|
Maamuma
anayeswali nyuma ya imamu kumeshurutizwa sharti
kadhaa ili kumfuata kwake imamu kusihi. Miongoni
mwa sharti muhimu ni kama zifuatavyo:-
1)
Mfuataji (maamuma) asijue kubatilika kwa
swala ya imamu wake au kuitakidi hivyo.
Mfano: Watu wawili wamefanya jitihadi katika kujua upande kilipo Qiblah. Kila
mmoja wa wawili hawa akaitakidi kwamba Qiblah
kiko upande ule auonao yeye na wala hakiko
upande auonao mwenzake. Katika hali kama hii
hakujuzu kwa mmojawapo wa wawili hawa
waliokhitalifiana katika upande kilioko Qiblah,
jambo ambalo ni mojawapo ya nguzo za swala.
Hakumjuzii kumfuata mwenzake
akamfanya kuwa ndio imamu wake na yeye
akawa maamuma nyuma yake. Kutokujuzu huku
kunatokana na ile itikadi ya kila mmoja wa
wawili hawa kwamba mwenzake amekosea
welekea/upande wa Qiblah. Sasa basi, maadam
amekosea Qiblah basi na swala yake anayoiswali
kuelekea upande huo itakuwa sio sahihi, ni
batili tu na si vinginevyo kwa itikadi yake
hiyo.
2)
Imamu asiwe umiyi (asiyejua kusoma wala
kuandika) na ilhali maamuma ni msomi:
Muradi wa makusudio ya “umiyi”, hapa ni
mtu asiyeweza kuisoma vizuri Suratil-faatihah
(Al-hamdu) kwa hukumu zake za usomaji kama
zilivyotajwa katika vitabu vya fani ya
“Tajweed”. Angalia ikiwa imamu na maamuma
wote ni maumiyi, basi kutamjuzia kila mmoja wao
kumfuata mwenzake.
3)
Imamu asiwe mwanamke na maamuma akawa ni
mwanamume:
Mwanamke hana mamlaka kisheria kumtangulia
mwanamume katika swala, akawa ndio imamu
wa mwanamume. Hili ndilo agizo la Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-katika kauli
yake: “Mwanamke asimswalishe mwanamume”. Ibn
Maajah-Allah amrehemu.
XI/.
NAMNA YA KUFUATA:
Kufuata
kulikoelezwa na sheria hakutathibiti ila kwa
sharti na namna ambazo inatakikana kwa mwenye
kufuata (maamuma) kuzichunga. Sharti hizi ni
nyingi, tunazifupiliza kama ifuatavyo:-
1)
Maamuma asimtangulie imamu wake katika
mahala pa kusimama (masimamo):
Ili ufuataji usihi ni sharti maamuma
asimtangulie imamu wake katika masimamo.
Akimtangulia, ufuataji wake umebatilika kwa
mujibu wa kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie: “Kwa yakini imamu amewekwa ili
afuatwe” – (na sio kutanguliwa).
Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
Ni dhahiri kuwa kufuata hakupatikani ila atakapokuwa mfuataji (maamuma)
yu nyuma ya afuatwaye (imamu). Lakini haidhuru
maamuma kulingana sawa na imamu wake katika
masimamo, ijapokuwa ni
karaha
kufanya hivyo kwani suna ilivyo ni kuwa nyuma
yake kidogo. Maamuma akimtangulia imamu wake,
akawa yeye ndio yuko mbele na imamu nyuma, hapo
swala yake itabatilika tu na si vinginevyo. Na
mazingatio katika suala la
kutangulia au kuakhirika ni kisigino.
Hiki ndicho kinachoangaliwa, kisigino cha
maamuma kikiwa mbele ya kisigino cha imamu,
maamuma huyo atazingatiwa kuwa kamtangulia imamu
wake. Na kikiwa nyuma, huyo anazingatiwa
kumfuata imamu wake.
Namna
ya kusimama nyuma ya imamu:
Maamuma wakiwa ni wawili na kuendelea ,
watapiga safu nyuma ya imamu wao. Maamuma akiwa
ni mmoja, ni yeye tu na imamu wake, anatakiwa
kusimama kuliani kwa imamu nyuma kidogo.
Akiongezeka mtu wa pili, huyu atasimama
kushotoni kwa imamu, kisha maamuma wawili hawa
watarejea nyuma walingane sawa. Au imamu wao
atasogea mbele kidogo ili kuwapa wao nafasi ya
kulingana sawa. Imepokelewa kutoka kwa
Jaabir-Allah amuwiye radhi-amesema: “Niliswali
nyuma ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-nikasimama kuliani kwake. Halafu akaja
Jaabir Ibn Swakhri akasimama kushotoni kwake
(Mtume). (Bwana Mtume) akatushika mikono sote na
kutusimamisha nyuma yake”. Muslim-Allah
amrehemu.
Kumesuniwa kutokuzidi umbali ulio baina ya
imamu na maamuma wake zaidi ya dhiraa tatu na
hivi ndivyo itakiwavyokuwa baina ya kila safu
mbili. Angalia maamuma wakiwa ni mchanganyiko
unao wachanganya pamoja wanamume na wanawake.
Katika hali hii maamuma wanamume watasimama
nyuma ya imamu na wanawake watakuwa nyuma ya
wanamume. Haya ni katika jumla ya mafundisho ya
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kama
yalivyo katika kauli zake zifuatazo:-
v
“Bora
ya safu za wanamume ni ile ya kwanza yao na
shari (mbaya) yake ni ile ya mwisho yao (hizo
safu za wanamume). Na bora ya safu za wanawake
ni ile ya mwisho yao na shari yake ni ile ya
mwanzo yao (inayoifuatia ile ya mwisho ya
wanamume)”. Muslim-Allah amrehemu.
v
Anas-Allah
amuwiye radhi-amesema kwamba Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimswalisha
yeye na mama yake. Akanisimamisha mimi kuliani
kwake na akamsimamisha
mwanamke (mama yangu) nyuma yetu”.
Muslim-Allah amrehemu.
TANBIHI:
Ama
jamaa ya wanawake, yaani jamaa inayowahusisha
wanawake watupu tu peke yao bila ya kuwemo
miongoni mwao mwanamume. Imamu wao; mwanamke
mwenziwao atasimama katikati yao, kama
lilivyothibiti hili kutoka kwa bibi Aysha na
bibi Ummu Salamah-Allah awawiye radhi.
Ni
karaha maamuma kusimama peke yake katika safu,
yaani kuanza safu peke yake bila ya kuwa na
mwenzake. Imepokelewa na Waabiswah kwamba Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimuona mtu
akiswali nyuma ya safu peke yake, akamwambia:
“Ewe mswali pweke, kwani usiunge safu (ya
mbele yako) ukaingia katikati yao au ukamvutia
kwako mtu mmoja ikiwa mahala pamekudhikikia
akasimama pamoja nawe! Wewe huna swala (swali
tena)”. Twabaraaniy-Allah amrehemu.
Kwa
hivyo basi utaona kuwa ni suna kwa huyu aliye
pweke kumvuta mtu mmoja kutoka katika safu iliyo
mbele yake baada ya kuhirimia ili aje kusimama
pamoja nae. Kadhalika ni suna kwa huyu mwenye
kuvutwa kumsaidia ndugu yake kwa kurejea nyuma
kusimama naye ili apate fadhila za kusaidiana
katika wema: “...NA SAIDIANENI KATIKA WEMA NA
TAQWA...” [5:2]
2)
Maamuma amfuate imamu wake katika
vihamohamo (maguroguro) vyake na katika baki ya
nguzo vitendo nyingine.
Maamuma kumfuata imamu maana yake ni
kuchelewa kuanza kwa kitendo chake, yaani
kitendo chake kitanguliwe na kile cha imamu
wake. Hivi ndivyo alivyotufundisha Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-kupitia kauli
yake: “Kwa yakini imamu amewekwa ili afuatwe,
akikabiri (akileta takbir) basi nanyi (ndipo)
mkabiri na wala msikabiri mpaka (kwanza) akabiri
yeye. Na akirukuu nanyi rukuuni na wala msirukuu
mpaka arukuu yeye. Na ataposujudu nanyi sujuduni
na wala msisujudu mpaka asujudu yeye”. Ahmad
& Abuu Daawoud-Allah awarehemu.
Na kauli yake hii: “Enyi watu! Mimi ndio
imamu wenu, basi msinitangulie kwa kurukuu, wala
kwa kusujudu wala kwa kusimama, wala kwa kukaa
na wala kwa kutoa salamu”. Ahmad &
Muslim-Allah awarehemu.
Angalia na uzingatie kwamba kumtangulia imamu ni jambo lililokemewa
vikali sana na Mtume wako, hata akafikia kusema:
“Ehee hachelei mmoja wenu anaponyanyua kichwa
chake kabla ya imamu, Allah kukigeuza kichwa
chake kuwa kichwa cha punda. Au Allah kuigeuza
sura yake sura ya punda”.
Bukhaariy & Muslim-Allah amrehemu.
Lakini maamuma akiwa nyuma ya imamu wake
kwa nguzo moja, hilo litakuwa ni karaha. Na
iwapo atachelewa nyuma ya imamu wake kiasi cha
nguzo mbili ndefu, sura ya hili ni kama vile
imamu kurukuu, kuitadili, kisha akasujudu na
kuinuka kutoka sijida ya kwanza. Akayafanya yote
haya na ilhali maamuma ameendelea kusimama bila
ya udhuru wo wote, swala yake itabatilika. Ama
ikiwa kuchelewa kwake huko ni kwa sababu ya
udhuru mithili ya uzito katika kusoma Al-hamdu.
Basi kunamuelea kuwa nyuma ya imamu wake kwa
nguzo tatu. Iwapo nguzo tatu hizi hazitoshi
kumpa nafasi ya kukamilisha
kisomo chake cha Al-hamdu na kisha
kumfuata imamu wake. Hapa sasa kutamuwajibikia
kukata hapo alipofikia na amfuate imamu wake,
kisha atadiriki kilichobakia baada ya imamu wake
kutoa salamu.
|