibu wa riwaya ya Abiya Said-Allah amuwiye radhi. Kwamba Mtume wa Mwenyezi Allah –Rehema na Amani zimshukie – alisema kuhusiana na mwanamke wakati alipoulizwa juu ya maana ya upungufu wa dini yake (mwanamke): "Je, hakuwa aingapo hedhini, haswali na hafungi?". Bukhariy na Muslim

Atakidhi/atalipa mwenye hedhi swaumu iliyomfutu katika kipindi cha hedhi baada ya kutwahirika kwake. Wala hawajibikiwi kukidhi swala zilizompita katika kipindi hicho. Itakapokatika hedhi yake, itamuwajibikia funga hata bado hajakoga. Impokelewa kutoka kwa Bi Muaadhah, amesema : nilimuuliza Bi Aysha –Allah amuwiye radhi–na akasema: kwa nini mwenye hedhi anakidhi swaumu na wala hakidhi swala ? Akasema: "hayo yalikuwa yakitupata tulipokuwa pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimeshukie, basi tukiamrishwa kukidhi swaumu na wala hatukuamrishwa kukidhi swala"Bukhariy na Muslim

  1. Kuingiliwa yaani kufanya naye tendo la ndoa. Haya yanatokana na kauli ya Allah: "BASI JITENGENI NA WANAWAKE WAKATI WA HEDHI (zao) WALA MSIWAKARIBIE MPAKA WATWAHARIKE. WAKISHAKUTWAHIRIKA BASI WAENDEENI KATIKA PALE ALIPOKUAMRISHENI ALLAH…" [2:222].

Muradi na makusudio ya kujitenga na wanawake ni kuacha kuingiliana nao kimwili. Imepokelewa kutoka kwa Abdillah Ibn Saad. Allah Amuwiye radhi –kwamba yeye alimuuliza Bwana Mtume –Rehema na Amani zimshukie: Ni kipi kinachonihalalikia kwa mke wangu wakati awapo hedhini? (Mtume) akamjibu: "Ni halali yako kilicho juu ya ya shuka (gaguro). Abu Daawoud.

NYONGEZA KATIKA KUTAJA UMRI WA KUBALEGHE

Tamaanisha na kukusudia kwa neno "baleghe" ule umri ambao atakapoufika mtu mwanamume au mwanamke hupata sifa ya kuwa ni mtu MUKALLAFU. Yaani sasa anatakiwa kuyatekeleza yale yote aliyoamrishwa au kukatazwa na sheria; tangu swala, swaumu, hijah na ibada nyingenezo.

Baleghe hujulikana kwa kupatikana mojawapo ya mambo matatu haya :-

  1. kujitolea na kutokwa na manii. Hili hushirikiana msichana na mvulana yaani msichana naye hujitolea usingizini kama ajiotoleavyo mvulana.
  2. Msichana kuanza kutokwa na damu ya hedhi kipindi cha mwanzo ambacho msichana anaweza kujiotelea au kutokwa na damu ya hedhi ni miaka tisa ya mwezi muandamo. Kuchelewa au kuwahi kupata hedhi hutofautiana baina ya nchi na nchi, mtu na mtu na hali za kimaisha.
  3. Mvulana au msichana kutimiza umri wa miaka kumi na tano kwa mwaka wa mwezi mwandamo. Hili ni iwapo hajajitolea au kupata hedhi mpaka kufikia umri huo

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |