Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

SOMO LA PILI

Faida

ADHANA NA IQAAMA.

 

A: ADHANA

i) MAANA YA ADHANA:

 

Adhana ni neno la Kiarabu lenye maana mbili; maana ya kilugha na maana ya kisheria (kifiq-hi). Kilugha neno adhana lina maana ya “tangazo” kama lilivyotumika ndani ya Qur-ani Tukufu: “NA NI TANGAZO (adhana) LITOKALO KWA ALLAH NA MTUME WAKE, KUJUVYWA WATU SIKU YA HIJA KUBWA KWAMBA ALLAH YU MBALI NA WASHIRIKINA…..” (9:3)

“NA (tukamwambia): UTANGAZE (uadhini) KWA WATU HABARI ZA HIJA….” (22:27)

Ama maana ya adhana kisheria ni dhikri (utajo) maalum iliyowekwa na Uislamu kwa ajili ya kutangaza kuingia kwa wakati wa swala ya fardhi na kuwaita waislamu kuja kuswali.

 

  1. HUKUMU YA ADHANA:
  2.  

    Adhana ni suna kwa swala ya sasa (ya wakati huu) na swala iliyofutu (inayoswaliwa nje ya wakati wake). Kwa upande wa swala inayoswaliwa kwa jamaa adhana inakuwa ni SUNA KOKOTEZWA (Muakadah) kwa anjia ya kutoshelezeana. Yaani akiadhini mmoja miongoni mwao atakuwa amewatoshelezea wengine wote na suna hii, kwa hivyo haitalazimu kutolewa adhana nyingine. Ama kwa mtu anayeswali peke yake, yeye mwenyewe tu bila ya kuwa na wa pili yake, kwake huyu adhana itakuwa ni SUNA AINIYAH (yenye uzito wa fardhi).

    Adhana ina umuhimu mkubwa na uzito wa pekee katika kudhihirisha alama za kuadhimisha dini ya Allah.

     

  3. FADHILA ZA ADHANA:

 

Zimepokelewa hadithi kadhaa kutoka kwa Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – zinazofahamisha fadhila na thawabu adhimu zinazopatikana ndani ya adhana.

Miongoni mwa hadithi hizo ni kama zifuatavyo:

    1. Imepokewa kutoka kwa Abuu Hurayrah – Allah amuwiye radhi kwamba Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – amesema: “Lau watu wangelijua yaliyomo katika wito (adhana) na safu ya kwanza (ya swala ya jamaa) (yaani fadhila na thawabu adhimu zinazopatikana humo). Kisha wasipate (fursa hizo) ila kwa kupiga kura, basi wangelipiga kura.”
    2. Bukhaariy & Muslim

    3. Imepokelewa kutoka kwa Abuu Said Al-khudriy- Allah amuwiye radhi – amesema: Amesema Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie: “Utapokuwa katika (kundi la) mbuzi na kondoo wako (malishoni) au (utapokuwa) kitongojini mwako, ukaadhini kwa sababu (ya kuingia wakati wa) swala. Basi inyanyue sauti yako kwa wito huo (adhana) kwani hakika haisikii sauti ya muadhini jini wala mwanadamu wala kitu cho chote ila (sauti hiyo) itamshuhudia (mtu huyo) siku ya kiyama.”
    4. Bukhaariy

    5. Amesema Mtume wa Allah- Rehema na Amani zimshukie: “Bora ya waja wa Allah ni wale wachungao jua, nyota na vivuli (waadhini) kwa ajili ya dhikri ya Allah (swala).” Al-Haakim

 

  1. DALILI NA USHAHIDI WA ADHANA:
  2.  

    Adhana inapatikana ndani ya Qur-ani Tukufu na suna ya Mtume. Katika Qur-ani adhana inapatikana katika kauli ya Allah: “ENYI MLIOAMINI! KUKIADHINIWA KWA AJILI YA SWALA SIKU YA IJUMAA, NENDENI UPESI KUMTAJA ALLAH NA ACHENI BIASHARA….” (62:9) Na katika kauli ya Allah: “NA MANAPOITA KWENDEA SWALA (mnapoadhini) WANAIFANYIA MZAHA NA MCHEZO. HAYO NI KWA SABABU WAO NI WATU WASIO NA AKILI.” (5:58)

    Katika suna ya Mtume, adhana inaelezewa na kauli ya Mtume – Rehema na Amani zimshukie: “Unapoingia wakati wa swala, basi na akuadhinieni mmoja wenu na akuswalisheni aliye mkubwa wenu.” Bukhaariy & Muslim

    Kutokana na nukuu hizi za kitabu (Qur-ani) na Sunah (hadithi) uma wa Kiislamu umekongamana juu ya kwamba adhana imeshariiwa kwa swala tano za fardhi ili kuwajulisha waislamu kuingia kwa wakati wa swala husika.

     

  3. HISTORIA YA ADHANA (MWANZO WA ADHANA):
  4.  

    Kwa mujibu wa kauli zenye nguvu, adhana imeshariiwa katika mwaka wa kwanza wa Hijrah. Sababu ya kuanza kutumika kwa adhana ambayo haikuwepo katika kipindi chote cha utume Makah. Inatajwa kwamba baada ya Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – kufika Madinah, iliwawia uzito waislamu kujua nyakati za swala. Bwana Mtume akawataka shauri maswahaba wake wafanyeje ili swala ya jamaa isije ikawafutu. Baadhi ya maswahaba wakashauri ipigwe kengele kila unapoingia wakati wa swala. Wengine wakasema lipulizwe tarumbeta (baragumu) ili kuashiria kuingia kwa wakati wa swala. Na pia wako waliotoa ushauri uliokhitilafina na huu, lakini katika majumuisho yote ya ushauri uliotolewa hakuna uliompendeza Bwana Mtume. Akapendezwa na ushauri uliotolewa na Umar Ibn Al-Khatwaab – Allah amuwiye radhi. Imepokelewa kutoka kwa Naafi, kwamba Ibn Umar Allah awawiye radhi – alikuwa akisema: Waislamu walikuwa wakikutana na kukadiria nyakati za swala na hakukuwepo ye yote anayeita kwendea swala (anayeadhini). Siku moja wakalizungumzia suala hilo. Wakasema baadhi yao: Jifanyieni kengele kama wafanyavyo Manaswara. Na wengine wakasema: Bali tupulize baragumu kama Mayahudi. Basi (hapo ndipo) Umar aliposema: Kwa nini hamumpeleki mtu akanadi swala? Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – akasema: “Ewe Bilali inuka unadi swala.

    Bukhaariy

    Imamu Ahamd – Allah amrehemu – amepokea kwamba mmoja wa maswahaba nae ni Abdullah Ibn Zayd – Allah amuwiye radhi – alimuona malaika usingizini akamfundisha adhana na Iqaamah. (Alipoamka) akampa Mtume khabari ya ndoto yake hiyo. Mtume – Rehema na Amani zimshukie – akasema: “Bila shaka hiyo ni ndoto ya haki (kweli) pindipo akitaka Allah, basi inuka umfundishe Bilali maneno uliyoota ndotoni nae aadhini kwayo, kwani yeye ana sauti kali kuliko wewe”. Umar Ibn Al-Khatwaab akiwa nyumbani kwake akaisikia adhana hiyo, akatoka wanguwangu kuja kwa Mtume na kumwambia, namwapia yule aliyekutuma kwa haki, hakika nimeona usingizini haya haya aliyoyaona Abdullah Ibn Zayd”.

     

  5. TAMKO LA ADHANA (NAMNA YA KUADHINI):

 

Tamko na umbo la adhana ambayo Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – alimfundisha Abuu Mahdhuurah ni:-

ALLAAHU AKBAR X 4

ASH-HADU AN-LAA ILAAHA ILLAL-LAAH X 2

ASH-HADU ANNA MUHAMMADAN RASUULULLAAH X 2

(Kisha hufanya Tarjii (1) )

HAYYA ALAL-SWALAAH X 2

HAYYA ALAL-FALAAH X 2

Ikiwa ni adhana ya Alfajiri ataongeza:

AS-SWALAATU KHAYRUN MINAN-NAWM X 2

ALLAAHU AKBAR X 2

LAA ILAAHA ILLAL-LAAH X 1

 

Abuu Mahdhuurah – Allah amuwiye radhi amesema: Hakika Mtume wa Allah – Rehema na Amani zimshukie – alinifundisha adhana: Allaahu Akbar Allaahu Akbar Allaahu Akbar Allaahu Akbar, Ash-hadu An-laa Ilaaha Illal-laah, Ash-hadu An laa Ilaaha Illal-laah, Ash-hadu Anna Muhammadan rasuulullaah, Ash-hadu

Anna Muhammadan Rasuulullaah. Kisha hurudia akasema: Ash-hadu Ilaaha illal-laah (mara mbili) Ash-hadu Anna Muhammadan Rasuulullaah (mara mbili). Hayya Alas-swalaah (mara mbili) Hayya Alal-Falaah (mara mbili). Ikiwa ni swala ya Sub-hi nilisema: As-swalaatu khayrun minan-nawm. As-swalaatu khayrun minan-nawm. Allaahu Akbar Allaahu Akbar, Laa Ilaaha illal-laah”.

Tirmidhiy, Bukhaariy, Muslim & wengineo

 

MAANA YA MATAMKO YA ADHANA

 

Allaahu Akbar - Allah ni Mkubwa kuliko kila kitu.

Ash-hadu An-laa Ilaaha Illal-laah- Ninashuhudia kwamba hapana afaaye kuabudiwa kwa haki ila Allah pekee.

Ash-hadu Anna Muhammadan Rasuulullaah – Ninashuhudia kwamba Muhammad ni Mtume wa Allah.

Hayya Alas-swalaah – Njooni kuswali.

Hayya Alal-falaah – Njooni kwenye kufaulu.

Asswalaa tu khayrun Minan-nawm – Swala ni bora kuliko usingizi.

Allaahu Akbar – Allah ni Mkubwa kuliko kila kitu.

Laa Ilaaha Illal-laah – Hapana aabudiwaye kwa haki ila Allah.

 

(1) Tarji’i ni kuyarudia tena matamko hayo kwa sauti ya chini kidogo.

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: kuwa “WALE WANAOSIMAMISHA SWALA NA KUTOA ZAKAH, AMBAO WANA YAKINI NA AKHERA. HAO NDIO WALIO JUU YA UONGOFU UTOKAO KWA MOLA WAO, NA HAO NDIO WENYE KUFAULU”. [31:4-5]

 

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |