|
i) MAANA YA NAJISI
Najisi ni neno la kiarabu lenye maana mbili; maana ya kilugha na ya kisheria.
Najisi katika lugha ni kila kilicho kibaya hata kama ni twahara kama vile
makamasi, makohozi, tongotongo na kadhalika. Maana hii ya najisi kilugha tunaipata katika
kauli ya Mola anaposema :
"ENYI MLIOAMINI ! HAKIKA WASHIRIKINA NI NAJISI
." [9:28]
Sote tunakubaliana kwa dalili zote; dalili nakala na dalili akili kwamba binadamu
yeyote ni kiumbe twahara lakini utaona kwenye aya hii Mola Mtukufu anawaita washirikina
kuwa ni NAJISI kwa sababu ya ubaya na uchafu wa nafsi zao katika katika kumshirikisha
MwenyeziMungu na viumbe alivoviumba mwenyewe.
Kwa darubini ya sheria najisi ni kila kitu kichafu ambacho kinazuia kusihi kwa
ibada kama vile swala, kutufu (twawafu) na kadhalika.
ii) WAJIBU WA KUJITWAHARISHA KUTOKANA NA
NAJISI
Imempasa na kumuwajibikia mwislamu kuutwahirisha mwili, nguo, mahala/sehemu alipo
na mazingira yake kwa ujumla kutokana na kila kilicho najisi kwa maana zote mbili kwani
hiyo ni amri ya MwenyeziMungu alipomwambia Mtume wake bali ummah mzima :
"NA NGUO ZAKO UZISAFISHE" [74:4]
MwenyeziMungu pia amewasifia waja wake ambao hujitahidi katika suala la usafi na
kujiepusha/kujilinda na najisi aliposema
"HAKIKA ALLAH HUWAPENDA WANAOTUBU NA HUWAPENDA WANAOJITAKASA" [2:22]
Katika kulisisitiza na kulitilia mkazo suala la twahara na kujiepusha na najisi
Bwana Mtume anatuambia :
"Twahara ni nusu ya imani"
Kadhalika Bwana Mtume amewaagiza na kuwaamrisha wanawake kujitwaharaisha kutokana
na damu ya hedhi kama alivotuamrisha sote kuondosha kila najisi.
iii) VITU VILIVYO NAJISI
Vitu vilivyo najisi ni pamoja na :
- Mfu/Mzoga ila mwanadamu, samaki na nzige.
- Kiungo cha mnyama kilichokatwa naye yu hai. Amesema Bwana Mtume :
"Kilichokatwa kwa mnyama na ilhali yu hai hicho (kilichokatwa) ni mzoga" Abu
Dawud.
- Damu, mkojo, kinyesi (mavi) ya wanadamu, wanyama au ndege.
- Nguruwe ! MwenyeziMungu anatuambia : "SEMA SIONI KATIKA YALE NILIYOFUNULIWA
MIMI KITU KILICHOHARIMISHWA KWA MLAJI KUKILA ISIPOKUWA KIWE NI MZOGA AU DAMU INAYOMWAGIKA
AU NYAMA YA NGURUWE KWANI HIYO NI UCHAFU
" [6:145]
- Mbwa kwa ushahidi wa hadithi isemayo "Mbwa atakaporamba chombo cha mmoja wenu
basi na akimwage (kilichomo ndani) kishe akikoshe (chombo) mara saba"
- Matapishi, usaha, maji ya madonda
- Wadii na Madhii. Wadii ni maji mazito yatokayo baada ya mkojo kutokana na kazi
ngumu/nzito. Madhii ni maji meupe yanayoteleza, haya hutoka wakati wa matamanio khafifu
(kwa mfano kuchezeana baina ya mwanaume na mwanamke). Matamanio yakiwa ya nguvu ndio
hutoka manii.
- Tembo/Pombe kwa aina zake zote. MwenyeziMungu anasema :
"ENYI MLIOAMINI ! BILA SHAKA ULEVI NA KAMARI NA KUABUDIWA ASIYEKUWA ALLAH NA
KUTAZAMIA KWA MSHARE YA KUPIGIA RAMLI (na kwa vinginevyo, yote haya) NI UCHAFU UTOKANAO NA
KAZI YA SHETANI. BASI JIEPUSHENI NAVYO ILI MPATE KUFAULU" [5:90]
- Maziwa ya mnyama asiyeliwa.
|