|
Ili
adhana iweze kusihi na kuzingatiwa kisheria kuwa
ni adhana kumeshurutizwa kupatikana sharti
zifuatazo:-
- UISLAMU:
Kisheria haisihi adhana kwa kafiri kutokana
na kutokuwa kwake na utayarifu/ustahiki wa
ibada (ahliyah). Kwa mantiki hii ni lazima
muadhini awe ni muislamu.
- UPAMBANUZI
(discrimination): Haisihi adhana kwa mtoto
mdogo ambaye bado hajafikia umri wa
upambanuzi. Kutokusihi huku kwa adhana ya
mtoto kunatokana na kutokuwa kwake na
utayarifu wa ibada na udhibiti wa wakati.
- UANAMUME:
Haisihi adhana ya mwanamke, kwa sababu
adhana haikushariiwa wala haikusuniwa kwake
bali imeharamishwa. Hii ni kutokana na
kuwepo uwezekano wa kufitinika wanaume na
sauti yake. Na hii pia ni mojawapo ya sababu
nyingi zinazomnyima uimamu mbele ya
mwanamume. Kama isivyosihi adhana ya
mwanamke, kadhalika haisihi adhana ya
“khuntha”-(Hermaphrodite) kwa sababu ya
kutokujulikana uanamume au uanamke wake. Kwa
mantiki hii ni lazima muadhini awe
mwanamume.
- UTARATIBU:
Ni sharti matamko ya adhana yaletwe kwa
mtungo na utaratibu wake kama yalivyopokewa
kutoka kwa Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie. Hii ni kwa sababu kuacha
utaratibu kunatuhumisha kufanya mchezo na
kupunguza uzito wa tangazo hili la kuingia
kwa wakati wa swala.
- MFULULIZO:
Ni sharti upatikane mfululizo baina ya
matamko ya adhana, kiasi cha kutopatikana
mwanya mkubwa baina ya tamko la kwanza na
lile la linalofuatia.
- KUINGIA
WAKATI WA SWALA: Haisihi adhana na ni haramu
kuadhini kabla ya kuingia wakati wa swala
husika, hili linatokana na kongamano (Ijmaa)
la mafaqihi. Kongamano hili linatokana na
kauli ya Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie: “Itakapohudhuria swala, basi na
akuadhinieni mmoja wenu”.
Bukhaariy
& Muslim
Ni
dhahiri kuwa swala haihudhurii ila kwa kuingia
wakati wake.
Ikiwa
adhana itatolewa nje ya wakati, kutalazimu
kuadhini tena utakapoingia wakati wa swala.
Hii ni kwa sababu adhana nje ya wakati inakosa
falsafa ya adhana ambayo ni kufahamisha
kuingia kwa wakati wa swala. Kwa mantiki hii
ni haramu kuadhini kabla ya kuingia kwa wakati
wa swala husika kutokana na kuwatatiza
(kuwachanganya) watu. Na kuwaongopea kwa
kungia wakati wa swala na ilhali bado
haujaingia.
TANBIHI:
Adhana ya swala ya Sub-hi haiguswi na sharti
hii ya kuingia kwa wakati. Kwani inajuzu
kuadhini baada ya kupita nusu ya usiku (usiku
wa manane) kama inavyofanywa leo Makkah na
Madinah. Hili ni natija ya riwaya ya Abdallah
Ibn Amrou-Allah amuwiye radhi-kwamba Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alisema:
“Hakika Bilali huadhini usiku, basi kuleni
na kunyweni mpaka muisikie adhana ya Ibn Ummu
Maktuum”. Bukhaariy
& Muslim
- IWE
KWA KIARABU: Ni sharti matamko yote ya
adhana yaletwe kwa lugha ya Kiarabu kama
yalivyopokelewa kutoka kwa Mtume wa Allah.
Haijuzu kutolewa adhana kwa lugha nyingine
yo yote isiyo Kiarabu, kwani hiyo haitakuwa
adhana bali tarjamah (tafsiri ya neno kwa
neno) ya adhana.
- KUWASIKILIZISHA
BAADHI YA WATU: Ni sharti adhana ya jamaa
itolewe kwa sauti inayoweza kusikiwa na watu
walio jirani na mahala inapotolewa. Ama
ikiwa ni adhana ya mtu anayeswali peke
(Munfarid) si sharti kunyanyua sauti, bali
adhana hiyo itolewe kwa sauti ya chini kiasi
cha kusikia muhusika pekee. Imepokewa kwamba
Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-alimwambia Abuu Said
Al-Khudriy-Allah amuwiye radhi: “Mimi
ninakuona wewe ni mpenzi wa mifugo na kuishi
mashambani. Utapokuwa pamoja na mifugo yako
au kitongojini kwako na ukaadhini kwa ajili
ya swala, basi inyanyue sauti yako kwa
wito huo (wa swala). Kwani hausikii upeo
wa sauti ya muadhini jini wala mwanadamu ila
(sauti hiyo) itamshuhudia siku ya Kiyama”.
Bukhaariy
TANBIHI:
Haikusuniwa adhana kwa jamaa ya wanawake, kwa
sababu ya fitina inayoweza kupatikana kutokana
na kusikilizika sauti zao na wanamume.
Iliyosuniwa kwao ni Iqaamah tu, kwa sababu
hekima (falsafa) yake ni kuwainua waliohudhuria
swala kuswali. Na haina kuinua sauti kama ilivyo
kwa adhana.
VIII/.
SUNA ZA ADHANA.
Kumesuniwa
katika adhana kufanya mambo yafuatayo:-
- KUELEKEA
QIBLAH: Ni suna muadhini kuelekea Qiblah
wakati wa kuadhini, kwa sababu bora ya pande
za kuelekewa kwa ajili ya ibada ni upande
uliyoko Qiblah. Na hakuna hata mmoja
anayeweza kuthubutu kukanusha uibada wa
adhana. Na isitoshe imethibiti kwamba
waadhini wa Bwana Mtume-Allah awawiye
radhi-walikuwa wakielekea Qiblah wakati wa
kuadhini.
- TWAHARA
YA HADATHI NDOGO NA KUBWA: Ni suna mtu
kuadhini hali ya kuwa yu katika hali ya
twahara, yaani hana hadathi ndogo
inayompasishia udhu wala ile kubwa
inayompasishia josho. Kwa maana hii, ni
karaha kuadhini mtu mwenye hadathi ndogo
(asiye na udhu). Na ukaraha unazidi zaidi
kiasi cha kuelekea kwenye uharamu kwa mtu
mwenye janaba (hadathi kubwa). Amesema Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie:
“Nachukia (sipendi) kumdhukuru Allah
Mtukufu ila niwe na twahara”.
Abuu
Daawoud & wengineo
- KUSIMAMA
WIMA: Ni suna mtu kuadhini hali ya kuwa
amesimama, hili linatokana na kauli ya
Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Ewe
Bilali simama unadi swala
(uadhini)”.
Bukhaariy
& Muslim
Ikiwa
mtu ana udhuru kama ugonjwa akisimama
ataanguka au maumivu yatazidi, basi ataadhini
kwa kukaa kwa sababu: “ALLAH HAIKALIFISHI
NAFSI YO YOTE (kutenda) ILA YALIYO SAWA NA
UWEZA WAKE...” [2:286]
- KUGEUZA
SHINGO KULIANI NA KUSHOTONI: Miongoni mwa
suna za adhana kama zilivyothibiti kutoka
kwa Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie.
Ni pamoja na muadhini kugeuza shingo yake
kuliani wakati wa kusema: (Hayya
alas-swalaah) na kushotoni anaposema: (Hayya
Alal-falaah). Imepokewa kwamba Abuu
Juhayfah-Allah amuwiye radhi-amesema:
“Nilimuona Bilali akiadhini, nikawa
ninaufuatilia mdomo (kinywa) wake huku na
huko. (Akageuka)
kuliani na kushotoni (wakati wa kusema):
Hayya Alal-swalaah, Hayya Alal-falaah”.
Bukhaariy
- KUFANYA
TARJI’I: Ni suna muadhini kuleta matamko
ya shahada mbili. Yaani (Ash-hadu An-laa
Ilaaha Illal-laahu) na (Ash-hadu Anna
Muhammadan Rasuulullaah) kwa siri (sauti ya
chini), kabla ya kuyajihirisha (kuyatamka
wazi/kwa sauti). Suna hii imethibiti katika
hadithi ya Abuu Mahdhuurah-Allah amuwiye
radhi-kama ilivyopokelewa na Imamu
Muslim-Allah amrehemu: “...Kisha hurudia
(hufanya Tarji’i) akasema: Ash-hadu An-laa
Ilaaha Illal-laah...”
- KURATILI
MANENO YA ADHANA (KUYALETA KWA NJIA/MTINDO
WA TARTIYLI): Ni katika jumla ya suna mtu
kuadhini kwa “Tartiyli”. Yaani ayatamke
maneno ya adhana kwa mtungo wa utuvu mithili
ya mtu aimbaye kidogo. Na si kutetea kwa
kuivuta mno sauti kiasi cha kutokueleweka
maneno au kuharibika herufi. Hili linatokana
na kuizingatia adhana kuwa ni tangazo la
kuwajulisha walio mbali kuingia kwa wakati
wa swala. Ikawa mtindo huu wa “Tartiyli”
ni fasaha zaidi katika kufikisha tangazo kwa
walengwa.
- KULETA
“TATH-WIYBU” KATIKA ADHANA YA ALFAJIRI:
“Tath-wiybu” ni muadhini kusema baada ya
(Hayya alal-falaah x2); ASWALAATU KHAYRUN
MINAN-NAUM, mara mbili.
Amesema
Bilali-Allah amuwiye radhi: Aliniamrisha Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kuleta
“Tath-wiybu” katika adhana ya Alfajiri”.
Ahmad,
Abuu Daawoud & wengineo
- SAUTI
KALI (INAYOFIKA MBALI) NA NZURI: Ni suna
muadhini kuwa na sauti kali na nzuri
itakayomudu kuulainisha moyo wa msikilizaji
na kumpelekea kuuitika wito huo. Suna hii
inatokana na kauli ya Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-alipomwambia Abdullah Ibn
Zayd-Allah amuwiye radhi-ambaye ndiye
aliyeiona adhana usingizini: “Inuka/simama
pamoja na Bilali, umtamkishe (maneno)
uliyoyaona (usingizini) na aadhini kwayo. Kwani
yeye ana sauti kali kuliko wewe”.
Abuu
Daawoud & wengineo
- TABIA
NJEMA: Muadhini anapaswa kutangaa baina ya
watu kwa tabia njema na uadilifu. Hii ni kwa
sababu tabia njema na uadilifu huwapelekea
watu kumsadiki anapowapa khabari ya wakati
(adhana).
|