Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Fiqh na Sheria  

"Mwenyezi Mungu akimtakia kheri Mja humfahamisha (humpa elimu) kwenye dini" Hadith Tukufu

XI. NAMNA YA KUFUATA      (Inaendelea)...

 

 

3. Maamuma kujua vihamohamo/maguroguro ya Imamu wake:

    Maamuma ni sharti avijue vihamohamo vya Imamu wake, ama kwa kumuona yeye mwenyewe akitoka qiyamu kwenda rukuu, kutoka rukuu kuja itidali na kutoka hapo kuporomokea sijida na kadhalika. Au kwa kuiona safu ya mbele yake au kwa kumsikia mbalighishaji.

4. Kisiwepo baina ya Imamu na maamuma kitenganishi eneo kikubwa:

     Ikiwa jamaa inaswaliwa nje; mawandani mahala ambapo si ndani ya jengo la msikiti. Kumeshurutizwa kisiwepo baina ya Imamu na maamuma wake kitenganishi eneo kikubwa. Ama wakiwa ndani ya msikiti, ufuataji utakuwa ni sahihi vyo vyote yatakavyombalika masafa baina yao au kuingia kati majengo yenye kupitika. Yaani mtu anaweza kutoka jengo moja hadi jingine. Ama Imamu na maamuma wote wawili wakiwa nje ya msikiti, au imamu akawa msikitini na maamuma nje yake. Katika hali na mazingira kama haya kumeshurutizwa kutombalika masafa baina ya imamu na maamuma wake.

5. Maamuma anuie jamaa au kumfuata imamu:

    Ni sharti nia ya jamaa au kumfuata imamu ikutanishwe pamoja na Takbira ya kuhirimia swala. Angalia iwapo maamuma ataacha kuleta nia ya kufuata na kisha akamfuata imamu katika vihamohamo na matendo, swala yake maamuma huyo itabatilika ikiwa alikusudia kumfuata. Kwani ilivyo ndivyo ni amgonjee mgonjeo mwingi kwa ada, kwa sura ambayo mtazamaji ataona kuwa hizo ni swala mbili tofauti; haziko katika mtungo mmoja. Ama kukisadifu kufuatana bila ya kukusudia au kumngojea kwake imamu kukawa ni kuchache, swala yake haitabatilika kwa matendo yake haya.

Kwa upande wa maamuma, si wajibu kwake kunuia “uimamu”, bali yapendekeza tu kufanya hivyo ili aweze kuzihodhi fadhila za jamaa. Kwani kama hakunuia hatazipata fadhila hizo za jamaa, hili linatokana na ukweli kwamba mtu hapati ujira ila wa alilolinuilia. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “Hakika si vinginevyo, matendo yote yamefungamana na nia, na kwa yakini kila mtu atapata alilolinuilia...”. Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.

Elewa kuwa maamuma atapata fadhila za jamaa maadam imamu hajatoa salamu. Na maamuma kuidiriki takbiratul-ihraam pamoja na imamu wake, kuna fadhila za pekee kabisa. Fadhila hizi hupatikana kwa maamuma kujishughulisha kuleta takbiratul-ihraam mara tu baada ya kuhirimia imamu wake. Na fahamu kuwa rakaa itamthibitikia maamuma pale tu atakapomdiriki imamu wake katika rukuu, nae akarukuu pamoja nae kabla imamu hajainuka kutoka rukuu (Qiyaamu). Hivi ndivyo inavyoelezwa na kauli ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Mtapoijia swala na ilhali sisi tumesujudu, basi nanyi sujuduni na wala msiihesabu hiyo (sijida) kuwa ni sehemu (ya swala yenu). Na atakayediriki rukuu, hakika ameidiriki rakaa”. Abuu Daawoud-Allah amrehemu.

 

BAADHI YA MAS-ALA YANAYOFUNGAMANA NA SWALA YA JAMAA:

 

1.     Kunyoosha safu na kuziba mianya:

Kumesuniwa kwa Imamu kuwaamrisha maamuma wake kunyoosha safu zao na kuziba mianya baina yao, hili lifanyike baada ya Iqaamah na kabla ya kuhirimia swala. Imepokelewa kutoka kwa Anas-Allah amuwiye radhi-kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akituelekea kwa uso wake kabla hajakabiri (Takbiratul-Ihraam), akituambia: “Kamataneni barabara na mlingane sawa, na zisawazisheni safu zenu kwani kusawazika kwa safu ni katika jumla ya utimilifu wa swala”. Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.

2.    Imamu kufanya takhfifu:

Kumesuniwa imamu awakhafifishie swala maamuma wake, asitwawilishe (asirefushe) swala kiasi cha maamuma kuona dhiki mioyoni mwao. Hivi ndivyo anavyotuagiza Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-katika hadithi iliyopokelewa na Abuu Hurayrah-Allah amuwiye radhi: “Atapowaswalisha mmoja wenu watu basi na akhafifishe (asifanye swala kuwa ndefu kupita kiasi), kwani miongoni mwao (hao maamuma) kuna walio dhaifu, wagonjwa na watu wazima. Na mtu akiswali peke yake na atwawilishe atakavyo (awezavyo)”. Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.

3.     Imamu atwawilishe rakaa ya kwanza na amsubiri anayemuhisi kutaka kuunga jamaa ili aweze kuidiriki jamaa:

Imamu ameruhusiwa na sheria kutwawilisha rakaa ya kwanza kwa ajili ya kumngojea mwenye kutaka kuunga jamaa ili kumpa fursa ya kudiriki fadhila za jamaa. Kama ambavyo kumesuniwa kwa imamu kumngojea mtu aliyemuhisi kuingia naye akiwa katika rukuu au katika kikao cha mwisho. Imepokelewa hadithi kutoka kwa Abuu Qataadah-Allah amuwiye radhi-kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akitwawilisha rakaa ya kwanza. (Akasema Abuu Qataadah): Tukadhania kwamba yeye amewakusudia kwa hilo watu waidiriki rakaa ya kwanza. Na imepokewa na Abuu Said-Allah amuwiye radhi-amesema: Swala ilikuwa ikikimiwa, mtu akaenda ‘Baqiy’ akakidhi haja yake, akatawadha kisha akaja na ilhali Mtume wa Allah akiwa (bado) katika rakaa ya kwanza kutokana na jinsi anavyoitwawilisha. Ahmad, Muslim, Ibn Maajah & Nasaai-Allah awarehemu.

4.    Mtanguliwa (masbuuq) kujiunga na imamu:

Mtu atapoingia msikitini na kukuta swala imesimama tayari, kutamuwajibikia kujiunga upesi na imamu katika hali yo yote aliyomkuta. Ni mamoja akimkuta katika rukuu, sijida, kitako au qiyamu (kisimamo). Hivi ndivyo inavyoeleweka kutokana na kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Mmoja wenu atapoijia swala na imamu akiwa katika hali fulani, basi na afanye kama afanyavyo Imamu”. Tirmidhiy-Allah amrehemu.

5.    Hakujuzu (hakuruhusiwi) swala ya suna itakapokimiwa swala ya faradhi:

Si rukhsa mtu kuswali swala ya suna ikimiwapo swala ya faradhi. Angalia swala hiyo ya faradhi ikikimiwa na tayari mtu yumo ndani ya swala ya suna, ataikata swala hiyo ya suna na kwenda kujiunga na swala ile ya faradhi. Ukataji huu ni iwapo haijafungamana rakaa kwa kuinuka kutoka rukuu na iwapo imeshafungamana ataitimiza katika hali ya ukhafifu. Yote haya yamekusanywa na kauli ya Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Itapokimiwa swala, basi hapana (rukhsa ya kuswali) swala (ya suna) ila ile ya fardhi tu”. Muslim-Allah amrehemu.

Mpenzi msomaji wetu, ni vema ukafahamu kwamba swala ya jamaa ina vipengele chungu nzima ambavyo kunakupasa kuvijua. Hivi tulivyovigusia kwa mukhtasari ni vichache tu miongoni mwa hivyo kathiri (vingi). Kwa kulizingatia hili, Website yako; WEBSITE UISLAMU inakushauri kujiunga na masomo ya dini katika eneo unaloishi. Ili uweze kuipata kokwa ya elimu na khasa kwa kujifunza lugha ya Qur-ani Tukufu (Kiarabu). Endelea kuwa nasi na zidi kutuombea taufiq kwa Allah ili tuzidi kukutumikia.

 


 

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |