|
Katika
kushariiwa swala ya Ijumaa kuna hekima na faida
kathiri (nyingi). Katika jumla ya faida hizo ni
kule kukutana waislamu katika ngazi ya mji,
kitongoji au kijiji mahala pamoja. Ambapo ni
ndani ya msikiti wa Ijumaa, mara moja kila juma,
mara nne kila mwezi na mara khamsini takriban
kila mwaka. Hii ni fursa muhimu na ya pekee
ambayo huwaunganisha waislamu na kuzidisha nguvu
yao kama ambavyo huwazidishia kuzoeana,
kufahamiana na kusaidiana. Ijumaa ni idhaa ya
waislamu yenye dhima kuu ya kuwapasha
waislamu matukio ya kila juma yanayojiri katika
ulimwengu wao. Idhaa hii huwanganisha waislamu
na matukio haya na kuwaonyesha nafasi yao kama
waislamu nyuma ya matukio hayo. Ni kwa kiasi
gani matukio hayo yanawadhuru au kuwanufaisha
waislamu na wao kama waislamu wafanye nini
kuyaboresha manufaa au kuyaondosha madhara
yatokanayo na matukio hayo. Ijumaa ni chuo
cha nidhamu kinachowafundisha waislamu kuwa
ni lazima wawe nyuma ya kiongozi wao mmoja,
wakimtii na kumsikiliza katika maamrishi na
makatazo, ikiwa wanataka kufaulu kama
walivyofaulu maswahaba nyuma ya kiongozi wa uma;
Bwana Mtume. Ijumaa ni chuo cha usawa kinachoondosha
tofauti za rangi, lugha, hadhi na hali za
kimaisha baina ya waislamu. Katika swala ya
Ijumaa utamuona tajiri bilionea amekaa pembeni
ya masikini hohehahe, kiongozi yuko bega kwa
bega na raia wake duni, mkubwa amekaa sambamba
na mdogo na hata mweupe na mweusi pia hukaa
pamoja. Hakuna nafasi maalum kwa tabaka la watu
fulani, bali kila muislamu ana haki ya kukaa po
pote na hakuna mwenye haki ya kumuondoa. Ila
aamue yeye mwenyewe kwa khiari yake kusogea au
kumpisha nduguye muislamu, hili ni suala binafsi
la matashi ya mtu. Hii ni sehemu ya falsafa kuu
ya swala hii ya siku ya Ijumaa.
V/.
SHARTI ZA KUWAJIBISHA SWALA YA IJUMAA
(WANAOWAJIBIKIWA NA IJUMAA):
Swala
ya Ijumaa kwa mujibu wa sheria ni wajibu kwa mtu
ambaye zimepatikana kwake sharti saba
zifuatazo:-
- Uislamu:
Swala
ya Ijumaa ni wajibu kwa muislamu tu na wala
haimuwajibikii kafiri kwa kuwa hana sifa ya
Ijumaa, ambayo ni Uislamu.
- Baleghe:
Swala
ya Ijumaa inamuwajibikia mtu mzima
aliyefikia umri wa baleghe. Kwa maana hiyo,
swala ya Ijumaa si wajibu kwa mtoto mdogo;
aliye chini ya umri wa baleghe.
- Akili
timamu: Inamuwajibikia
swala ya Ijumaa mtu mzima mwenye akili
timamu. Kwa hivyo basi, mwendawazimu
hawajibikiwi na swala hii ya Ijumaa.
- Uhuru
kamili (Uungwana): Swala
ya Ijumaa si wajibu kwa mtumwa
anayezingatiwa na sheria. Hii ni kwa sababu
ya kushughulishwa kwake na haki ya utumwa
kwa bwana wake. Haki hii ya bwana wake ndio
inayomnyima uwajibu wa swala ya Ijumaa.
- Uanamume:
Ijumaa
si wajibu kwa wanawake wa Kiislamu kwa
sababu ya kushughulika kwao na ulezi wa
watoto na shughuli za nyumbani. Pia Ijumaa
si wajibu kwao kutokana na imkani
(uwezekano) ya kupatikana mashaka kwao kwa
sababu ya ule uwajibifu wa kuhudhuria katika
wakati na mahala maalum.
- Siha
(afya) ya kiwiliwili: Swala
ya Ijumaa si wajibu kwa mgonjwa ambaye
anapata maumivu (machungu) kutokana na
harakati za kuhudhuria msikitini au kukaa
msikitini mpaka kumalizika kwa swala. Pia
anapewa hukumu ya mgonjwa mtu ambaye
anamuuguza na kumtumikia mgonjwa na pakawa
hapana mtu wa kumshikia zamu wakati wa
kwenda msikitini. Huyu bila ya kuangalia
mgonjwa ni ndugu au si ndugu yake wa nasabu,
haimuwajibikii swala ya Ijumaa maadam
mgonjwa anahitajia huduma yake.
- Ukazi
wa mahala pa Ijumaa: Ijumaa
si wajibu kwa msafiri aliyesafiri safari ya
halali ijapokuwa ni ile inayohusisha rukhsa
ya kukusuru. Hukumu hii ni iwapo safari yake
ilianza kabla ya kuchomoza kwa alfajiri ya
siku ya Ijumaa.
Sharti
saba hizi za uwajibifu wa swala ya Ijumaa ambazo
ni: Uislamu, baleghe, akili timamu, uungwana,
uanamume, siha ya mwili na ukaazi wa mji. Zote
hizi zinatokana na kauli hizi za Bwana
Mtume-Rehema na Amani zimshukie:-
ü
“Ijumaa
ni haki ya wajibu juu ya kila muislamu
katika/pamoja na jamaa ila watu wanne:
·
mtumwa
aliyemilikiwa, au
·
mwanamke,
au
·
mtoto
mdogo, au
·
mgonjwa”.
Abuu Daawoud-Allah amrehemu.
ü
“Ye
yote mwenye kumuamini Allah na siku ya mwisho
(muislamu), basi imemuwajibikia Ijumaa ila
mwanamke, msafiri, mtumwa na mgonjwa”.
Daaruqutwniy na wengineo-Allah awarehemu.
VI/.
SHARTI ZA KUSIHI KWA SWALA YA IJUMAA:
Zikipatikana
sharti saba hizi tulizozitaja, swala ya Ijumaa
itakuwa tayari ni wajibu kwa muhusika ila tu
itakuwa haisihi ila kwa kupatikana sharti nne
zifuatazo:-
- Kuwa
ndani ya mipaka ya mji: Ili
Ijumaa isihi kisheria ni wajibu isimamishwe
ndani ya mipaka ya mji, kitongoji au kijiji
chenye wakazi wasiopungua arobaini [40]
ambao kwao swala ya Ijumaa ni wajibu. Kwa
mantiki hii, swala ya Ijumaa haisihi
mawandani, kambini (mahala walipopiga
makhema) wala katika kijiji ambacho kina
watu walio chini ya idadi ya wanaopasiwa na
Ijumaa. Lakini watu wa kijiji hiki wakisikia
adhana ya swala ya Ijumaa inayotolewa katika
kijiji kilicho jirani yao, kutawawajibikia
kutoka kwenda kuswali swala ya Ijumaa katika
kijiji jirani hicho. Na kama hawaisikii
adhana ya kijiji jirani, basi Ijumaa
itaendelea kuwa sio wajibu kwao.
Dalili/ushahidi
wa sharti hii:
Swala
ya Ijumaa katika zama zake Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-na pia katika zama za
makhalifa waongofu-Allah awawiye
radhi-haikuswaliwa ila ndani ya mipaka ya mji.
Pembezoni mwa Madinah yalikuwepo makabila ya
mabedui, haikuthibiti hata katika hadithi dhaifu
kwamba waliswali Ijumaa au Bwana Mtume
aliwaamrisha kuswali. Kadhalika pamoja na
kukithiri kwa safari za Mtume wa Allah nje ya
Madinah, katu haikuthibiti kwa riwaya sahihi
kwamba aliiswali swala ya Ijumaa safarini. Huu
ndio ukweli, zingatia!
- Kupatikana
watu arubaini:
Idadi
ya watu wanaojumuika kwa ajili ya swala ya
Ijumaa na ambao kwao Ijumaa ni wajibu isipungue
watu arubaini. Watu arubaini hawa wawe ni
wanamume, watu wazima, wakazi wa mji husika.
Dalili
ya sharti hii ya pili:
v
Imepokelewa
kutoka kwa Jaabir Ibn Abdillah-Allah amuwiye
radhi-amesema: Suna ya Mtume imepita kwamba
katika kila (idadi ya watu) arubaini na
kuendelea ni Ijumaa (hiyo).
v
Imepokelewa
na Ka’ab Ibn Maalik-Allah amuwiye radhi-kwamba
wa mwanzo aliyewaswalisha Ijumaa ni As’ad Ibn
Zaraarah-Allah amuwiye radhi-na wakati huo
walikuwa ni watu arubaini.
TANBIHI:
Elewa
na ufahamu ewe mpenzi ndugu msomaji wetu kwamba
kuna makindano baina ya wanazuoni katika kadhia
hii ya idadi ya watu inayofungamana nayo Ijumaa.
Ni arubaini, ama ni kumi na mbili au ni watu
watatu, rejea vitabu vya Fiq-hi kwa ufafanuzi wa
kina na rejea vema dalili za kila upande.
|