|
Vita vya Khaybar vilichukua takriban mwezi mmoja na nusu, kwani
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alikwenda huko mwanzoni mwa mwezi wa Muharram,
mwaka wa saba. Na kurudi kutoka huko mwishoni mwa mwezi wa Safar, akakaa
Madinah mwezi wa Rabiul-Awwal, Rabiut-thaaniy, Jumadaal-Uula,
Jumaadal-Aakhirah, Rajab, Shaaban, Ramadhan na Shawwal, miezi minane. Na miezi
yote hii minane ilipita katika hali ya utulivu na amani, hayakutokea ndani
yake matukio yo yote makubwa yanayotishia amani au kuleta madhara kwa
waislamu. Ila baadhi ya mapambano mepesi mepesi baina ya waislamu na makabila
ya Kiarabu katika vitongoji vilivyouzunguka mji wa Madinah. Uchokozi wa watu
hawa wachache, ulimlazimisha Bwana Mtume kutuma sariya (kikosi cha askari)
kuyatia adabu makabila hayo madogo madogo. Pamoja na kuuawa kwa baadhi ya
askari hawa wa Bwana Mtume mapambanoni, hali ya mambo kwa ujumla wake ilikuwa
ikitengenea siku hata siku. Na haiba (utisho) ya waislamu ikaendelea kukita
katika nafsi za watu na wigo wake ukizidi kutanuka.
i.
Mtume wa Allah achukua
hatua za tahadhari dhidi ya usaliti unaoweza kujitokeza upande wa Makurayshi:
Ulipoandama mwezi wa Dhul-Qa’adah wa mwaka huu wa
saba, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaanza kufanya maandalizi kwa
ajili ya Umrah ya Qadhaa. Hii ndio ile Umrah waliyowafikiana na Makureishi
katika suluhu ya Hudaybiyah, kwamba mwaka ule asiingie Makah na badala yake
aje mwakani. Kwa hivyo Mtume akawaamuru maswahaba wake kujiaandaa kwenda
kukidhi Umrah yao na kwamba asibakie hata mtu mmoja katika wale wote
waliokuwepo Hudaybiyah mwaka jana. Kwa kauli hii ya Mtume, hakuna hata mtu
mmoja aliyebakia nyuma asitoke na Mtume ila wale waliokufa au kuuliwa Khaybar.
Pia walitoka pamoja na Mtume waislamu wengine ambao hawakuwa wamehudhuria
Hudaybiyah. Idadi jumla ya waislamu katika msafara huu wa Umrah ya Qadhaa
ilikuwa watu alfu mbili ukiachilia mbali watoto na wanawake. Mtume wa Allah
akamtawadha ukaimu wa Madinah, swahaba wake Abu Dharri Al-Ghifaariy. Akaswaga
ngamia sitini wakiwa ni wanyama wa sadaka na kuhirimia mlangoni mwa msikiti,
kisha huyoo akashika njia akileta talbiyah na waislamu kuitikia nyuma yake.
Na katika jumla ya masharti waliyopewa ni kutokuchukua silaha
yo yote zaidi ya panga zao zikiwa ndani ya ala zake. Lakini Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alichelea usaliti wa Makureishi, akachukua
silaha, kofia za chuma, deraya na mikuki. Na akawaswaga farasi mia kwa ajili
ya kuwasaidia iwapo vitazuka vita. Akamteua kuongoza suala la silaha Bashri
Ibn Sa’ad na farasi akapewa Muhammad Ibn Maslamah. Walipofika Dhul-Hulayfah;
kitongoji kilicho umbali wa kiasi cha maili nane kutoka Madinah,
akazitanguliza mbele yake silaha na farasi. Muhammad Ibn Maslamah akaenda na
farasi mpaka “Marid-dhwahraan”; mahala palipo umbali wa mwendo wa siku moja
kutokea Makah. Hapo akalikuta kundi la Makureishi ambao walimuuliza sababu ya
kuja na farasi, akawajibu: Huyoo Mtume wa Allah atapambazukiwa katika kambi
hii kesho, inshallah. Tena hawa Makureishi wakamuona Bashir Ibn Sa’ad akiwa na
silaha nyingi, wakatoka wangu wangu kuwaendea wenzao. Wakawapasha khabari ya
silaha na farasi waliowaona, Makureishi wakafadhaika na kusema: “Wallah, sisi
hatujapanga njama zo zote dhidi yao nasi bado tuko katika mkataba na
ahadi yetu. Basi ni kwa lipi Muhammad na maswahaba wake wanataka kutupiga?!’
ii.
Makureishi watishwa na
uchukuzi wa silaha:
Makureishi
wakamtuma Mukriz Ibn Hafswi kuliongoza kundi la Makureishi kwenda kwa Mtume wa
Allah, wakamwambia: “Ewe Muhammad! Hukupata kujulikana utotoni wala hivi
ukubwani kuwa na sifa ya usaliti/khiana. Unathubutu kuingiza silaha kuwadhuru
jamaa zako na ilhali mlishurutiziana kwamba usiingie na silaha ila silaha ya
msafiri; panga zikiwa zimefutikwa alani?!” Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akawajibu: “Hakika mimi siingizi silaha kuwadhuru”. Mukriz Ibn
Hafswi akasema: “Hivi ndivyo unavyojulikana kwa wema na utekelezaji wa ahadi”.
Kisha akarejea Makah mbio akiwa na ujumbe wake, akawaambia wenzake: “Hakika
Muhammad bado anaheshimu masharti mliyowekeana nae”. Makureishi waliposikia
hivyo, wakashusha pumzi na kumpisha njia ili aweze kutekeleza Umrah yake kama
walivyokubaliana.
iii.
Makureishi wakinzana kwa
kumuona Mtume na maswahaba wake wakifanya Umrah:
Baadhi ya
wapokezi wa Sira-Allah awarehemu-wanasema: Kwamba Makureishi walitoka mjini na
kwenda majabalini na kumuachia Mtume mji wa Makah na wakasema: Hatutaki
kumuona yeye wala maswahaba wake. Wengine wanasema: Kwamba walitoka kwenda
kumuangalia vileleni mwa majabali ili muradi zimesemwa takriban kauli sita
katika suala hili. Kwa ujumla ni kwamba wale watu watukufu/viongozi wa
mushrikina walijificha wakichukia kumuona Mtume akiingia Makah kifua mbele.
Kitendo ambacho walikihesabu kuwa ni kushindwa na hasimu yao huyu mkubwa.
Wakati ambapo watu wa kawaida walikuwa na shauku kuu ya kumuona Mtume na
maswahaba wake wakiingia Makah. Kwani khabari zilikwishatangaa baina yao
kwamba Mtume na maswahaba wake wamedhoofishwa na homa ya Yathrib kiasi cha
kushindwa hata kusimama. Kwa ajili hii, watu wakasukumwa kwenda kuwaona
madhaifu, wakondefu hawa ili wawakejeli na kuwacheza shere. Lakini Mtume na
maswahaba wake walipoingia, hali ya afya zao ilikuwa kinyume na uvumi ulioenea
miongoni mwao, kwani walikuwa na afya njema na walionekana kuwa na nguvu.
|