|
Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-alipoazimia kuitekeleza kazi hii, alijitengezea muhuri wa
fedha ulionakishiwa “Muhammadur-rasuulullah”. Na kisha akamuandikia barua
rasmi kila mfalme akimlingania kumuamini Allah asiye na mshirika na
akimkumbusha kwamba salama na mafanikio yako katika kumuamini Allah pekee. Na
akimkalifisha kuufikisha ujumbe huo kwa raia wake, na iwapo atakengeuka na
kupuuzia ujumbe huo basi atabeba dhambi zake mwenyewe na za watu wote walio
nyuma yake. Akimaliza kuandika, ndipo barua hugongwa muhuri wake na kumtuma
mmojawapo wa maswahaba wake kuifikisha kwa mlengwa. Akamtuma Dihyah Ibn
Khaliyfah-Allah amuwiye radhi-kupeleka barua kwa Qayswar; mfalme wa Urumi.
Abdullah Ibn Hudhaafah-Allah amuwiye radhi-akatumwa kwa Kisraa; mfalme wa
Uajemi na Amrou Ibn Umayyah-Allah amuwiye radhi-akatumwa kwa Najaash; mfalme
wa Uhabeshi. Akamtuma Haatib Ibn Abiy Balta’ah-Allah amuwiye radhi-kwa
Muqauqis; kiongozi wa Waqibtw (Egyptian Coptics) na Shujaa Ibn Ibn Wahbi-Allah
amuwiye radhi-akatumwa kwa Al-Haarith Al-Ghasaaniy; mfalme wa majimbo ya
Shamu. Maswahaba sita hawa ndio wajumbe wa mwanzo wa Mtume wa Allah aliowatuma
kwa wafalme waliomzunguka.
Ama mfalme wa Uhabeshi;
Najaash baada ya kuupokea ujumbe wa Mtume alisilimu na akaichukua barua ile ya
Mtume wa Allah na kuiweka machoni pake. Kwa kuitukuza barua ya Mtume akashuka
kutoka katika kiti chake cha enzi na kukaa chini akasema: “Lau ningeliweza
kumuendea (huko aliko), basi bila shaka ningelimuendea”. Kisha akamuandikia
barua Mtume akimfahamisha juu ya kusilimu na kuamini kwake. Kisraa; mfalme wa
Uajemi, huyo alionyesha jeuri na dharau kubwa, kwani aliichukua barua ya Mtume
na kuichanachana. Kisha akamuandikia barua gavana wake aliyeko Yemen, akiitwa
Baadhaan akimuamuru kutuma watu wakamletee huyu anayedai kuwa yeye ni mtume.
Baadhaan akaipokea kwa utii amri ya mkuu wake, akawatuma wawili miongoni mwa
watu wake mashujaa wakamlete mtume ili apelekwe kwa bwana wake. Walipofika
Madinah kwa Mtume, alichukizwa mno na mandhari ya kike na ulainilaini
waliokuwa nao wajumbe hawa wa Baadhaan, akawauliza: “Ni nani aliyekuamrisheni
kuvaa hivyo?”, wakajibu: “Bwana wetu” – wakimkusudia Kisraa. Mtume akawaambia:
“Mpelekeeni salamu huyo mtu wenu aliyekutumeni kwamba bwana wangu amemuua
bwana wake Kisraa katika usiku huu wa leo”. Wapokezi wa Sira-Allah
awarehemu-wanasema: Hakika usiku huo ulikuwa ni usiku wa kuamkia Jumanne,
mwezi kumi Jumaadal-Uula (Mfunguo nne), mwaka wa saba wa Hijrah. Wajumbe
wakarudi kwa Baadhaan na kumkhabarisha waliyoyasikia kutoka kwa Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie. Na haukupita muda mrefu tangu aelezwe khabari
hiyo, ila ilimuwasilia khabari ya kuuawa Kisra kwa mkono wa mwanawe mwenyewe;
Shiyrawaihi. Baadhaan akasilimu pamoja na Wafursi wote waliokuwa nae Yemen.
Ama Muqauqis; kiongozi wa
Waqibtw, yeye aliisoma barua ya Mtume na akasema maneno mazuri. Kisha
akaihifadhi barua hiyo katika chombo kilichotengenezwa kwa meno ya tembo na
akaigonga muhuri wake. Halafu akaandika barua kumjibu Mtume, akisema: “Ama
baad, nimeisoma barua yako na nimeyafahamu uliyoyaandika na unachokilingania.
Kwa yakini mimi najua kwamba kuna Mtume atakayekuja na nilikuwa nadhania kuwa
atatokea pande za Shamu. Na nimempokea vema mjumbe wako na ninakuletea zawadi
ya vigori wawili wenye heshima kubwa kwa Waqibtw. Na nimekupa zawadi ya nguo
na nyumbu utakayemtumia katika usafiri, wassalaam”. Muqauqis hakwenda mbele
zaidi ya hapo na Mtume akaipokea zawadi yake na kumfanya suria mmoja wa vigori
wawili wale. Naye ndiye mama Maariah aliyemzaa Sayyidina Ibrahim; mmoja wa
watoto watatu wa kiume wa Mtume.
ii.
Qayswar apeleleza ukweli
wa Mtume.
Ama Qayswar;
mfalme wa Urumi, huyu alitaka kupata ukweli na uhakika wa Mtume. Akatuma
mjumbe kumuitia kundi la wafanyabiashara wa Kiarabu waliokuja Shamu kufanya
biashara, wakaletwa mbele ya mfalme. Na miongoni mwao alikuwemo Abu Sufyaan
Ibn Harb na wakati huo alikuwa bado hajasilimu. Akaanza kumuuliza khabari za
Mtume, nae Abu Sufyaan akimueleza kwa ukamilifu kila anachokijua juu ya Mtume.
Baada ya usaili wake huo, ikambainikia kwamba Muhammad ni mtume wa Allah
kweli, akaupondokea Uislamu. Na akawaelezea khabari ya Uislamu wakubwa wa
Urumi wanao mzunguka katika baraza yake, akaona kwao uchukivu mkubwa. Nae
akajifanya kama kwamba alikuwa anataka kutahini imani yao na upeo wa
kushikamana kwao na dini yao. Na tunafikiri kwamba si vibaya iwapo tutakuletea
mapokezi ya Bukhaariy juu ya mazungumzo ya Qayswar na Abu Sufyaan. Kwani ndani
yake kuna sura ya wazi ya uchunguzi yakinifu na mfano mzuri kwa kila mwenye
kutaka kujua haki na ilivyo ndivyo/sawa katika mambo makubwa yanayompitikia.
Imepokewa kutoka kwa Abdullah Ibn Abbas-Allah awawiye radhi-“Kwamba Abu
Sufyaan Ibn Harb alimkhabarisha kwamba Hiraqli alimtumia ujumbe akiwa pamoja
na msafara wakifanya biashara Shamu. (Hii ilikuwa ni) katika kile kipindi cha
masitisho ya vita (kipindi cha suluhu ya Hudaybiyah) baina ya Mtume na
Makureishi. Basi wakamuitika akiwa Eliyaa, akawaita katika baraza yake
iliyokuwa imezungukwa na wakubwa wa Urumi. Akamuita mkalimani wake, akasema:
Ni nani kati yenu aliye karibu kinasabu na huyu mtu anayedai utume? (Abu
Sufyaan anasema) nikajibu: Mimi ndio niko karibu nae kinasabu kuliko wengine
wote hapa. Akaagiza nisogezeeni karibu mtu huyo na wasogezeni wenzake wakae
kwa kumpa mgongo. Halafu akamwambia mkalimani wake: Waambie mimi ninamuuliza
maswali mwenzenu huyu, akiniongopea mkadhibisheni. (Abu Sufyaan) anasema: Lau
kama si kuona haya kukadhibishwa basi ningemuongopea. Kisha swali la mwanzo
aliloniuliza likawa: Ikoje nasabu yake kwenu? Nikajibu: Yeye kwetu ni mtu
mwenye nasabu njema. Akauliza: Je, ulipata kuwepo ufalme kwa wahenga wake?
Nikajibu: Hapana, akauliza: Je, kuna mtu alipata kusema haya (ayasemayo) kabla
yake? Nikajibu: Hapana, akauliza: Je, ni watu watukufu ndio wamfuatao au ni
watu dhaifu (masikini)? Nikajibu: Watu dhaifu, akauliza: Je, wanazidi au
wanapungua? Nikajibu: Wanazidi, akauliza: Je, kuna ye yote anayetoka katika
dini yake kwa kuichukia baada ya kuingia? Nikajibu: Hapana, akauliza: Je,
mlipata kumtuhumu uwongo kabla hajasema ayasemayo sasa? Nikajibu: hapana,
akauliza: Je, anafanya khiana? Nikajibu: Hapana, nasi tumepeana nae muda wa
kusitisha vita, hatujui atafanya nini ndani yake. Akauliza: Je, mmewahi
kupigana nae? Nikajibu: Naam, akauliza: Yalikuwaje mapigano yenu nae?
Nikajibu: Vita baina yetu nae ni kupokezana, anatushinda nasi tunamshinda.
Akauliza: Anakuamrisheni nini? Nikajibu: Anasema muabuduni Allah peke yake na
wala msimshirikishe na cho chote na acheni itikadi ya baba zenu. Na
anatuamrisha kuswali, kusema ukweli, kuacha zinaa na kuunga udugu.
Akamwambia mkalimani
wake, mwambie: Nimekuuliza juu ya nasabu yake, ukasema yuna nasabu njema
kwenu, na hivyo ndivyo mitume walivyo, hutumwa katika nasabu za kaumu zao. Na
nikakuuliza: Je, kuna mtu alipata kusema haya (ayasemayo) kabla yake? Ukajibu
hapana, nikajisemea: Lau angelikuwepo aliyemtangulia kuyasema hayo,
ningelisema: Ni mtu anaye yaendeleza yaliyosemwa kabla yake. Nikakuuliza: Je,
ulipata kuwepo ufalme kwa wahenga wake? Ukajibu hapana, nikajisemea: Lau
ungelikuwepo ufalme kwa wahenga wake, ningelisema: Huyo ni mtu tu anayetaka
ufalme wa baba zake. Nikakuuliza: Je, mlipata kumtuhumu uwongo kabla hajasema
ayasemayo sasa? Ukajibu hapana, basi nikajua kwamba yeye hawezi kuacha
kuwaongopea watu, halafu akamuongopea Mungu. Nikakuuliza: Je, ni watu watukufu
ndio wamfuatao au madhaifu wao? Ukasema kwamba madhaifu ndio wamfuatao na hao
ndio wafuasi wa mitume. Na nikakuuliza: Je, wanazidi au wanapungua? Ukasema
kuwa wanazidi na hivyo ndivyo lilivyo suala la imani mpaka litimie. Na
nikakuuliza: Je, kuna ye yote anayetoka katika dini yake kwa kuichukia baada
ya kuingia? Ukasema hapana, na hivyo ndivyo imani ilivyo inapoziingia nyoyo.
Na nikakuuliza: Je, anafanya khiana? Ukasema hapana, na hivyo ndivyo walivyo
mitume, hawafanyi khiana. Na nikakuuliza: Anakuamrisheni nini? Ukasema
anakuamrisheni kumuabudu Allah na wala msimshirikishe na cho chote na
anakukatazeni kuabudu masanamu. Na anakuamrisheni swala, kusema ukweli na
kutokuzini. Ikiwa haya uyasemayo ni kweli, basi mtu huyo atamiliki mahala hapa
ilipokanyaga miguu yangu miwili hii nami nilkuwa najua kuwa atatokea. Na wala
sikudhania kwamba atatoka kwenu (Waarabu), basi lau mimi ningelimfikia
ningelijikalifisha kukutana nae. Na lau ningelikuwa mbele yake, ningeliiosha
miguu yake.
Ama Al-Haarith
Al-Ghasaaniy, huyu aliisoma barua ya Mtume, kisha akaitupilia mbali na
akaazimia kwenda kumuua Mtume. Qayswar akamuandikia barua ya kwamba asithubutu
kufanya hivyo. Ama mfalme wa Yamaamah, yeye akadhania kuwa ni suala la ufalme
na sio utume, akawa na tamaa na kupata sehemu ya ufalme huu. Akamuandikia
barua Mtume akimwambia: “Eeh uzuri ulioje wa unayoyalingania, basi nipe sehemu
ya jambo hili nitakufuata”. Mtume alipoisoma barua yake akasema: “Lau
angeliniomba tende mbichi iliyoanguka chini nisingelimpa”.
Hawa wafalme sita ndio
ambao Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliwapelekea ujumbe katika
mwaka wa saba. Na katika mwaka wa nane, alimtuma Al-Araai Ibn Al-Hadhwramiy
kupeleka waraka wake kwa Al-Mundhir Ibn Saawaa; mfalme wa Bahrein, huyu
akaupokea vema ujumbe na akasilimu. Na akamtuma Amrou Ibn Al-Aaswi kwa wafalme
wa Oman, nao pia wakasilimu. Akamtuma Al-Muhaajir Ibn Abiy Umayah kwa
Al-Haarith Al-Humeiriy; mfalme wa Sanaa, nae akasilimu. Na akawatuma Abu Mousa
Al-Ash-ariy na Muaadh Ibn Jabal kwenda kuulingania Uislamu Yemen, wakasilimu
wengi wa watu wa huko. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akamuandikia
waraka Jabalah Ibn Al-ayham; mfalme wa Ghasaan akimlingania Uislamu,
akasilimu. Kisha akaja kuritadi katika zama za ukhalifa wa Sayyidina Umar Ibn
Al-Khatwaab-Allah amuwiye radhi.
|