|
3.
Iswaliwe katika wakati wa swala ya Adhuhuri:
Ni
sharti swala ya Ijumaa iswaliwe ndani ya wakati
wa Adhuhuri ndipo iweze kusihi. Wakati wa swala
ya Adhuhuri ukidhikika kiasi cha kutosalia
kitambo cha kutosha kuiswali swala ya Ijumaa
ndani ya kipindi hicho kabla ya kuingia kwa
wakati wa swala ya Alasiri. Katika hali kama hii
kutawawajibikia hawa waliodhikiwa na wakati
kuiswali Ijumaa adhuhuri rakaa nne badala ya
mbili kama ambavyo ingeswaliwa ndani ya wakati.
Lau watu wataingia kuiswali swala ya Ijumaa,
wakati wa Adhuhuri ukatoka na ilhali wao bado
wangali ndani ya swala hiyo; hawajaimaliza. Hapa
wataigeuza swala ya Ijumaa kuwa Adhuhuri na
kutimiza rakaa nne kwa nia ile ile ya Ijumaa
waliyoanza nayo.
Dalili
ya sharti hii:
Dalili
na ushahidi huu wa sharti hii ya tatu ya kusihi
kwa Ijumaa ni kitendo chake Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-kuiswali swala
ya Ijumaa ndani ya wakati huo wa Adhuhuri. Haya
ni kama yanavyofahamika kupitia hadithi
zifuatazo:-
I.
Imepokelewa kutoka kwa Anas-Allah amuwiye
radhi-kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-alikuwa akiswali swala ya Ijumaa wakati
jua linapopinduka”. (Na huo ni wakati
wa Adhuhuri kwani jua halipinduki ila wakati
huo). Bukhaariy-Allah amrehemu.
II.
Imepokelewa kutoka kwa Salamah Ibn
Al-Ak-waa-Allah amuwiye radhi-amesema: “Tulikuwa
tukiswali pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-swala ya Ijumaa. Kisha
tukiondoka (kurudi majumbani) na ilhali kuta
zikiwa hazina kivuli tunachoweza kujikinga nacho”.
Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
III.
Imepokelewa kutoka kwa Sahli Ibn
Sa’ad-Allah amuwiye radhi-amesema: “Hatukuwa
tukipata lepe la mchana (hatulali usingizi mdogo
wa mchana) wala chakula cha mchana ila baada ya
(kuswaliwa) swala ya Ijumaa”. Bukhaariy
& Muslim-Allah awarehemu.
Hadithi zote hizi zinafahamisha kwamba Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-alikuwa haiswali swala ya Ijumaa ila
ndani ya wakati wa Adhuhuri. Na si tu ndani ya
wakati wa Adhuhuri bali ndani ya wakati wa
mwanzo wa Adhuhuri, elewa na ufahamu hivi. Kwa
mantiki hii basi, hakusihi kuiswali swala ya
Ijumaa kabla ya wakati huu wa Adhuhuri wala
baada yake, yaani baada ya kumalizika na kuingia
Alasiri.
IV.
Ijumaa iwe moja tu katika mji ila kwa
dharura:
Kumeshurutizwa kutoidadika (kutokuwa nyingi) swala za Ijumaa katika mji au
kitongoji kimoja muda wa kumkinika hilo. Hii ni
kutokana na ule wajibu wa kukutana watu wa mji
mmoja mahala pamoja ili kuonyesha nembo ya swala
tukufu ya Ijumaa.
Angalia:
a)
Iwapo watu watakithiri (watakuwa wengi)
kiasi cha kushindikana kukusanyika mahala pamoja
kutokana na ufinyu wa mahala hapo. Katika hali
na mazingira haya kutajuzu kuwepo na Ijumaa
nyingi kwa kiasi cha kukidhi haja tu.
b)
Lau swala za Ijumaa zitakuwa nyingi
katika mji mmoja bila ya kuwepo na haja ya
kisheria ya kufanya hivyo. Haitasihi miongoni
mwa Ijumaa hizo ila ile iliyozitangulia
nyingine. Na mazingatio na marejeo katika
kutangulia ni katika kuanza na sio katika
kumalizika. Kwa mantiki hii basi, ile swala
ya Ijumaa ambayo imamu wake ataanza kuswali
kabla ya zile nyingine, hiyo ndiyo itakayokuwa
sahihi. Na nyingine zote zilizobakia zitakuwa ni
batili na kutawapasa watu waliozihudhuhuria
kuswali Adhuhuri mahala pa Ijumaa.
c)
Ikiwa haijulikaniwi ni Ijumaa ipi
iliyotangulia, basi Ijumaa zote hizo zitakuwa ni
batili. Na kutawalazimu watu wa Ijumaa hizi
kukusanyika mahala pamoja iwapo hilo linamkinika
na wakati ukawa unaruhusu, waswali tena Ijumaa
upya. Iwapo hili halitawezekana, wote
watalazimika kuswali Adhuhuri kwa ajili ya
kuunga mapungufu yaliyojitokeza.
Dalili
ya sharti hili:
Sharti
hili la nne la kusihi kwa swala ya Ijumaa
linatokana na ukweli kwamba si tu katika zama za
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Bali
hata katika zama za makhalifa waongofu-Allah
awawiye radhi-na pia katika zama za Taabiina.
Ijumaa haikuswaliwa ila mahala pamoja tu katika
mji/kitongoji kizima. Zama/enzi hizo ulikuwepo
katika mji/kitongoji msikiti mkubwa kushinda
misikiti yote iliyopo katika mji/kitongoji
husika. Msikiti huu ulijulikana kama
“AL-MASJIDUL-JAAMII”-yaani “MSIKITI WA
IJUMAA”, inamoswaliwa ndani yake Ijumaa ya
mji/kitongoji hicho. Na misikiti mingine ilibaki
ikitumiwa kwa swala tano nyingine, yaani zile za
kila siku na sio Ijumaa. Hivi ndivyo tunavyoweza
kufahamu kupitia hadithi zifuatazo:-
I.
Imepokelewa kutoka kwa mama wa waumini;
Bi. Aysha-Allah amuwiye radhi-amesema: “Watu
walikuwa wakija mara kwa mara siku ya Ijumaa
kutoka majumbani mwao na kutoka (pande) za
‘AWAALIY” (Hizi ni sehemu/vitongoji vya mashariki mwa Madinah.
Kilichokuwa karibu zaidi na Madinah kilikuwa
umbali wa maili tatu au nne kutokea
mjini Madinah palipokuwa pakiswaliwa hiyo
Ijumaa)”.
Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.
II.
Imepokelewa kutoka kwa Ibn Abbas-Allah
awawiye radhi-kwamba amesema: Hakika Ijumaa
ya mwanzo iliyoswaliwa baada ya ile Ijumaa
(iliyoswaliwa) katika msikiti wa Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-(ilikuwa) katika
msikiti wa Abdili-Qaysi huko Juwaathaa (hiki kilikuwa ni kimojawapo ya vitongoji vya nchi ya Bahrein enzi hizo)
pande za Bahrein”. Bukhaariy &
Muslim-Allah awarehemu.
Falsafa ya sharti hili ni kwamba kitendo cha kutosheka na mahala pamoja watu
wote kinapelekea zaidi kufikiwa kwa lengo la
swala hii ya Ijumaa inayowakusanya watu wengi
kwa pamoja mara moja kila juma. Na lengo hili si
lingine bali ni kule kuwa wamoja waislamu na
kuonyesha mshikamano utakaowaogofya na kuwatisha
maadui wao. Na kitendo cha kutapanyika huku na
huko bila ya haja, hutengeneza na kujenga
mazingira ya kugawika na kutengana na hivyo
kutoa mwanya kwa adui kuingia kati yetu kirahisi
na kutugonganisha wenyewe kwa wenyewe.
|