|
Hii ndio hali ya pili ya swala
ya khofu. Katika hali hii ya kuuma kwa vita,
hakuna namna maalumu ya swala iliyopokelewa,
bali kila mtu anatakiwa kuswali kwa namna
inavyomkinikia. Ataswali huku akipigana akienda
kwa miguu au akiwa amepanda mnyama. Kadhalika
anaweza kuswali akiwa anatembea bila ya kupigana
au akiwa amesimama. Katika hali hii anaruhusiwa
kuswali kwa kuelekea upande inakotokea khatari,
ni mamoja imesibu kuwa ndio upande wa Qiblah au
la. Na atayafanya matendo ya rukuu na sijida kwa
kuotezea yaani kwa kukitukutisha kichwa chake
hali ya kushiria hiyo rukuu na sijida.
Yatakikana kuotezea kwa sijida kuwe ni zaidi
kuliko kuotezea kwa rukuu ili kufarikisha au
kutofautisha baina ya viwili hivyo; sijida na
rukuu. Ikiwamkinikia kufuatana na kuswali jamaa
pamoja itakuwa ni bora hata kama
watakhitalifiana kimuelekeo, huyu kaelekea huku
na yule kaelekea kule au maamuma akamtangulia
imamu wake. Kuhusiana na haya tunasoma:
“ANGALIENI SANA SWALA (zote kuziswali, khasa
jamaa) NA (khasa) ILE SWALA YA KATI NA KATI. NA
SIMAMENI KWA UNYENYEKEVU KATIKA KUMUABUDU ALLAH.
NA KAMA MKIWA NA KHOFU (kuswali kidasturi; mmo
katika kupigana, basi swalini) NA HALI YA KUWA
MNAKWENDA KWA MIGUU AU MMEPANDA (wanyama). NA
MTAKAPOKUWA KATIKA AMANI, BASI MKUMBUKENI ALLAH
(swalini) KAMA ALIVYOKUFUNZENI YALE MLIYOKUWA
HAMUYAJUI”. [2:238-239]
Imamu Bukhaariy amepokea riwaya
kutoka kwa Ibn Umar-Allah awawiye radhi-katika
kuitaja kwake swala ya khofu. Baada ya kuzitaja
aina mbili zilizotangulia (kuelezwa katika darsa
iliyopita) akasema: Na khofu ikiwa bado ni kubwa
kushinda hivyo, waliswali hali ya kuwa
wanakwenda kwa miguu au hali ya kupanda
(wanyama), wakiwa wameelekea Qiblah au wakiwa
hawakuelekea. Imamu Maalik akasema: Amesema
Naafii: Simuoni Abdullah Ibn Umar kuwa kayataja
hayo (aliyoyataja) ila ni kutoka kwa Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie.
Katika hali hii ya mapambano
husamehewa harakati na matendo anayoyafanya
mwenye kuswali kwa kulazimishwa na hali hiyo ya
vita, matendo na harakati ambazo hazisameheki
katika hali ya amani. Maneno na ukelele, hivi
havisameheki kwa sababu hakuna dharura
inayohitajisha kufanya hivyo. Katika hali hii
mtu akipatwa na najisi isiyosameheka kama vile
damu na mfano wake, swala yake itakuwa ni sahihi
lakini kutamuwajibikia kuikidhi baadae akiwa
katika hali ya amani.
Ni vema ukatambua kwamba aina
hii ya swala tuliyoitaja imeruhusiwa kuswaliwa
kwa kaifia hii katika kila vita vya kisheria. Na
katika mazingira ambayo mtu anakuwa na khofu
kubwa, kama wakati anamkimbia adui au mnyama
mkali. Kilichozingatiwa katika kuwekwa sheria ya
kuswali kwa namna hii iliyokhalifiana na
ada/dasturi ya swala ni kuchunga kuitekeleza
swala katika wakati wake uliowekwa na sheria.
Hii yote ikiwa ni kuamrika na kauli yake Allah
isemayo: “...KWA HAKIKA SWALA KWA WAUMINI NI
FARDHI ILIYOWEKEWA NYAKATI MAKHSUSI”. [4:103]
FALSAFA/HEKIMA YA KUSHARIIWA
(KUWEKWA SHERIA) SWALA YA KHOFU.
Falsafa/hekima pekee ya
kushariiwa swala ya khofu ni kumfanyia mja
wepesi ili aweze kuitekeleza nguzo hii kuu ya
dini katika hali na mazingira yo yote yale. Ili
kuonyesha kuwa Uislamu ni dini inayokwenda
sambasamba na maumbile ya mwanadamu: “BASI
UELEKEZE USO WAKO KATIKA DINI ILIYO SAWA
SAWA-NDILO UMBILE ALLAH ALILOWAUMBIA WATU (yaani
dini hii ya Kiislamu inawafikiana barabara na
umbo la binadamu) HAKUNA MABADILIKO KATIKA
MAUMBILE YA VIUMBE VYA ALLAH. HIYO NDIO DINI
ILIYO HAKI, LAKINI WATU WENGI HAWAJUI”.
[30:30]
Kadhalika swala hii ya khofu ni
kielelezo cha wazi kinachoonyehsa wepesi wa dini
hii ya Kiislamu kama alivyosema Allah:
“...ALLAH ANAKUTAKIENI YALIYO MEPESI WALA
HAKUTAKIENI YALIYO MAZITO....” [2:185]
“...WALA HAKUWEKA JUU YENU
MAMBO MAZITO KATIKA DINI (nayo dini hii) NI MILA
YA BABA YENU IBRAHIMU...” [22:78]
Pia kwa kuzingatia kuwa swala ni
mawasiliano na kiungo baina ya mja na Mola wake
ikawekwa swala hii ya khofu ili mja asikatikiwe
na mawasiliano na Mola wake katika kipindi hiki
kigumu ambacho anayahitajia zaidi mawasiliano
hayo. Kupitia mawasiliano hayo amuombe Mola wake
nusra na ushindi dhidi ya maadui wake
aliojisabilia maisha yake katika kupambana nao.
Ndani ya mawasiliano hayo atamtaja Bwana Mlezi
wake, utajo ambao utampa utulivu wa moyo na
makini ya akili, vitu ambavyo ni nyenzo muhimu
sana katika uwanja wa mapambano. Ni utulivu na
umakini huu ndivyo vitakavyomuwezesha kupanga
mikakati na mbinu zitakazomsaidia na
kumuhakikishia ushindi. Tusome na tuamini:
“...SIKILIZENI! KWA KUMKUMBUKA
(kumtaja/kumdhukuru) ALLAH NYOYO HUTULIA”.
[13:28] Isitoshe kumdhukuru Allah katika hali
ngumu hii ya vita ni sababu kuu ya ushindi na
nusra, tusome na tuamini tukitaka: “ENYI
MLIOAMINI! MKUTANAPO NA JESHI (la makafiri)
KAZANENI BARABARA (wala msikimbie) NA MUMKUMBUKE
ALLAH KWA WINGI ILI MPATE KUFAULU”. [8:45]
HITIMISHO:
SWALA HAIPOMOKI KWA HALI YO YOTE
ILE IWAYO.
Inabainika kutokana na maelezo
yote haya yanayoitaja swala ya khofu kwamba
swala haipomoki kwa hali yo yote ile iwayo
maadam mtu ana akili timamu. Si mwendawazimu na
ni mkubwa si mtoto mdogo. Hivi ndivyo kusema
kuwa mja hana udhuru wo wote utakaompa kibali
cha kuacha kuswali, hilo lingelikuwepo basi
angelikipata kibali hicho katika hali ya vita.
Kilichoruhusiwa si kuacha kuswali bali ni wepesi
wa kuswali kwa mujibu wa mazingira na hali
aliyomo mtu. Msafiri kwa mfano ameruhusiwa
kujumuisha swala mbili iwe ni mjumuisho wa
kutanguliza au ule wa kuakhirisha na kukusuru
yaani kuziswali swala za rakaa nne, rakaa mbili
mbili badala ya nne. Hakuambiwa asiswali eti kwa
kuwa tu yumo safarini bali Uislamu kwa kuutambua
uzito na taabu ya safari ukampa wepesi wa namna
fulani katika kuitekeleza nguzo hii ya swala.
|