|
i.
Ushindi wa waislamu dhidi
ya Mayahudi wa Khaybar wawabutwaisha na kuwastaajabisha mahasimu zao:
Hivi ndivyo
tukio la Khaybar lilivyotusha mshindo mkuu mioyoni mwa Makureishi na wala
hapana shaka kwamba lilikuwa ni tukio hemezi na stushi. Kwani Makureishi
hawakutarajia kabisa kwamba Khaybar itasamabaratika na kuangukia mikononi mwa
waislamu kwa kasi kiasi hicho. Na hali Khaybar ndio Khaybar kwa ngome
madhubuti na watu mashujaa iliyokuwa nao. Na haikuwapitikia akilini kwamba
Muhammad na maswahaba wake wanaweza kuishinda nguvu hiyo kwa haraka kiasi
hicho. Ukweli ulivyo khasa, ushindi huu wa waislamu dhidi ya Mayahudi wa
Khaybar unalazimisha kuleta fikra na mazingatio. Kwa sababu Mayahudi hawa
walikuwa na nguvu kubwa mno kwa sura ambayo hawakuwa ni watu wa kushindwa.
Kwanza idadi yao ilikuwa ni wapiganaji alfu kumi wenye umahiri wa vita na wao
ndio waliokuwa kundi hatari katika medani ya vita kuliko Wana-Israeli wote.
Isitoshe walikuwa na umahiri mkubwa katika urushaji wa mishale, mikuki na
kuvurumisha mawe, tena walikuwa na ushujaa mkubwa katika uwanja wa mapambano.
Halafu tena walikuwa wamezungukwa na ngome madhubuti zisizopenyeka kwa
urahisi, si hivyo tu walikuwa na zana nzito za kivita ukilinganisha na
waislamu. Walikuwa na chakula cha kutosha kujikimu kwa muda mrefu na walikuwa
na kila sababu ya kuwatia mori vitani. Ikiwa ni pamoja na kulinda
heshima/utukufu wao, kuuhami mji wao na kumfagilia mbali adui anayetishia
maslahi yao. Wakati ambapo jeshi la waislamu halikuwa na zaidi ya wapiganaji
alfu moja na mia sita tu. Na halikuwa na zana za vita zaidi ya majambia,
mikuki na mishale, wala hawakuwa na ngome ya kuwakinga dhidi ya mashambulizi
ya adui. Isitoshe walikuwa na uhaba wa chakula na hawakuwa na msaada pindi
wangezidiwa.
Pamoja na tofauti hii
kubwa na ya wazi kabisa katika idadi na zana baina ya makundi mawili haya,
bado waislamu waliwashinda Mayahudi kwa ushindi wa kishindo. Je, hivi kweli
hili si jambo linalolazimisha kuleta mazingatio na tafakari kina?! Hapana
shaka kwamba ushindi huu wa kishindo walioupata waislamu uliwatunduwaza na
kuwabutwaisha Makureishi. Kama ulivyowashtua Waarabu wote na wasio Waarabu
katika pande zote za Peninsula ya Waarabu. Huenda pengine kule kujisalimisha
Mayahudi wa Fadaka na Taymaa bila ya vita na kuporomoka kwa Waadil-Quraa
haraka haraka, kulikuwa ni miongoni mwa athari za ushindi huu wa ajabu.
Ushindi uliozihemeza akili za watu na kuzijaza khofu nyoyo zao kutokana na
nguvu hii ya ajabu. Nguvu isiyoshindwa na wingi wa idadi/zana, isiyozuiliwa na
ngome madhubuti wala haikengeushwi na cho chote katika kufikia malengo yake.
Mayahudi wa Khaybar walijiaminisha kuwa wako salama na kamwe hawakudhania
kwamba siku moja Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-anaweza hata
kuthubutu kuwashambulia seuze kuwashinda. Hii ndio hakika inayoelezwa na
Qur-ani Tukufu: “...NAO WALIDHANIA KUWA NGOME ZAO ZITAWALINDA NA (kufikwa na
amri ya) ALLAH, LAKINI ALLAH ALIWAJIA KWA MAHALA WASIPOPATAZAMIA, NA AKATIA
WOGA KATIKA NYOYO ZAO (wasiweze kupigana na waislamu walipokuja kupigana
nao)...” [59:02]
Naam, ni kweli kabisa
kwamba khofu aliyoitia Allah nyoyoni mwa Mayahudi ni miongoni mwa sababu
muhimu zilizowapa waislamu ushindi huu mnono. Na amesema kweli Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-anapoukiri na kuuthibitisha ukweli huu kupitia
kauli yake: “...nimenusuriwa kwa khofu mwendo wa mwezi mzima...”
ii.
Ushindi wa Khaybar
wahitimisha ukaliaji na utawala wa Mayahudi katika nchi ya Hijaazi:
Miongoni mwa natija za ushindi huu wa kishindo wa Khaybar ni
kuvunjwa kabisa nguvu za kisiasa, kiuchumi na kidini walizokuwa nazo Mayahudi
katika ardhi ya Hijaazi. Vivuli vyao vikaanza kufutika kidogo kidogo mpaka
athari yao yote ikafutika na kutoweka kabisa. Kwa hiyo katika zama za Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-mpaka anaondoka duniani, Mayahudi walibakia
katika kipande kidogo cha ardhi wakiendesha shughuli za kilimo kwa makubaliano
waliyofunga na Mtume wa Allah. Alipokufa Mtume na hatamu za uongozi wa
waislamu kushikwa na Sayyidina Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-aliendelea
kuyaheshimu maamuzi na makubaliano yaliyofikiwa baina ya Mtume na Mayahudi
mpaka anakufa. Sayyidina Umar-Allah amuwiye radhi-akashika hatamu za uongozi
na kuyaendeleza na kuyaheshimu maamuzi ya Mtume na yale ya mtangulizi wake
mwanzoni mwa ukhalifa wake. Kisha Sayyidina Umar akafikiwa na khabari kwamba
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alisema katika maradhi-mauti yake:
“Hazikusanyiki pamoja dini mbili katika kisiwa cha Waarabu”. Sayyidina
Umar akazichunguza khabari hizo mpaka akapata ithibati kuwa ni za kweli, hapo
ndipo alipowatumia Mayahudi ujumbe akisema: “Hakika Allah Taala ametoa idhini
ya nyinyi kutolewa, kwani nimefikiwa na khabari kwamba Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-alisema: “Hazikusanyiki pamoja dini mbili katika kisiwa
cha Waarabu”. Basi ye yote miongoni mwa Mayahudi aliyefunga ahadi na Mtume
wa Allah, basi na aje nimtekelezee. Na ambaye hakufunga ahadi na Mtume wa
Allah, basi na ajitayarishe kuondoka”. Baada ya tangazo hili, ndipo Sayyidina
Umar-Allah amuwiye radhi-alipoanza zoezi rasmi la kuwahamisha Mayahudi wote
ambao hawakuwa wamefunga ahadi na Mtume. Akawatoa katika ardhi za Waarabu
Mayahudi wa Khaybar na Fadaka na akawa bakisha wale wa Taymaa na Waadil-Quraa,
kwa sababu ardhi mbili hizo zimo katika mipaka ya Shamu. Nae Sayyidina Umar
alikuwa anaona kwamba eneo lote lililo nyuma ya Waadil-Quraa mpaka Madinah ni
sehemu ya Hijaazi. “Mayahudi wengi wakabakia Waadil-Quraa mpaka karne ya kumi
na moja Miladia na makundi mengine madogo madogo yalikuwa pande za Taymaa
mpaka karne ya kumi na mbili. Kisha wakaanza kutoweka kidogo kidogo katika
ardhi ya Hijaazi mpaka wakachanganyika na kumezwa na makabila ya Kiarabu”.
{Rejea TAARIKHUL-YAHUUD FIY BILAADIL-ARAB BITASWARUF} na {AL-BIDAAYAH
WAN-NIHAAYAH}.
|