|
Je, Mayahudi
waliuthamini wema wote huu waliotendewa na Mtume? Na je, waliuhifadhi wema huu
na kujua kwamba Mtume wa Uislamu hakuwadhamiria shari? Na kwamba misingi ya
Uislamu imesimama juu ya haki, uadilifu na kuwaheshimu watu kama wanaadamu. Na
kwamba Uislamu unawafanyia uadilifu maadui zake kama unavyowafanyia wapenzi na
marafiki zake bila ya tofauti yo yote. Na je, Mayahudi walitambua kwamba
Muhammad ni mkweli kuliko watu wote kwa kauli na mwingi wao kwa uadilifu? Na
kwamba ni mtwaharifu wa moyo kuliko watu wote na ni mwenye matangamano mema?
Mayahudi hawakuthamini cho chote katika utu, uanadamu na wema
huu mkubwa waliotendewa. Bali waliendelea kubakia na umbile lao la asili;
dhamira chafu na kukanusha wema. Na nyoyo zao zikaendelea kutokota mifundo
dhidi ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Wakairejea ada yao ya tangu
zama wakaanza kufikiria kumfanyia khiana Mtume na kula njama za kumuua.
Wakamkabidhi jukumu hilo la kummaliza Mtume mwanamke mmoja, huyu akapanga hila
kabambe katika kuitekeleza dhima hii chafu aliyopewa. Mwanasira; Ibn
Ishaq-Allah amrehemu-anasimulia: “Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-alipomakinika na kutulizana, Zaynab Bint Al-Haarith; mke wa Salaam
Ibn Miksham alimletea zawadi ya mbuzi mzima wa kuchoma. Khabithi huyu alikuwa
tayari amekwishauliza ni nyama ipi aipendayo mno Mtume wa Allah, akaambiwa
anapenda sana mkono wa mbuzi. Basi akatia sumu nyingi sehemu hiyo na akamtia
sumu mbuzi wote, kisha akamletea Mtume zawadi hii ya kifo. Alipomuweka mbele
ya Mtume, akachukua mkono na kung’ata pande lakini hakutafuna. Na wakati huo
Mtume alikuwa na swahaba wake; Bishru Ibn Al-Baraai Ibn Ma’aruur-Allah amuwiye
radhi. Huyu nae akakata kipande pale pale alipokata Mtume wa Allah,
akakitafuna na kukimeza. Ama Mtume yeye alikitema kipande alichokikata, kisha
akasema: “Hakika mfupa huu unaniambia kwamba umetiwa sumu”, akamuita mwanamke
yule kumuuliza nae akakiri. Mtume akamuuliza: Ni lipi lililokupelekea kufanya
haya uliyoyafanya”, akajibu: “Umefikia kwa watu wangu daraja ya kutochelewa,
basi nikajiambia akiwa ni mfalme (atakufa) nasi tutapumzika nae. Na akiwa ni
Mtume kweli, basi ataambiwa”. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-baada
ya kumsikiliza, akamsamehe na swahaba wake; Bishru akafa kutokana na sumu ya
kile kipande alichokula”.
iv.
Makurayshi wazifuatilia
kwa makini khabari za Khaybar:
Ushindi wa
Khaybar ulikuwa ni tukio adhimu lililowatikisa Makurayshi na kuwafanya
walifuatilie kwa karibu mno. Wakaanza kuangalia natija na kuitathmini tangu
pale walipotambua kwamba Mtume ameelekea Khaybar. Katika kulielekea tukio
hili, waligawika makundi mawili; kundi lililoangalia nguvu ya Mayahudi, uimara
wa ngome zao na wingi wa idadi yao na zana zao za vita. Na kuangalia ushirika
waliokuwa nao na Ghatwfaan, kwa maono yao haya wakisema: “Mayahudi na
washirika wao wataibuka washindi”. Na kundi jingine likiangalia hali-kisogo
(iliyopita) ya waislamu huko nyuma na nguvu na uthabiti wa nyoyo walio nao.
Nidhamu na mipangp yao makini, ushirikiano wao mzuri na kuyaona kwao mauti si
kitu katika kuipigania itikadi/imani yao, kwa maono yao haya wakisema:
“Muhammad na maswahaba wake wataibuka washindi”. Kila kundi likishikamana na
maono yake mpaka wakafikia kuwekeana madau makubwa, wakawa wakifuatilia
khabari za mambo yanavyojiri huko Khaybar kwa karibu mno. Na wakiyangojea
matokeo kwa shauku kubwa kiasi cha kufikia kungojea kwenye njia kuu
wakimuuliza kila ajaye hali ilivyo baina ya Muhammad na Mayahudi.
Wanasema wana sira-Allah awarehemu: “Al-Hajaj Ibn Alaatw
As-sulamiy-Allah amuwiye radhi-alikuwa amekwishasilimu na kuhudhuria Khaybar
pamoja na Mtume wa Allah. Khaybar ilipoangukia mikononi mwa waislamu alisema:
“Ewe Mtume wa Allah, hakika mimi ninayo mali Makah kwa mke wangu; Ummu Sheibah
Bint Abiy Twalhah. Na mali yangu imetawanywa kwa wafanyabiashara wa Makah,
basi nakuomba unipe idhini ewe Mtume wa Allah nikaikusanye”. Mtume akampa
idhini, Al-Hajaaj akasema: “Sina budi kuzua uongo ewe Mtume wa Allah (ili
niweze kutimiza azma yangu hii)”, Mtume akamwambia: “Sema”. Al-Hajjaaj
anaendelea kusimulia: “Basi nikatoka hata nilipofika Makah nikawakuta watu
katika Makureishi katika pande za jangwa la Thaniyah wakinusa khabari na
kuulizia suala la Mtume. Na wakati huo ilikwishawafikia khabari kwamba Mtume
ameenda Khaybar, waliponiona wakasema: “Wallah, Al-Hajaaj anazo khabari
tuzitakazo”. – Anaendelea kusimulia – na walikuwa hawajui cho chote juu ya
kusilimu kwangu, wakaniambia: “Hebu tupe khabari ewe babie Muhammad, kwani
imetufikilia khabari kwamba mkata watu (wakimlenga Mtume) amekwenda Khaybar.
Na hali ya kuwa huo ni mji wa Mayahudi na ni sehemu ya mashambani ya Hijaazi”.
Nikawajibu: “Nami imekwishanifikia khabari hiyo na ninazo khabari
zitakazokufurahisheni”. Walivyosikia hivyo haraka haraka wakamzunguka ngamia
wangu na kusema: “Haya lete khabari ewe Hajjaaj”. Nikawaambia: “Muhammad
ameshindwa vibaya mno haijapata kutokea na maswahaba wake wameuawa hamjapata
kusikia katu na Muhammad mwenyewe amechukuliwa mateka. Wakasema Mayahudi sisi
hatumuui tunampeleka huko Makah akauliwe na ndugu zake kulipa kisasi cha watu
wao aliowaua”. Kusikia hivyo wakainuka na kupiga ukelele mkubwa wakisema: “Kwa
yakini imekujilieni khabari, hakika si vinginevyo mnachongojea ni kuletewa
Muhammad akauawa mbele yenu nyote mkishuhudia”. Nikawaambia: “Nipeni msaada wa
kukusanya mali yangu kutoka kwa wadeni wangu wa Makah, kwani mimi ninataka
kurudi Khaybar nilikute kundi la Muhammad, kabla sijatanguliwa huko na
wafanyabiashara wengine”. Wakainuka na kunikusanyia mali yangu kwa haraka mno
hujapata kusikia haraka kama hiyo. Nikamuendea mke wangu na kumuuliza: “I wapi
mali yangu?, - kwani mimi nilikuwa na mali niliyoiwekesha kwake – ili
nizipatilize fursa za biashara kabla sijatanguliwa na wafanyabiashara
wengine”.
Anaendelea kusimulia Hajjaaj, Al-Abbas Ibn Abdul-Mutwalib
alipoisikia khabari ile na kwamba imetoka kwangu. Akaja mpaka akasimama
pembeni yangu nami nikiwa ndani ya mojawapo ya mahema ya wafanyabiashara,
akasema: “Ewe Hajjaaj ni khabari gani hii uliyokuja nayo? Nikamuuliza: “Je,
unaweza kuficha siri kwa nitakayokwambia?”, akajibu: “Naam”. Nikamwambia:
“Basi ningojee mpaka nimalize”, nilipomaliza kukusanya kila kitu kilichokuwa
changu pale Makah na nikaazimia kuondoka, nilikutana na Al-Abbas na
nikamwambia: “Nifichie siri ewe Abul-Fadhli, kwani mimi ninachelea kutafutwa
kwa siku tatu, baada ya hapo sema utakavyo”, akajibu: Nitafanya hivyo
utakavyo”, ndipo nilipomwambia: “Basi wallah, hakika mimi nimemuacha mwana wa
nduguyo akiwa ni bwana harusi kwa binti ya mfalme wao yaani Safiyah Bint Huyay
Ibn Akhtwab. Na kwa yakini ameishinda na kuitia mikononi mwake Khaybar nzima
na kuhodhi mali yote”. Akauliza: “Unasemaje ewe Hajjaaj?, nikamjibu: “Wallah
ni kweli, lakini nifichie siri na kwa yakini mimi nimekwishasilimu na sikuja
ila kwa ajili tu ya kukusanya mali yangu. Kwa sababu nachelea nisije
kudhulumiwa, basi zikishapita siku tatu unaweza kulifichua hili ukipenda”.
Anaendela kuhadithia: “Nikaenda zangu hata ilipofika siku ya
tatu tangu kuondoka kwangu, Al-Abbas akavaa mavazi yake rasmi, akajitia
manukato na kuitia bakora mkononi. Kisha huyoo akatoka, akaenda zake mpaka
kwenye Al-Ka’abah akatufu, Makureishi walipomuona wakamwambia: “Ewe babie
Fadhli, huku wallah ni kustahamilia joto la msiba”, akasema: “Sivyo hivyo,
ninaapa kwa Allah mnayeapa kwa jina lake, kwa yakini Muhammad ameifungua
Khaybar. Na tena ameachwa akiwa bwana harusi kwa kumuoa binti ya mfalme wao na
amehodhi mali zao na zimeangukia kuwa ni zake na maswahaba wake”. Wakamuuliza:
“Ni nani aliyekuletea khabari hizi?”, akawaambia: “Ni yule yule aliyekuleteeni
khabari alizo kuleteeni na ameingia kwenu akiwa tayari ni muislamu, akatwaa
mali yake na kuondoka zake ili kujiunga pamoja na Muhammad na maswahaba wake”.
Wakasema: “Ameponyoka adui wa Mungu, ama wallah lau tungelijua basi
pangelikuwa na kazi baina yake nasi”. Na haukupita muda mrefu ikawajia khabari
iyathibitishayo waliyoambiwa na Al-Abbas.
|