Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Fiqh na Sheria  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

V) HUKUMU YA MWENYE KUACHA SWALA

Faida

    Mtu mwenye kuacha swala ama Taarikuswalaat kama anavyojulikana katika sheria.  Huyu ama atakuwa ameiacha swala kwa uvivu tu na uzembe au atakuwa ameiacha kwa kuipinga kuwa si wajibu na kuiona kuwa si cho chote. Hukumu  ya mtu huyu kisheria inaiandamia sababu ya kuacha kwake swala. Kwa mantiki hii mtu mwenye kuacha swala kwa kupinga na kukanusha uwajibu wa swala kwake au kwa kuifanyia shere. Huyu kwa upingaji wake huu ana kuwa ni KAFIRI na ANATOKA KATIKA UISLAMU.  Sheria inamuwajibisha kiongozi kumuamrisha muacha swala huyu kutubia, akikubali kutubia baada ya kutakwa toba na akasimamisha swala itakiwavyo. Atarejea kuwa muislamu na hivyo kupata kinga ya nafsi na mali yake, yaani itakuwa si halali kuuliwa. Kama hakukubali kutubia, kiongozi ataamuru kuuliwa na atauliwa hali ya kuwa ni murtadi (ametoka katika Uislamu). Baada ya kuuawa si jaizi kukoshwa, kukafiniwa (kuvikwa sanda) wala kumswalia.  Kama isivyojuzu kumzika katika makaburi ya waislamu kwa sababu yeye si miongoni mwa waislamu.

     Ama mtu akiiacha swala kwa uvivu tu huku akiitakidi kuwa ni wajibu kwake.  Huyu atakalifishwa kuikidhi swala aliyoiacha na kutubia kutokana na maasi ya kuacha swala mbele ya kiongozi.  Kama hakuinuka kutekeleza amri ya kiongozi ya kukidhi swala, atauwawa kwa “haddi” (penalty). Yaani kutazingatiwa kuuawa kwake ni kutiwa adabu kwa mujibu wa sheria kama wanavyotiwa adabu maasi wengine (mzinifu, mwizi na kadhalika). Huyu atazingatiwa kuwa ni muislamu baada ya kuuawa, kwa hivyo atatendewa yote wana yotendewa waislamu. Ataoshwa, atakafiniwa, ataswaliwa na kuzikwa katika makaburi ya waislamu kwa sababu ni mmoja wao.

     Imepokelewa kutoka kwa Ibn Umar–Allah awawiye radhi–kwamba Mtume wa Allah–Rehema na Amani zimshukie–amesema: “Nimeamrishwa nipigane na watu mpaka Washuhudie kwamba hapana apasaye/afaaye kuabudiwa kwa haki ila Allah, na washuhudie kuwa Muhammad ni Mtume wa Allah. Na wasimamishe swala, na watoe Zakah. Wakiyatekeleza hayo watakuwa wamezihifadhi kwangu damu zao na mali zao ila kwa haki ya Uislamu   na hisabu yao ni juu ya Allah”.  Bukhaariy & Muslim

Hadithi hii inafahamisha kwamba mtu aliyekiri na kutamka shahada mbili atapigwa/atauwawa kama hakusimamisha swala na wala hawi kafiri.  Dalili na ushahidi wa hili ni ile riwaya iliyopokelewa kutoka kwa Ubaadah Ibn As-swamit–Allah amuwiye radhi–amesema: Nilimsikia Mtume wa Allah–Rhema na Amani zimshukie–akisema: “Swala tano amezifaradhisha Allah kwa waja wake, atakayezitekeleza bila ya kupoteza cho chote katika  hizo swala kwa sababu ya kuikhafifisha haki yake. (Huyu) atakuwa na ahadi mbele ya Allah ya kumuingiza peponi.  Na asiyezitekeleza, hatakuwa na ahadi mbele ya Allah, akitaka atamuadhibu (kwa kuacha kwake swala) na akitaka atamuingiza peponi”.  Abuu Daawoud & wengineo.                         Hadithi hii pia inafahamisha kuwa muacha swala hawi kafiri, kwa sababu kama angelikuwa kafiri asingeliingia katika kauli ya Mtume: “...na akitaka atamuingiza peponi.” Kwa maana kafiri haingii katu peponi, kwa hivyo ikachukuliwa kuwa huyu ni yule aliyeiacha swala kwa uvivu. Hili linatokana na mjumuisho wa dalili.

Imepokelewa hadithi kutoka kwa Jaabir–Allah amuwiye radhi– amesema: Nilimsikia Mtume-Rehema na Amani zimshukie–akisema: “Hakika baina ya mtu na shirki na ukafiri ni kuacha swala.” Muslim & wengineo.

Hadithi hii inachukuliwa juu ya kuacha swala kwa kupinga ufaradhi wake na kuikanusha au kuicheza shere na kuiona kuwa si cho chote.

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: kuwa watu wa peponi watawauliza wenzao wa motoni: “NI KIPI KILICHOKUPELEKENI MOTONI? WASEME: HATUKUWA MIONGONI MWA WALIOKUWA WAKISWALI.”     (74:42-43)

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |