|
3.
SHARTI ZA SAFARI ILIYORUHUSIWA KUKUSURU NA
KUJUMUISHA NDANI YAKE.
Msafiri
hapati rukhsa ya kukusuru au kujumuisha swala
ndani ya safari mpaka kwanza safari yake hiyo
itimize sharti tatu zifuatazo:-
I.
MASAFA YA KILOMETA THEMANINI NA MOJA
(80km) NA KUENDELEA: Ni sharti safari iwe ndefu
inayoanzia kilometa themanini na moja na
kuendelea. Kwa matazamo wa sheria haiwi ni
safari, safari iliyo chini ya masafa haya. Hiyo
haitakuwa ni safari inayopata rukhsa hii ya
kujumuisha au kukusuru. Imepokelewa kwamba Ibn
Umar na Ibn Abbas-Allah awawiye radhi-walikuwa
wakikusuru swala na wakifuturu (wakila mchana wa
Ramadhan) katika (safari ya umbali wa)
‘burudi’ nne, ambazo ni sawa na
‘farsakh’ kumi na sita (zilizo sawa na
kilometa themenini na moja takriban). Walikuwa
wakifanya hivyo kutokana na elimu/ujuzi
walioupata kutoka kwa Mtume-Rehema na Amani
zimshukie.
II.
MUELEKEO WA SAFARI (DESTINATION): Rukhsa
ya kukusuru au kujumuisha haitapatikana mpaka
safari husika iwe na muelekeo maalumu. Kwamba
mtu anasafiri kutoka sehemu fulani kwenda sehemu
fulani, yaani kuwepo kituo cha kuanzia na
kumalizikia safari. Isiwe mtu yumo safarini
anakwenda tu bila ya kujua safari itakomelea
wapi. Mfano wa mtu anayemtafuta mtu/kitu
kilichopotea au askari anayemfuata kamanda wake
bila ya kujua anakwenda wapi. Hawa na kama hawa
hawapati rukhsa ya kukusuru/kujumuisha mwanzoni
mwa safari yao ila baada ya kusafiri umbali wa
kilometa themanini na moja. Katika umbali huo
ndio wataanza kupata rukhsa ya kujumuisha/kukusuru
swala.
III.
UHALALI WA SAFARI: Ili safari iambatane
na rukhsa hii ya kujumuisha/kukusuru swala ni
lazima iwe na malengo halali. Lengo la safari
lisiwe limefungamana na maasi kwa namna yo yote
ile iwayo. Ikiwa mtu anasafiri kwa ajili ya
biashara haramu (kama
kuuza/kutangaza ulevi), kwenda kupokea
riba/rushwa au kufanya unyang’anyi njiani na
kadhalika. Huyu/hawa kisheria sio wasafiri na
hiyo sio safari.
KIAMBATISHI.
KUJUMUISHA
SWALA KWA SABABU YA MVUA.
Sheria
inampa muislamu rukhsa ya kujumuisha swala mbili
mjumuisho
wa
kutanguliza kwa sababu ya mvua. Rukhsa hii ni
zao la riwaya iliyopokelewa kutoka kwa Ibn Abbas-Allah
awawiye radhi-kwamba Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-aliswali Madinah rakaa saba na rakaa
nane: Adhuhuri na alasiri (rakaa nane), na
maghribi na ishaa (rakaa saba) bila ya kuwepo
khofu wala safari. Bukhaariy & Muslim.
Na
katika riwaya aliyopwekeka nayo Imamu Bukhaariy:
Alisema Ayoub-mmoja wa wapokezi wa hadithi hii:
Huenda ilikuwa katika usiku wa mvua? Akasema (Ibn
Abbas): Labda/huenda.
Rukhsa
hii ya kujumuisha kwa sababu ya mvua inahusisha
tu ujumuishaji wa kutanguliza na si ujumuishaji
wa kuakhirisha. Hii ni kutokana na kuwepo
uwezekano wa kukatika kwa mvua wakati ule wa
swala ya pili na hivyo kumfanya kuwa ameitoa
swala ya kwanza katika wakati wake bila ya
udhuru. Ujumuishaji huu kwa sababu ya mvua
umeshurutiziwa sharti zifuatazo:-
1)
Swala inayojumuishwa iwe ni swala ya
jamaa inayoswaliwa katika msikiti wa mbali.
Msikiti ambao kama mtu ataamua kuuendea
atafika akiwa ametota kabisa au kuchafuka
kutokana na tope la njiani au kupata maudhi ya
aina yo yote ile. Marejeo ya umbali, yanaachiwa
ada/desturi ya mahala husika.
2)
Kudumu/kuendelea kunyeesha kwa mvua
mwanzo wa swala mbili hizo na wakati wa kutoa
salamu ya swala ya kwanza. Kwa maneno mengine
hivi ni sawa na kusema kuwa swala ya mwanzo
miongoni mwa swala mbili hizo zinazojumuishwa
iswaliwe yote ndani ya mvua yaani wakati mvua
ikiendelea kunyeesha.
4.
SWALA YA KADHAA (KUKIDHI SWALA ZILIZOPITA).
Miongoni
mwa nembo na alama ambazo ni kielelezo cha
muumini wa kweli ni kuswali swala katika nyakati
zake zilizowekwa na sheria. Kwa kuitekeleza
kauli ya Allah Mola Muumba wake: “...KWA
HAKIKA SWALA KWA WAUMINI NI FARDHI ILIYOWEKEWA
NYAKATI MAKHSUSI”. [4:103] Kwa mujibu wa
kauli hii ya Allah, muislamu atakapoiakhirisha
swala mpaka ukatoka wakati wake bila ya kuiswali
ndani ya wakati wake huo, atakuwa amefanya
dhambi kubwa. Nini kinachofuatia baada ya mtu
kupitwa na swala? Mafaqihi wamekongamana na
kuwafikiana kwamba itakayemfutu (itakayempita)
swala, kunamlazimu kuikidhi (kukidhi swala ni
kuiswali nje ya wakati wake). Kwa mfano mtu
iliyomfutu swala ya adhuhuri na ukaingia wakati
wa alasiri, kutamlazimu mtu huyo kuswali swala
ya adhuhuri iliyomfutu kabla ya kuiswali ile ya
alasiri. Hii ni kwa sababu utaratibu katika
swala tano za fardhi ni suala la wajibu. Kwa
maana hii basi, kumalizika kwa wakati wa swala
iliyofutu (adhuhuri) hakuupomoshi utaratibu
baina yake na swala ya sasa (alasiri). Angalia utaratibu hautafuatwa wala kuzingatiwa iwapo tu swala
ilimfutu kwa sababu ya kusahau kunakozingatiwa
na sheria. Au kwa kudhikika (kuwa finyu) wakati
wa swala ya sasa (alasiri), kiasi kwamba kama
ataanza kuswali adhuhuri, wakati wa alasiri
utakuwa umetoka na kuingia maghribi na hivyo
kuifanya hii alasiri nayo kuwa ni kadhaa ya pili.
Au kuwa swala zilizofutu ni zaidi ya swala sita
au mtu kukumbuka kuwa hajaswali alasiri mathalan,
wakati yumo ndani ya swala ya maghribi. Katika
hali na mazingira yote haya utaratibu
hautazingatiwa.
Ni
haramu kwa mtu ambaye anawiwa na swala za fardhi
zilizomfutu kujishughulisha kuswali swala za
suna, bali anapaswa kuutumia muda huo wa kuswali
suna kuzikidhi swala hizo za fardhi zilizomfutu.
Angalia anaweza kuswali suna andamizi za swala (Qabliyah
na Ba’adiyah) na suna kokotezwa (Muakadah)
kama witri na rakaa mbili za kabla ya alfajiri.
Kadhalika anaweza kuswali swala ya Eid na swala
zote za suna zilizopata hukumu ya ‘suna
kokotezwa’.
Kadhalika
kunampasa mtu aliyefutiwa swala na wakati wake
kutoka, kuiswali swala hiyo wakati wa kuikidhi
kwa namna yake iliyopasa. Ikiwa ni swala ya
jahriyah ataiswali kwa jahra (kwa kutoa sauti)
na ikiwa ni swala ya siriyah ataiswali kwa
kuisirisha (bila ya kutoa sauti).
HITIMISHO:
Imekongamana
na kuwafikiana Jumuhuri ya ulamaa wa madhehebu
zote kwamba mtu mwenye kuacha swala
anakalifishwa kuikidhi swala hiyo aliyoiacha.
Taklifu hii itamuandama bila ya kujali kuwa
aliiacha swala kwa kusahau au kwa makusudi
lakini pamoja na upambanuzi wa hali mbili hizo;
kusahau na kusudi. Iwapo mtu aliiacha swala kwa
udhuru unaozingatiwa kisheria kama kulala au
kusahau. Huyu hapati dhambi na wala hakumlazimu
kukidhi haraka bila ya kuchelewa. Ama yule
mwenye kuiacha bila ya udhuru, yaani kaacha
kuswali kwa makusudi tu, huyu pamoja na kupata
dhambi kutamuwajibikia kukidhi haraka bila ya
kuchelewa.
Dalili/ushahidi
wa kukidhi swala ni kauli yake Bwana
Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Atakayelala
(akapitwa) na swala au akaisahau, basi na
aiswali atakapoikumbuka, haina kafara (swala
iliyoachwa) ila hiyo”. Bukhaariy, Muslim
& wengineo.
Kauli
ya Bwana Mtume (haina kafara ila hiyo), ndio
inayofahamisha kwamba hapana budi kuikidhi swala
ya fardhi iliyofutu, kwani hiyo ndio njia pekee
ya kumvua mja na dhima ya swala iliyomfutu.
|