Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

NGUZO  ZA SWALA ...

Faida

11.             KUMSWALIA MTUME BAADA YA TASHAHUDI YA MWISHO.

Hii ndio nguzo ya kumi na moja ya swala. Nguzo hii yaani

kumswalia Bwana Mtume, huchukua nafasi mara tu bada ya kukamilka kwa tashahudi na kabla ya kutoa salamu. Hapo ndipo mahala pake nguzo hii.

Dalili ya swala  ya Mtume.

Kumswalia Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – ndani ya swala ni katika kulitekeleza agizo na amri ya Allah isemayo “HAKIKA ALLAH ANAMTEREMSHIA REHEMA MTUME (anaswalia) NA MALAIKA WAKE (wanamuombea dua) BASI, ENYI WAUMINI MSWALIENI (Mtume, muombeeni rehema) NA MUOMBEENI AMANI” (33:56).

Wanazuoni wamekongamana na kuwafikiana kwamba kumswalia Mtume si WAJIBU ila ndani ya swala tu. Uwajibu huu unatokana na riwaya nyingi sahihi ikiwemo hii iliyopokelewa kutoka kwa Ibn Masoud – Allah amuwiye radhi – katika (kueleza) swali aliloulizwa Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – juu ya kuswaliwa kwake. Tukuswalieje ndani ya swala? Akajibu, Semeni.

ALLAHUMMA SALLI ALAA MUHAMMAD WA ALAA AALI MUHAMMAD KAMAA SALLAYTA ALAA IBRAHIM WA AALI IBRAHIM WABAARIK ALAA MUHAMMAD WA ALAA AALI MUHAMMAD KAMAA BAARAKTA ALAA IBRAHIM WA ALAA AALI IBRAHIM FIL-AALAMINA INNAKA HAMIDUN MAJID  Bukhariy na Muslim

Riwaya hii ndio inayoanisha kwamba mahala pa wajibu pa kumswalia Bwana Mtume ni ndani ya swala.

Uchache wa matamko ya kumswalia Mtume ni  kusema: ……………ALAAHUMMA SALLI ALAA MUHAMMAD

Matamko kamili ni kamili ni kama hayo yaliyomo ndani ya hadithi tuliyoitaja. Katika baadhi ya riwaya kuna zaida au pungufu.

Sharti za swala ya Mtume.

          Kumeshurutizwa katika kumswalia Mtume ndani ya Swala, kuchunga mambo yafuatayo:-

(i)                Ajisikilizishe mwenyewe matamko yake, iwapo hana matatizo ya usikivu.

(ii)              Iwe ni kwa tamko la “ Muhammad” au Rassul” au “An-nabiy”. Lau mtu atamswalai kwa kusema mathalan “Alaa Ahmad”, haitamjuzia.

(iii)            Iwe ni kwa Kiarabu.

Akishindwa, ataleta tafsiri yake kwa lugha yeyote aiwezayo LAKINI afahamu bado inamuwajibikia na kumlazimu kujifunza upesi imkinikavyo.

(iv)            Mtungamano (Utaratibu) wa matamko yake. Asiyacheleweshe matamko yaliyotangulia na kuyatanguliza yaliyocheleweshwa, bali ayatamke kama yalivyopokewa katika hadithi.

(v)              Mtungamano baina yake (swala ya Mtume) na Tashahudi. Haisihi kuanza  kumswalia Mtume kabla ya kusoma Tashahudi.

12.             SALAMU YA KWANZA.

Kutoa salamu ni ule ugeukaji wa kutumia shingo tu wa

mwenye kuswali kuliani kwake il-hali akisema…………ASSALAAMU ALAYKUM WARAHMATULLAH

Nguzo hii ni natija ya kauli ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie “ Ufunguo wa swala ni Twahara na Ihramu yake ni Takbiyra na ufunguzi wake ni Kutoa salamu”. Turmidhiy, Abuu Daawoud na wengineo.

Uchache wa salamu ni mtu kusema mara moja:

……………………………………… ASSALAAMU ALAYKUM

Ama ukamilifu wake ni kusema.

………………………………………. ASSALAAMU ALAYKUM WARAHMATULLAH

Mara mbili, mara ya kwanza kuliani na ya pili kushotoni.

Imepokelewa hadithi kutoka kwa Sa’ad – Allah amuwiye radhi – amesema : Nilikuwa nikimuona Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – akitoa salamu kuliani kwake na kushotoni kwake mpaka ninaona weupe wa kitefute (shavu) chake” Muslim.

13.             MTUNGAMANO (UTARATIBU) WA NGUZO HIZI KAMA ZILIVYOTAJWA.

Kutungamanisha nguzo za swala ni kuziratibisha kwa utaratibu wake kama zilivyo moja baada ya nyingine kila moja ikachukua nafasi yake bila ya kuitangulia nyingine. Kwa mantiki hii, mwenye kuswali analazimika kuianza swala yake kwa nia, halafu Takbiyra ya kuhirimia, kisha, asome Suratil-Faatiha, halafu arukuu, aitadili, asujudu……..na kuendelea kama hivi Angalia ikiwa mtu ataihamisha nguzo kwa makusudi kuitoa mahala pake ilipowekwa na sheria na kuipeleka mahala si pake, swala  yake nzima itabatilika, haikubaliwi. Ama akitenda hivyo bila ya kukusudia, basi swala yake itakuwa imebatilika kuanzia katika ile nguzo aliyoitenda mahala si pake na itamuwajibikia kuirudia swala yake tokea pale alipokosea tu. Kwa mantiki, iwapo mtu ataendela na swala yake baada ya kuwa ameshabadili utaratibu wa nguzo mpaka akafikia mahala alipopabadilisha katika rakaa iliyotangulia. Mathalann rukuu mpaka rukuu nyingine ya rakaa nyingine, nguzo shaihi ya rakaa hii ya sasa  itakaa mahala pa nguzo fasidi ya ile rakaa iliyotangulia. Kwa hivyo basi, itamuwajibikia azidishe rakaa moja, katika swala yake ili kuifidia ile rakaa iliyofisidika kwa kufisidika utaratibu wa nguzo.

(Allah ndiye Mjuzi mno wa lililo la sawa.)

Hizi ndizo nguzo za swala ambazo swala haisihi ila kwa kuzileta zote, tena kwa utaratibu huu tulioubainisha. Ni wajibu kwa mwenye kuvaana na ibada hii awaye yeyote, mwanamume wau mwanamke aihifahdi ibada hii kwa kuiteleza kwa ikhlasi, ufanisi  na unyenyekevu.

X/.     SUNA ZA SWALA.

          Muradi na makusudi ya suna za swala ni zile: kauli na matendo ambayo atakapoyasema au kuyatenda mwenye kuswali, atapata thawabu kutoka kwa Allah na kama hakuzisema kauli hizo au kuyatenda matendo hayo humfutu (hapati) thawabu. Na atastahili kulaumiwa kwa kuziacha kauli au matendo hayo kwa sababu Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – alikuwa akiyasema na kuyatenda.

Kama ambavyo swala ina nguzo na sharti zinazomlazimu mwenye kuswali kuzitekeleza kwa njia ya uwajibu ili swala  yake iweze kusihi. Kadhalika inazo suna ambazo mwenye kuswali anatakiwa azitekeleze LAKINI sio kwa njia ya UWAJIBU/ULAZIMA. Bali kuzitenda suna hizo hakutamaanisha kingine zaidi ya kurudufika na kuzidi thawabu za swala zake na kuacha hakumaanishi kupata dhambi: Suna hizi za swala ni nyingi baadhi ya Mafaqihi wamezichambua mpaka kufikia idadi yake khamsini . Suna zote hizi kwa ujumla wake zinagawanyika katika matapo/mafungu matatu yafuatayo:-

a.       Suna zilizo kabla ya Swala.

b.      Suna zilizo ndani ya swala.

c.       Suna zilizo baada ya swala.

a./.     SUNA ZILIZO KABLA YA SWALA.

Haya ni mambo ambayo mwenye kuswali anatakiwa kuyatenda kabla hajaingia ndani ya swala, haya hayazidi mambo matatu ambayo ni:

(i)                Adhana

(ii)              Iqaamah.

Inshaalah, tutazielezea adhana na Iqaamah kwa ufafanuzi wa kutosha katika somo la pili.

(iii)            Kuweka sitara mbele.

Ni suna kwa mwenye kuswali kuweka kitu mbele yake kitakachokuwa ni sitara baina yake na wale wapitao mbele yake. Sitara hii inaweza kuwa ni ukuta au nguzo ya msikiti, akaswali karibu na ukuta au nyuma ya nguzo. Au anaweza kuweka fimbo mble yake au kitu kingine mithili ya hivyo. Kama hakupata sitara kabisa, basi anaweza kuchora/kupiga mstari. Imepokelewa kutoka kwa Ibn Umar- Allah awaridhie kwamba Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – alikuwa anapotoka siku ya Eid (kwa ajili ya swala) huamrisha  (uletwe)  mkuki wake na huwekwe mbele yake, naye huswali kwa kuuelekea na il-hali watu (wakiswali) nyuma yake. Na hivyo ndivyo alivyokuwa akifanya awapo safarini. Bukhaariy na Muslim.

Na ni bora sitara ikawa karibu na mahala pake pa kusujudia. Hili linatokana na riwaya iliyopokelewa kutoka kwa sahli  Ibn Sa’ad – Allah amuwiye radhi – amesema: Ulikuwa (Umbali) wa baina ya muswala (mahala pa kusujudia) wa Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie na ukuta wa msikiti ni (kama) mapito ya mbuzi (nafasi awezayo kupita mbuzi). Bukhaariy na Muslim.


TUJIFUNZE NA TUKUBALI kuwa: kumuiga na kumfuata Mtume katika kauli na matendo yake ni amri ya Allah, tusome:” BILA SHAKA MANO MFANO MWEMA (wa kuiga) KWA MTUME WA ALLAH, KWA MWENYE KUMUOGOPA ALLAH NA SIKU YA MWISHO NA KUMTAJA ALLAH SANA” (33: 21)


Forum | Guestbook | Tuandikie |