Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

SUNA ZA ADHANA                         Inaendelea

 

10. KUTOKUTETEA: Ni suna kuacha kutoa adhana kwa kutetea, yaani kuvuta mno sauti kiasi cha kupelekea kuharibika kwa maana au kutokueleweka maneno. Adhana isigeuzwe nyimbo ambapo mtu hughani upeo wa sauti yake, hilo ni karaha.

 

11. WAADHINI WAWILI: Ni suna msikiti kuwa na waadhini wawili kwa ajili ya swala ya alfajiri. Mmoja ataadhini kabla ya kuingia kwa alfajiri na mwingine baada ya alfajiri. Suna hii imethibiti kutokana na hadithi (riwaya) ya Abdullah Ibn Amrou-Allah amuwiye radhi: “Hakika Bilali huadhini usiku, basi kuleni na kunyweni mpaka muisikie adhana ya Ibn Ummu Maktuum”. Bukhaariy & Muslim

Falsafa ya adhana nje ya wakati ni kwa ajili ya kuwaamsha watu kujiandaa na kujitayarisha kwa ajili ya swala, hiyo ndio ilikuwa adhana ya Bilali. Lakini kunatakikana kwa muadhini huyu anayeadhini nje ya wakati kuwa na wakati mmoja ili kuepuka kuwatatiza na kuwachanganya watu. Kama ada yake ni kuadhini saa kumi kamili, basi siku zote aadhini ndani ya wakati huo. Sio leo kaadhini saa kumi, kesho saa tisa na keshokutwa saa kumi na nusu.

 

12. KUNYAMAZA (KUKAA KIMYA): Ni suna kwa mwenye kusikia adhana kukaa kimya na kuisikiliza adhana hiyo na kusema mithili ya anavyosema muadhini. Dalili ya usuna huu ni kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Mtapousikia wito (wa swala), basi semeni mithili ya asemavyo muadhini”. Bukhaariy & Muslim

Lakini wakati muadhini ataposema: “HAYYA ALAS-SWALAAT X2, HAYYA ALAL-FALAAH X2”. Yeye mwenye kumsikia atasema: “LAA HAWLA WALAA QUWWATA ILLA BILLAAH”. Haya ni sehemu ya mafundisho ya hadithi: “Na (muadhini) ataposema: Hayya alas-swalaah, aseme (anayemsikia): Laa hawla walaa quwwata illa billaah. Na ataposema: Hayya alal-falaah, aseme: Laa hawla walaa quwwata illa billaah”. Bukhaariy & Muslim.

Ama katika “Tathwiybu”- yaani muadhini anaposema: “Asswalaatu khayrun mina-naumu” katika swala ya alfajiri, ni suna amjibu kwa kusema: “Swadaqta wabararta”.

 

13. KUOMBA DUA NA KUMSWALIA MTUME BAADA YA ADHANA: Kunasuniwa kwa wote wawili; muadhini na mwenye kumsikia muadhini kumswalia Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-mara tu baada ya kumalizika kwa adhana. Kisha waombe dua iliyopokewa kutoka kwa Mtume na akatuhimiza sana kuisoma kila baada ya adhana. Haya yote ni kwa mujibu wa hadithi iliyopokewa na Abdullah Ibn Amrou-Allah amuwiye radhi-kwamba yeye alimsikia Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akisema: “Mtakapomsikia muadhini, basi semeni mithili ya asemavyo kisha niswalieni. Kwani hakika mwenye kuniswalia mimi swala moja (tu), Allah atamswalia (mtu huyo kwa swala moja) hiyo swala kumi. Kisha niombeeni “wasiyla” kwa Allah, kwa sababu hiyo wasiyla ni daraja/cheo cha peponi. Haitakikani daraja/cheo hicho ila kwa mja miongoni mwa waja wa Allah na ninataraji kuwa mimi ndiye (mja huyo). Basi ye yote atakayeniombea wasiyla huo, umemuhalalikia (ameupata) uombezi wangu (siku ya kiyama)”. Muslim & wengineo

Na dua inayotakiwa kusomwa baada ya adhana ni kama ilivyopokelewa na swahaba Jaabir-Allah amuwiye radhi-kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Atakayesema wakati (anapomaliza) kusikiliza adhana: ALLAAHUMMA RABBA HAADHIHID-DA’AWATIT-TAAMMAH, WASSWALAATIL-QAAIMAH, AATI SAYYIDANAA MUHAMMADAN AL-WASIYLAH WAL-FADHWIYLAH, WAB-ATH-HU MAQAAMAN MAHMUUDANIL-LADHIY WA’ADTAHU, umemuhalalikia uombezi wangu siku ya kiyama”. Bukhaariy & wengineo.

MAANA YA MATAMKO YA DUA:

Allaahumma: Ewe Mola wa haki wee!

Rabba haadhihid-da’awatit-taammah: Bwana wa wito huu (wa Tauheed) uliotimia (usoingiliwa na mabadiliko).

Aati sayyidanaa Muhammadan: Ninakuomba umpe Bwana wetu Muhammad.

Al-wasiylah: Wasila (Ukaribu na Allah/daraja peponi).

Wal-fadhwiylah: cheo chenye kuzidi viumbe wote.

Wab-ath-hu: na umpe

Maqaaman mahmuudah: uombezi mkubwa siku ya kiyama.

Alladhiy wa’adtahu: ambao uliomuahidi.

Ahadi hii ya Allah kwa mtume aliye kipenzi chake imo katika kauli yake: “...HUENDA MOLA WAKO AKAKUINUA CHEO KINACHOSIFIKA”. [17:79]

Muadhini anatakiwa kumswalia Bwana Mtume na kuomba dua kwa sauti ya chini na sio kwa sauti kama ile aliyoitumia katika kuadhini. Isije kuchukuliwa na kudhaniwa kwamba hiyo swala ya mtume na dua ni sehemu ya adhana. Ni vizuri kwa muadhini mwenye kutumia kipaaza sauti kumswalia Bwana Mtume na kuomba dua baada ya kuzima kipaaza sauti hicho.

 

14. UUNGWANA, UKUBWA, WEMA NA UJUZI WA WAKATI:

Kumesuniwa Muadhini kuwa:-

Muungwana (huru), yaani asiwe mtumwa anayeweza kuzuiwa na bwana wake kutoka kwenda kuadhini.

Mkubwa (mtu mzima) mwenye akili timamu anayejua anachokifanya, asiwe mtoto mdogo ambaye hajabaleghe bado.

Mtu mwema, mwenye tabia njema, anayekubalika na jamii, asiwe mtu fasiki mwenye mambo ya hovyo hovyo.

Mjuzi wa nyakati za swala.

Suna hii ni kama ilivyothibiti katika hadithi ya Ibn Abbas-Allah amuwiye radhi: “Akuadhinieni aliye mbora wenu na akuswalisheni msomi wenu zaidi wa Qur-ani”.

TANBIHI: Isieleweke kwamba haisihi adhana ya mtumwa wala mtoto mdogo, wakiadhini adhana yao itasihi lakini si suna kwao kuadhini kama wapo watu wenye sifa.

 

15. UONI WA MUADHINI: Ni suna muadhini kuwa mtu mwenye kuona, asiwe kipofu kwani kipofu hajui wakati ila kwa msaada. Lakini kipofu akiadhini adhana yake itasihi kwa sababu Ibn Ummu Maktuum (swahaba wa Mtume aliyekuwa kipofu) alikuwa akimuadhinia mtume wa Allah. Amesema Ibn Amrou katika riwaya iliyopokelewa na Imamu Bukhaariy: “(Ibn Maktuum) alikuwa ni mtu kipofu, hanadi swala mpaka aambiwe: kumekucha kumekucha”.

 

16. KUWEKA VIDOLE MASIKIONI: Kumesuniwa kuweka vidole masikioni wakati wa kutoa adhana, kwa sababu kufanya hivyo kuna msaada mkubwa katika kunyanyua sauti. Usuna huu wa kuweka vidole masikioni wakati wa kuadhini unatokana na riwaya iliyopokewa na Imamu Abuu Haniyfah-Allah amrehemu-“Kwamba Bilali aliadhini na akaweka vidole vyake masikioni”. Bukhaariy & Muslim.

Kadhalika imepokelewa kutoka kwa Sa’ad; muadhini wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-“Kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimuamrisha Bilali kuweka vidole vyake katika masikio yake na akasema: Hakika kufanya hivyo kunaiinua zaidi sauti yako”. Ibn Maajah, Al-Haakim, Twabaraaniy & Ibn Adiy.

 

17. KUJITOLEA (KUTOKUADHINI KWA UJIRA): Ni suna mtu kuadhini kwa kutaraji ujira kutoka kwa Allah, asichukue ujira kwa kazi hiyo. Hili ndilo kongamano la wanazuoni wote, hii ni kwa sababu Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimwambia Uthmaan Ibn Abul-Aaswi: “Na umuweke muadhini asiyechukua ujira kwa adhana yake”. Abuu Daawoud, Ibn Maajah & Tirmidhiy.

TANBIHI: Ikiwa watu wataifanya adhana kuwa ni kazi maalumu kama zilivyo kazi nyingine, basi kutajuzu kuchukua ujira kwa kazi hiyo kwa mujibu wa makubaliano ya uongozi wa msikiti husika na muadhini aliyeajiriwa.

 


 

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |