Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SIRA-UTANGULIZI

 

SIRA NI NINI?

       Sira ni fani inayojishughulisha kuelezea maisha ya Nabii Muhammad tangu kuzaliwa mpaka kufa kwake, ikiwa ni pamoja na malezi na makuzi yake, wasifu wake wa kimaumbile, tabia zake, harakati zake katika kuufikisha ujumbe wa Uislamu kwa ummah, mahusiano yake na watu na mataifa mbalimbali. Pia sira inaelezea hali ya ulimwengu kijamii na kiitikadi kabla na baada ya kuja Nabii Muhammad, kadhalika inataja maisha na utawala wa Makhalifa waongofu baada ya Mtume.

MADHUMUNI NA FAIDA ZA SIRA

Fani ya Sira inalenga kumfahamisha Muislamu:-

  1. Taswira na mfumo mzima wa Uislamu unatolewa na kutafsiriwa na maisha ya Mtume.
  2. Maisha ya Nabii Muhammad ndio kigezo na mfano mwema wa kuigwa na kufuatwa ili kuweza kupata mafanikio Duniani na Akhera. Mwenyezi Mungu atuambia:-"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"(33:21)
  3. Muislamu apate katika maisha ya Nabii Muhammad kitu kitakachomsaidia kuifahamu Qur-ani kwani aya nyingi za Qur-ani zinafasiriwa na kuwekwa wazi na matukio yaliyotokea katika uhai wa Mtume.
  4. Sira inaonyesha ni njia na mbinu zipi alizozitumia Mtume mpaka akaweza kuusimamisha Uislamu katika ulimwengu uliokuwa umefunikwa na kiza totoro cha ushirikina.
  5. Sira inaonyesha ni jinsi gani Mtume alivyoyatatua matatizo na vikwazo mbalimbali vya ndani na nje alivyokumbana navyo katika kumfikisha ujumbe wa Allah kwa watu wote.

Hizi ni baadhi tu ya faida zinazopatikana katika kuisoma na kuifuata sira ya Bwana Mtume.

SURA YA KWANZA

SOMO LA KWANZA

i  )BARA ARABU WAKATI WA MTUME NA WAKAZI WAKE

Bara Arabu lipo upande wa kusini wa Bara la Asia. Bara hili ndilo makazi ya Waarabu tangu kale na mpaka sasa kinaishi humo kizazi cha Waarabu. Maelfu ya miaka Waarabu wa kale wliishi maisha yaliyofanana na maisha yetu ya leo ukiondoa tofauti chache zilizokuwepo. Walikuwepo miongoni mwao wakazi wa mijini waliostaarabika na kuendelea.

Ama zile tofauti chache zilizokuwepo kati ya maisha ya Waarabu wale wa kale na maisha yetu ya leo ni kwa upande wa kidini (kiitikadi) na kijamii. Waarabu wa kale waliishi katika enzi/zama za viza zilizotawaliwa na itikadi potofu za kidini na desturi mbaya. Baada ya kudhihiri Uislamu hali mbaya hizi zilibadilika na Waarabu wakaanza kuishi katika zama za uchanuzi wa dini ya Kiislamu katika mji wa Makkah kisha ikaenea katika pande zote za Bara Arabu Uislamu ulizibadilisha hali na kupigiwa mfano.

ii) NCHI YA HIJAZI NA KUANZISHWA MJI WA MAKKAH

Mji wa Makkah ndio kitovu na chimbuko la kuenea dini ya Kiislamu. Mji huu upo katika nchi ya Hijazi, nchi ambayo imechukua eneo kubwa la Bara Arabu. Nchi hii ya Hijazi ilikaliwa na makabila mengi ya Kiarabu, kabila mashuhuri zaidi lilikuwa ni Qurayshi.

Historia ya mji wa Makkah na kuanzishwa kwake inaanzia pale alipofika katika mji huo kwa mara ya kwanza Nabii Ibrahimu – Amani na Rehma za Allah zimshukie -   akitokea nchi ya Palestina akiwa pamoja na mkewe Haajira na mwanawe Ismail. Wakati huo mji wa Makkah ulikuwa ni jangwa tupu lililozungukwa na majabali. Nabii Ibrahimu akamuacha mkewe na mwanawe katika jangwa hilo tupu lisilo na mimea na kurejea Palestina. Kabla ya kufunga safari ya kurudi Palestina Nabii Ibrahimu alimuomba Mola wake Mtukufu rehema zake ziyatawale maisha mapya ya mkewe na mwanawe jangwani hapo na Mola Muumba aliipokea na kuikubali dua ya Mtume wake kama tunavyosoma ndani ya Qur-ani. Mwenyezi Mungu akamchimbulia mama Haajira na mwanawe Ismail chemchem ya Zamzam katika ardhi kame ya jangwani.

Wasafiri wapitao njia ile walipokiona kisima cha Zamzam walikwenda mahala pale na kuamua kuishi kandokando ya chemchem ile, hii ni kutokana na shida sugu ya maji jangwani. Tangu wakati huo kitongoji hicho kikaanza kustawi mpaka kikawa ndio kitongoji mama cha nchi ya Hijazi. Mtoto Ismail alipofikia umri wa kuoa alioa katika makabila yale ya Waarabu waliokuja kukaa pale na kuuanzisha mji wa Makkah. Akajaaliwa kupata watoto.

Ibrahimu baba yake Ismail akawa anafanya ziara za mara kwa mara kujulia hali mkewe, mwanae na wajukuu zake. Katika mojawapo ya ziara zake hizi ndipo Mwenyezi Mungu alipompelekea wahyi wa kuijenga A-kaaba. Ibrahimu na mwanawe wakaitekeleza amri ya Mola wao wakaijenga Al-kaaba. Mwenyezi Mungu akamuamrisha Nabii Ibrahimu awaite watu kuja kuhiji na kufanya ibada katika nyumba yake hiyo tukufu. Ujenzi huu wa nyumba tukufu ya Mwenyezi Mungu na ibada tukufu ya Hijjah ndivyo vilivyoufanya mji wa Makkah kuwa ni mji mtakatifu. Hii ndio historia fupi ya kuasisiwa mji wa Makkah.

iii) KABILA LA QURAYSHI NA UTAWALA WAKE

Makabila mengi yalipatikana kutokana na kizazi cha Ismail mwana wa Nabii Ibrahimu katika nchi ya Hijazi, kabila la Qurayshi ndilo lililokuwa mashuhuri zaidi. Baadhi ya makabila haya yalikuwa yakimuabudu Mwenyezi Mungu kupitia mafundisho ya dini ya Nabii Ibrahim- Amani ya Allah imshukie. Uongozi wa kidini na kibiashara ulitawaliwa na Maqurayshi kwa sababu ya ushujaa na ufasaha waliokuwa nao, sifa hizi ndizo zilizolipelekea kabila la Qurayshi kuyatawala makabila mengine yote. Mji wa Makkah na Maqurayshi walizidi kupata utukufu pale Mzee Qusway Bin Kilaab-babu wa nne wa Mtume aliposhika hatamu za uongozi wa mji wa Makkah. Mzee huyu alikuwa ni mtu mwenye busara, fikra na hekima. Alianzisha mpango mji, bunge ili watu wote wa Makkah waweze kukutana humo na kushauriana/kujadili mambo yao, pia aliijenga upya Al-Kaaba baada ya kuanza kuonyesha athari za kubomoka. Kadhalika alianzisha utaratibu wa kuwasaidia masikini kwa kuwapa chakula na maji. Baada ya kupita vizazi vingi, taratibu Maqurayshi walianza kuyatupa mafundisho ya dini ya Nabii Ibrahimu na kuanza kuyaabudu masanamu yaliyotengenezwa na mikono yao wenyewe. Ibada ya msanamu ilikuwa ni matokeo ya safari ya mmoja wa viongozi wa Maqurayshi alipokewenda Shamu na kuwakuta watu wa huko wakiyaabudia masanamu na akapendezwa na kuvutiwa na ibada hiyo. Akarejea Makkah na sanamu moja, akaliweka ndani ya Al-kaaba na kuanza kuliabudia. Watu wa Makkah kuona hivyo nao wakamuiga kiongozi wao, wakatengeneza masanamu yao wakayaweka ndani ya Al-kaaba na kuyaabudia na huo ukawa ndio mwanzo wa kuiacha na kuitupa mila ya Nabii Ibrahimu.



Forum | Guestbook | Tuandikie |