|
Kumesuniwa katika utekelezaji wa tendo la kutayamamu mambo kadhaa,
miongoni mwa mambo hayo ni haya yafuatayo :-
- Kunasuniwa katika tayamamu yale yote ambayo ni suna katika udhu. Kuanzia na :
- Kupiga Bismillah mwanzo wa kutayamamu
- Kuanza na sehemu ya mwanzo ya uso.
- Kuanza kupangusa mkono wa kulia.
- Kupangusa sehemu kidogo ya kichwa wakati wa kupangusa uso
- Kupangusa sehemu ya kufupa panya wakati wa kupangusa mikono
- Kufululiza baina ya kupangusa uso na mikono
- Kuomba dua baada ya kutayamamu.
Imepokelewa hadithi na Ammaar Ibn Yaasir- Allah awawiye radhi
: Kwamba wao walitayamamu wakiwa pamoja na Mtume wa Allah Rehema na Amani zimshukie
kwa ajili ya swala ya Alfajiri. Wakapiga viganja vyao mchangani, kisha wakapangusa
nyuso zao mara moja. Halafu wakarudia tena kupiga viganja vyao mchangani mara nyingine,
wakapangusa mikono yao yote mpaka katika maungio ya kifupa panya na bega na (kupangusa)
kwapa kwa matumbo ya vitanga.Abuu Daawood
- Kutapanya vidole wakati wa kupiga viganja juu ya mchanga na kueneza uso kwa pigo
moja tu la mchanga na kuieneza mikono kwa pigo jingine.
- Kupunguza vumbi kwa kukunguta viganja baada ya kupiga au kwa kupulizia
viganja. Suna hii inapatikana katika hadithi iliyopokelewa na Swahaba Ibn Yaasiri- Allah
amuwiye radhi kwamba Mtume wa Mwenyezi Mungu Rehema na Amani zimshukie
alimwambia : Hakika si vinginevyo inakutosha kufanya hivi. Akapiga (Mtume)
viganja vyake juu ya ardhi pigo moja kasha akavikunguta (viganja). na katika riwaya nyingine: na
akapulizia ndani yake (viganja) halafu akapangusa kwa (viganja) hivyo.
Bukhaariy.
NUKTA ZA KUZINGATIWA KATIKA MAS-ALA YA TAYAMAMU.
Kabla hatujaanza kuzungumzia mambo yanayotengua tayamamu ni
vema tukaziangalia kwanza nukta kadhaa muhimu katika suala zima la kutayamamu. Nukta
zenyewe ni hizi zifuatazo:
1 : KUTAYAMMAMU BAADA YA KUINGIA WAKATI WA SWALA
Yeyote ambaye zimepatiakana kukamilika kwake sababu
zinazomuhalalishia kutayamamu badala ya kutawadha au kuoga, haimuelei na kumjuzia
kutayamamu kwa ajili ya swala ya fardhi ila baada ya kuingia wakati wa swala hiyo. Ni
lazima kutayamamu huko kuwe ndani ya wakati na sio
nje yake. Huo ndio utaratibu unaopatikana katika kauli yake Bwana Mtume- Rehema na Amani
zimshukie : "Popote pale mtu katika umati wangu itakapomdiriki swala, basi na
aswali." Bukhaariy " Popote inaponidiriki swala hupangusa (hutayamamu) na
kuswali Ahmad. Riwaya mbili hizi tulizozitaja
zinafahamisha kwamba kutayamamu huwa wakati wa kuidiriki swala, na kuidiriki swala
hakupatikani ila baada ya kuingia wakati wake hiyo swala husika. Haya ndiyo mafahamisho na
eleweko la hadithi mbili hizi, elewa !
2: KUTAYAMAMU KWA KILA SWALA YA FARDHI:
Kisheria mtu huruhusiwa kuswali kwa tayamamu moja swala moja tu ya
fardhi na tayamamu moja swala nyingi awezazo za suna ikiwa ni pamoja na swala ya jeneza
(maiti) ijapokuwa swala hii si suna bali ni fardhi ya kutoshelezeana kama tutakavyokuja
kuona katika masomo yetu yajayo. Kauli ya jumla
tunaweza kusema :
Kwa mantiki hii, mtu akitaka kuswali atayamamu tena hata kama
tayamamu yake ya kwanza haijatenguka. Maelekezo haya yanaihusu swala ya fardhi
inayoswaliwa ndani ya wakati ( ADAA) au ile inayoswaliwa nje ya wakati wake (KADHAA). Haya
ndiyo mafundisho ya Bwana Mtume Rehema na
amani zimshukie yanayopatikana katika riwaya iliyopokelewa na Ibn Umar Allah
awawiye radhi amesema ( Ibn Umar katika kuelezea tayamamu ya Mtume)
akitayamamu kwa kila swala hata kama hakuhuduthi. Al-Baihaqiy.
3: KUTAYAMMAMU HUWA NI BADALA YA JOSHO LA FARDHI KAMA KUNAVYOKUWA
BADALA YA UDHU.
Mtu anapopatwa na mojawapo ya mambo yanayomuwajibishia josho la
kisheria. Rejea somo la nne kipera/kipengele cha nne na akawa hawezi kutumia maji kwa
sababu tulizokwishazielezea katika masomo yaliyotangulia au hakuweza kupata maji mahala
alipo, basi tayamamu itamtoshelezea josho hilo. Tunakusudia kusema kuwa atayamamu badala
ya kuoga na kupata ruhusa na uhalali wa kuyafanya yale yote aliyokuwa haruhusiwi kuyafanya
kisheria. Hivyo ndivyo tunavyofahamishwa na tamko la Mwenyezi Mungu Mtukufu :
NA MKIWA NA JANABA BASI OGENI NA
MKIWA WAGONJWA AU MMO SAFARINI, AU MMOJA WENU AMETOKA CHOONI AU MMEINGILIANA NA WANAWAKE,
NA HAMKUPATA MAJI, BASI KUSIDIENI (tayamamuni) UDONGO (mchanga) ULIO SAFI
..
(5:6) Kadhalika hayo ndiyo maelekezo yanayopatikana kutokana na riwaya iliyoipokelewa na
Imraan Ibn Huswayn Allah awawiye radhi amesema : tulikuwa safarini pamoja na Mtume
wa Mwenyezi Mungu rehema na amani zimshukie, (Mtume) akawaswalisha watu
(maswahaba). Tahamaki huyo ni mtu amejitenga, Mtume akamuuliza, Ni lipi
lililokuzia kuswali?. Akajibu : Nimepatwa na janaba na
hakuna maji (ya kuoga), (Mtume) akamwambia: Tumia mchanga, hakika huo
unakutosha Bukaariy na Muslim.
VITENGUZI VYA TAYAMAMU
Tayamamu hutenguka na kubatilika kwa kupatikana mambo yafuatayo :
- Mambo yote yanayotenguka na udhu tuliyoyataja katika mlango wa udhu (rejea).
- Kupata maji baada ya kuyakosa. Hii ni kwa sababu kutayamamu ni badala ya maji, kwa
mantiki hii itakapopatikana asili (maji) hubatilika badala (tayamamu). Haya ndiyo
mafundisho ya Uislamu kwa mujibu wa hadithi
iliyopokelewa na Abu Dharri Allah amuwiye radhi kwamba Mtume wa mwenyezi
Mungu Rehema na Amani zimshukie amesema : hakika udongo (mchanga) ulio safi
ni tahara ya muislamu hata kama hakupata maji kwa miaka kumi. Atakapoyapata maji basi na
ajitwaharishe nayo kwani kufanya hivyo ndio bora Abuu Daawoud.
Hadithi hii inafahamisha kubatilika kwa tayamamu kwa kupatikana maji
TANBIHI : 1. Mtu akiyapata maji baada ya kumalizika kwa swala (baada
ya kuswali), swala yake itakuwa ni sahihi na haimpasii wala kumuwajibikia kuikidhi swala
hiyo. Kadhalika lau atayapata maji baada ya kuanza kuswali, basi na aikamilishe swala nayo
itakuwa ni sahihi. Lakini katika hali hii ni vema zaidi iwapo ataikata swala ili atawadhe
na kuswali kwa udhu. Atafanya hivyo ikiwa muda upo wa kutosha kutawadha na kuswali ndani
ya wakati yaani kabla ya kutoka wakati wa swala husika.
2. Uwezo wa kuyatumia maji. Hili ni kwa mtu aliyekuwa mgonjwa na
akashindwa kutumia maji katika udhu au josho. Huyu
akipona, hana tena ruhusa ya kutayammamu kwa sababu ya kuondoka jambo lililompa uhalali wa
kutayamamu ambalo ni ugonjwa.
3. Kuritadi yaani kutoka katika Uislamu tunamuomba Mola wetu
Mtukufu atukinge na hilo.
|