Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SOMO LA PILI

 Faida

  i.          Mtume kuwaandikia wafalme wa nchi zinazomzunguka, ilikuwa ni dalili tosha juu ya kudhihiri kwa haki na kushindwa kwa batili:

            Pengine jambo linalostaajabisha ni Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kuwalingania Uislamu wafalme hawa na ilhali Uislamu bado ni mchanga katika kisiwa cha Waarabu. Na bado haujakuwa na mihimili ya nguvu na mamlaka ya kumuwezesha kupambana na upinzani unaoweza kuonyeshwa na wafalme hawa wenye nguvu, utisho na mamlaka. Lakini Mtume hakuyafikira yote hayo, yeye alikuwa na yakini ya kutosha kwamba Allah Taala ataidhihirisha na kuipa ushindi dini yake na ataliinua neno lake. Na kwamba hapana shala atamtekelezea ahadi ya nusra na ushindi aliyompa na kwamba anachotakiwa yeye kukifanya ili Allah amtekelezee ahadi yake ni kuufikisha ujumbe wake kwa watu wote kwa juhudi zake zote: “...HAIKUWA JUU YAKO ILA NI KUFIKISHA (tu uliyoamrishwa)...” Ni kwa ajili hii ndio Mtume-Rehema na Amani zimshukie-hakusita kuwandikia waraka wa ujumbe wafalme hawa pamoja na ufalme mkubwa, mamlaka na nguvu walizokuwa nazo. Na huenda pia aliuhisi ufadhaifu wa maswahaba wake katika kuitekeleza kazi hii tukufu na msito wao katika kuziendea dola hizi zenye mali, nguvu na watu wengi. Akawatokea siku moja na kuwaambia: “Kwa yakini Allah amenitumiliza kuwa rehema kwa watu wote, basi nifikishieni (ujumbe wangu), Allah atakurehemuni. Na wala msikhitilafiane nami kama wanafunzi walivyokhitilafiana na Issa mwana wa Maryamu”. Wakauliza: “Ewe Mtume wa Allah, ikhtilafu yao ilikuwaje?”, akawajibu: “Aliwaitia hili ninalo kuitieni nyinyi hivi sasa, basi ama yule aliyemtuma eneo la karibu aliridhia na akasalimika (kufikwa na hukumu ya kumkhalifu Mtume wa Allah). Ama yule aliyemtuma (kufikisha ujumbe) eneo la mbali, akachukizwa na kujitia uzito (kama mfanyavyo nyinyi hivi sasa)”.

Mwachuoni Mulla Muhammad Aliy-Allah amrehemu-anasema: “Yakini na imani ya Mtume ya kupata ushindi/nusra haikutetereka na alikuwa na yakini thabiti kwamba Uislamu utaenea na kutawala mpaka nuru yake itazagaza pande zote za ulimwengu. Pamoja na udhaifu wa Uislamu kwa wakati huo, bado Mtume anawalingania kuingia katika dini yake wafalme wenye nguvu. Hakuyafanya yote hayo ila ni yakini na imani yake juu ya uwezo na nguvu zisizoshindika za Mola aliyemtuma kuifanya kazi hiyo. Hili ni jawabu zuri kwa lile kundi la waislamu ambao wana mashaka juu ya kufanikiwa kwa da’awah (wito/ujumbe) ya Uislamu katika ulimwengu wa Magharibi. Kwa hoja kwamba leo Uislamu unahitajia nguvu za kidunia na himaya/dola kuu litalalousaidia. Lakini hakika iliyo wazi ni kwamba Uislamu hauhitaji kusaidiwa, kwani wenyewe ni nguvu itishayo isiyoshindika”.

                ii.          Ukweli unaopasa kuzingatiwa na waislamu:

            Yawastahikia mno waislamu hivi sasa kuuzingatia uhalisia huu wa mambo na hakika/kweli hii. Kwamba ulimwengu wetu huu katika zama zetu hizi una kiu ya dini itakayo mfikisha mkiu (mwenye kiu) kwenye kata-kiu halisi na baridi. Kwani nguvu za kimaada zinazotakabari na kuufisidi ulimwengu katika zama zetu hizi, hazitofautiana sana na nguvu-maada za ulimwengu ule ulipodhihiri Uislamu. Dola kubwa za leo zinashabihiana na dola kubwa za enzi ya Mtume wa Allah; Urumi na Uajemi. Kama zilivyo sambaratika katika muda wa mpepeso wa jicho mbele ya nguvu za Uislamu. Basi hauko mbali wakati ambao Uislamu utapambana na Ulaya na Amerika na madola yote hayo kusalimu amri na nguvu-maada zao kuporomoka. Kwani dunia ni madola/nchi na historia hujirudia na zama ni mawimbi ya kiroho na kimaada na ya imani na ukafiri yenye kufuatana. Huenda pengine hili wimbi la mwamko na muasho linalosambaa kwa kasi ya moto nyikani katika ulimwengu wa Kiislamu. Ni bishara njema kwamba wimbi la imani limeshaanza kudhihiri/kuchomoza na kwamba wimbi la ustaarabu-maada lililoughuri ulimwengu kwa zama kadhaa. Umefika wakati wake wa kuondoka na kutoa nafasi kwa wimbi la imani kutawala: “...NA SIKU ZA NAMNA HII TUNAWALETEA WATU KWA ZAMU...” [3:140]

 



 | Tuandikie |