Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SOMO LA TANO-KUANGUKA KWA KHAYBAR

 Faida

        i.          Kuanguka kwa Khaybar:

            Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipokwishazifungua na kuzitia mikononi mwake ngome za Mayahudi alizoziteka na kuhodhi mali zao kiasi alichohodhi. Mayahudi wakawa hawana mahala pengine ila ngome mbili tu; Al-Watwiyh na Salaalim nazo ndizo zilizokuwa ngome za mwisho za Khaybar. Mtume akawazingira kwa muda wa siku kumi na kitu hivi, hata walipoyakinisha kuwa wataangamia wakamuomba Mtume awakubalie kujisalimisha kwa sharti ya kutokumwagwa damu yao. Akateremka kutoka ngomeni Kinaanah Ibn Rabee Ibn Abil-Huqayq, akasuluhiana na Mtume wa Allah juu ya kutokumwagwa damu ya wapiganaji waliomo ngomeni na wakubaliwe kuondoka Khaybar pamoja na familia zao. Nao wamuachie Mtume wa Allah ardhi, mali, farasi na silaha zote walizokuwa wakimiliki. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Na iwe mbali nanyi dhima ya Allah na ile ya Mtume wa Allah iwapo mtanificha jambo/kitu cho chote”. Akaandikiana nao mkataba kwa masharti hayo, kwa kuzisalimisha kwao ngome za Al-Watwiyh na Salaalim, Khaybar nzima ikawa imeangukia mikononi mwa waislamu. Na waislamu wakapata humo ngawira tele.

 

      ii.          Suluhu baina ya Mayahudi na waislamu:

           Ilipotimia suluhu baina ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-na watu wa Khaybar. Mayahudi hawakupenda kuhama na kuuacha mji wao huu wa Khaybar kama walivyoahidi. Kwa hivyo wakamuomba Mtume awaache waitumie ardhi hiyo kwa kilimo na wampe nusu ya mazao yatakayopatikana, wakamwambia: “Sisi tunaijua zaidi ardhi hii kuliko nyinyi na tunaweza kuiendeleza”. Mtume akawakubalia ombi lao hilo na kuwapa rukhsa ya kubakia Khaybar waendeleze kilimo. Na akafunga nao suluhu kwa sharti ya kupata nusu ya mazao yatakayovunwa na kwamba atakuwa na haki ya kuwatoa atakapotaka kufanya hivyo.

 

    iii.          Mayahudi wa “Fadaka” na wale wa “Waadil-Quraa” wataka amani:

             Mayahudi wa “Fadaka” walipoisikia suluhu iliyofikiwa baina ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-na watu wa Khaybar. Wakatia azma ya kuacha vita na wakaelekea katika meza ya amani na wakamtumia ujumbe Mtume wakimtaka afanye nao suluhu kama alivyofanya na watu wa Khaybar. Mtume akawaitika katika matakwa yao hayo na suluhu ikapita baina yao bila ya kutokea mapigano. Khaybar ikawa ni ngawira baina ya waislamu kwa sababu iliangukia mikononi mwao kwa matumizi ya nguvu. Ama Fadaka hii ikawa ni ya Mtume pekee, kwa sababu haikupatikana kwa njia ya vita. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipomaliza kulishughulikia suala la watu wa Khaybar, huyoo akashika njia kuelekea “Waadil-Quraa”. Akawazingira watu wake kwa siku kadhaa mpaka wakasalimu amri na kutangaza suluhu, Mtume akafunga nao suluhu kama alivyofanya kwa watu wa Khaybar. Ama Mayahudi wa “Taymaa”, hawa walikubali kutoa kodi bila ya kupatikana vita wala mapambano. Kwa hivyo basi, Mayahudi wote wakawa wamesalimu amri kwa Mtume na mamlaka waliyokuwa nayo katika miji ya Waarabu yakafikia tamati. Waislamu sasa wakawa na amani kwa upande wa Kaskazini mpaka Shamu kama walivyokuwa na Amani upande wa Kusini baada ya suluhu ya Hudaybiyah.

 

    iv.          Ugavi wa ngawira:

                  Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaipiga mafungu matano ngawira ya Khaybar na kuanza kuigawa. Askari mwenda kwa miguu akampa fungu moja na mpandaji akampa mafungu matatu. Na akampa kutoka katika khumsi (1/5) yake yeye Mtume yule aliyemdhihirishia Allah kumpa; akawapa wakeze, akawapa wanaume na wanawake wa ukoo wa Abdul-Mutwalib na akawapa pia mayatima na waombaji. Ama watumwa na wanawake waliohudhuria Khaybar, hawa aliwamegea kitu kidogo na wala hakuwatengea fungu maalum.

Wakati waislamu wakiwa katika furaha ya ushindi wa Khaybar, walijiwa na Ja’afar Ibn Abiy Twalib akiliongoza kundi la waislamu waliokuwa uhamishoni huko Uhabeshi (Eritrea ya leo). Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akafurahishwa mno na ujio wao, akamkumbatia Ja’afar, akambusu baina ya macho yake na kusema: “Sijui nimefurahishwa na lipi zaidi kati ya mawili haya; ushindi wa Khaybar au ujio wa Ja’afar?”.

 



 | Tuandikie |