Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SOMO LA SITA

 Faida

        i.          Vita hivi ndivyo vilivyowapa amani waislamu dhidi ya shari ya mayahudi:

            Naam, hivyo ndivyo ilivyokuwa katika suala zima la kumtiisha na kumshikisha adabu adui huyu mkubwa. Adui ambaye alifanya silaha yake kuwa vitimbi, khiana, uongo na udanganyifu (ghushi) na kuleta uchochezi baina ya waislamu. Kuyatilia shaka aliyoyateremsha Allah kwa Mtume wake na kugonganisha baina ya waislamu na Uislamu wao pia ni miongoni mwa silaha hatari zilizotumiwa na adui huyu. Na lengo lake kuu likiwa ni kuufuta Uislamu na waislamu juu ya uso wa sayari dunia kwa njia yo yote iliyokuwa ndani ya uweza wake. Basi pale Allah alipoikata nguvu yake, akaondosha mamlaka yake na kuidhalilisha jeuri yao, hapo ndipo waislamu walipoaminika dhidi ya shari ya adui huyu. Kama walivyoaminika dhidi ya shari ya Makureishi kwa kutimia mkataba wa suluhu ya Hudaybiyah. Na yote haya ndio Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliyokuwa akiyatafuta kutokana na mapigano haya dhidi ya Mayahudi.

Kufuatia kushindwa vibaya huku kwa Mayahudi, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaridhia Mayahudi kuendelea kuishi katika ardhi ya Khaybar na kugawana nao nusu kwa nusu ya mavuno yatokanayo na shughuli za kilimo. Mtume aliyafikia maridhiano haya baada ya Mayahudi hawa kukubali kutolewa Khaybar na kuiacha mali yote na silaha ikiangukia ngawira mikononi mwa waislamu. Kwa makubaliano haya, kukawa hakuna tena haja ya kuwafukuza na kuwatoa Khaybar baada ya kusalimisha silaha zao na kuvunjwa vunjwa nguvu yao. Kulikomaanisha kuwapatia amani waislamu dhidi ya adui yao huyu.

Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaendeleza juhudi zake za kutaka kuwepo na uhusiano mwema baina ya waislamu na mayahudi. Uhusiano utakaojengwa juu ya misingi ya upendo, ukweli na ujirani mwema na wala sio juu ya misingi ya uadui na chuki kama ilivyokuwa wakati huo. Ili kulifikia lengo hili, akaamua kutumia mbinu ya kuunga nao udugu kwa kuoa kwao. Akamteua katika wanawake wao Safiyah Bint Huyay na akampa khiari ya kuchagua moja ya mambo mawili; ama amuache huru na kumuoa au amuache huru na kumrudisha kwao. Bibi huyu akakhiari kuwa mke, Mtume akamuacha huru akamuoa na kuwa miongoni mwa mama wa waumini. Kwa kukubali kwa khiari yake kuolewa na Mtume, bibi huyu mwema akaisafisha nafsi yake na kuondosha uadui uliokuwamo humo dhidi ya Mtume, Uislamu na waislamu. Mpaka imepokewa kwamba yeye alipata kusema: “Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa ni wa mbele katika watu niliokuwa nikiwachukia kupindukia. (Kwa sababu) alimuua baba yangu na mume wangu. Kwa ajili hiyo (Mtume) aliendelea kunitaka udhuru akisema: Hakika baba yako alinikusanyia majeshi shirika ya Waarabu na akafanya akafanya...”, mpaka hilo likatoka ndani ya nafsi yangu.

 

      ii.          Mtume aishi na Mayahudi kwa siasa ya urafiki na uadilifu:

           Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa ni mpole kwa mahasimu wake hawa, akipupia mno kutangamana nao kwa uadilifu. Akijitahidi kwa nguvu zake zote kuondosha mioyoni mwao athari ya uadui huu, kwani uadui baina yao haukuwa uadui binafsi. Hakika si vinginevyo, uadui huo ulitokana na tofauti za itikadi/imani waliyo ibadilisha: “...KWA SABABU YA HUSUDA ILIYOMO NYOYONI MWAO; (iliyowapata) BAADA YA KUWAPAMBANUKIA HAKI...” [2:109] Imepokewa kwamba Sayyidina Bilali-Allah amuwiye radhi-alipita na Safiyah na binti ya ami yake kwa wauliwa (maiti wa vita) wa Mayahudi. Yule binti ya ami yake na Bi. Safiyah akapiga ukelele mkubwa, Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akaelezea kutopendezwa kwake na kitendo alichokifanya Bilali. Akamuuliza: “Umetokwa na huruma wewe? Unampitisha binti kigori kushuhudia waliouliwa!!” Bilali akajitetea: “Ewe Mtume wa Allah, mimi sikudhania kwamba wewe unalichukia jambo hilo na mimi nilipenda aone maanguko ya kaumu yake”. Kisha akaapa kutorudia kutenda tena kosa kama hilo. Kadhalika imepokewa kwamba Mayahudi walikwenda kumlalamikia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwamba waislamu wanaingia mashambani mwao na kuchukua mazao yao baada ya kupita kwa suluhu. Mtume alipowasilishiwa rasmi malalamiko haya ya Mayahudi, akatoa amri waislamu wakusanyike. Walipoitika wito, Mtume akasimama mbele yao, akamuhimidi Allah na kumsifia, kisha akasema: “Hakika Mayahudi wamenishtakia kwamba nyinyi mnaingia  katika bustani zao na ilhali wao wamekwisha kuaminini juu ya mali na damu zao zilizomo mikononi mwao katika ardhi yao. Na sisi tumechukua ahadi kwao kwamba waendelee kuimiliki ardhi ( hii ya Khaybar kwa shughuli za kilimo) walime na sisi tupewe nusu ya mazao yatakayovunwa. Kwa yakini hazihalaliki mali za wafungiwa ahadi ila kwa haki yake”. Baada ya khutba hii ya Mtume, waislamu wakawa hawachukui tena mboga za Mayahudi ila kwa kununua. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akawa anamtuma Abdullah Ibn Rawaahah-Allah amuwiye radhi-kwa watu wa Khaybar. Kuwa mkadiriaji na mthamini wa mavuno baina ya waislamu na mayahudi na kisha kugawa baina ya pande mbili hizi kwa mujibu wa makubaliano ya suluhu. Wakati akiitekeleza dhima hii aliyokabidhiwa na Mtume wa Allah, Mayahudi walipata kusema: “Umetufanyia uadui (umetudhulumu)”, yeye akiwaambia: “Mkitaka gaweni nyini na mkitaka basi tutagawa sisi”. Hapo Mayahudi husema: “Mbingu na ardhi zimesimama kwa uadilifu huu”.

Imamu Bukhaariy-Allah amrehemu-amepokea kwa sanadi ya Said Al-Khudriy na Abu Hurayrah-Allah awawiye radhi. Kwamba Mtume wa Allah alimpa ugavana wa mji wa Khaybar mtu mmoja. Gavana huyu akamletea Mtume tende bora kabisa, Mtume akamuuliza: “Tende zote za Khaybar ndio ziko hivi?”, akajibu: “Hapana ewe Mtume wa Allah, hakika sisi tunabadilisha pishi moja ya tende hizi kwa pishi mbili za aina nyingine ya tende na pishi mbili kwa tatu”. Mtume akasema: “Msifanye hivyo, ziuzeni zote kwa dirham kisha nunueni kwa dirham mlizopata tende zenye kiwango hiki cha ubora”.

Na katika jumla ya ngawira walizozipata waislamu Khaybar ni mbao za Taurati (vitabu), Mayahudi wakaja kuzidai, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaamuru warudishiwe. Kulielekea hili Muisraeli Dr. Wilnson anasema: “Tendo hili linaonyesha hadhi/daraja ya vitabu hivi iliyokuwemo ndani ya nafsi ya Muhammad. Hili liliwafanya Mayahudi kumuona Muhammad kuwa ni mjenzi (si mbomozi) na kumuheshimu kwa sababu hakuvitenda vibaya vitabu vyao vitakatifu. Sambamba na hili wanayakumbuka yaliyotendwa na Warumi pale walipouteka mji wa Jerusalem na kuutia mikononi mwao mnamo mwaka 70 K.K. walivichoma moto vitabu vitakatifu na kuvikanyaga kwa miguu yao. Hii ndio tofauti ya wazi baina ya wateka mji (washindi) tuliowataja na Mtume wa Uislamu”. Mwisho wa kunukuu.

 



 | Tuandikie |