|
Ukweli ni
kwamba kuingia kwa Mtume na maswahaba wake Makah, kulikuwa ni mandhari inayo
lazimisha kutafakari na kustaajabu pamoja. Kwani Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-aliingia Makah akiwa na doria inayokodosha macho na kuziroga akili.
Yeye alikuwa amempanda ngamia wake; Al-Qaswaa na waislamu wakiwa wamevaa
mapanga yao wamemzunguka kila upande wakimlinda dhidi ya lo lote linaloweza
kufanywa na Makureishi. Wakipaaza sauti za talbiyah: “LABBAYKAL-LAAHUMMA
LABBAYKA!”, na Abdullah Ibn Rawaahah akishika hatamu za ngamia wa Mtume
akiimba beti za mashairi. Hata walipofika “Haram” ya Makah, Mtume akamwambia:
“Eeh ewe Ibn Rawaahah! Sema: LAA ILAAHA ILLAL-LAAHU WAHDAU, SWADAQA WA’ADAU WA
NASWARA ‘ABDAU WA A’AZZA JUNDAU WAHAZAMAL-AHZAABU WAHDAU (badala ya kuimba
mashairi)”. Ibn Rawaahah akaanza kusema maneno hayo aliyofundishwa na Mtume na
watu wakimuitika nyuma yake kwa hamasa na mori mkuu. Na mwangwi ukizianikiza
sauti zao hizo pande zote za mji wa Makah na zikigonga ngoma za masikio ya
wale waliotoka ili wasizikie wala kuuona msafara wa Mtume ukiingia Makah.
SOMO LA NNE.
i.
Mtume wa Allah na
maswahaba wake wadhihirisha nguvu yao kwa maadui zao:
Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akiujua uvumi ulioenezwa dhidi yake na
maswahaba wake. Kwa ajili hii, akawausia maswahaba wake ya kwamba isionekane
kwao dalili yo yote ya uchovu/unyonge. Na akawaamrisha kuvaa rubega na kwenda
matiti (mbiombio) katika twawafu ili mushrikina wauone ukakamavu na nguvu yao.
Mtume wa Allah akaingia Masjidil-Haraam akiwa kavaa rubega na waislamu wakivaa
kama yeye, akaenda mpaka akaligusa “Hajarul-Aswad” kwa fimbo yake ndogo na
kusema: “Allah amrehemu mtu ambaye amewaonyesha (makafiri) leo nguvu”. Kisha
akaondoka akienda mbiombio kuizunguka nyumba tukufu ya Allah na maswahaba
wakimfuatia mpaka zikamalizika mara tatu za mwanzo. Halafu ndipo
alipowatembeza mwendo wa kawaida katika mara nne zilizobakia ili kukamilisha
mizunguko saba ya Twawafu. Mushrikina wakapatwa na mshangao mkubwa walipoiona
nguvu, ukakamavu na uchangamfu wa waislamu. Wakapigana vikumbo wanaume,
wanawake na watoto kuzunguka msikiti mtukufu wakigombea kuwaona waislamu
wakitufu huku wakiambizana: “Ni hawa ndio mlidai kwamba homa imewadhoofisha?!
Hakika wao wanachapusha mwendo kama anavyochapua swala”.
Walipomaliza kutufu,
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikwenda na maswahaba wake katika
eneo la ibada ya Sa’ayi (kwenda baina ya vilima Swafaa na Marwaa). Akafanya
sa’ayi akiwa amempanda ngamia wake mpaka akamaliza mara saba. Alipoikamilishia
Marwaa ile mara ya saba, Mtume alisimama akasema: “Hapa ndio mahala pa
kuchinjia wanyama wa sadaka na njia zote za Makah ni mahala pa kuchinjia”.
Kisha ndipo alipomchinja hapo Marwaa mnyama wake wa sadaka na wakashirikiana
nae katika mnyama huyo waislamu waliohudhuria Hudaybiyah. Aliyempata ngamia
alichinja ngamia na asiyepata alicihinja ng’ombe kutokana na uadimu wa ngamia
wakati huo. Halafu tena ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-aliponyoa akifuatiwa na maswahaba wake na kwa tendo hili la kunyoa,
wakawa wamefungukana na Umrah yao.
Na ikumbukwe kwamba
farasi na silaha zilikuwa zimeachwa katika eneo la karibu liitwalo “Ya’ajaj”
umbali wa maili nane kutokea Makah. Na wakaachwa watu mia mbili kulinda,
waislamu walipokamilisha Umrah yao, Mtume akawatuma maswahaba mia mbili kwenda
huko ili kulinda silaha na farasi. Ili kutoa nafasi kwa walinzi wa mwanzo kuja
kutekeleza ibada ya Umrah.
ii.
Bilali aadhini juu ya
Al-Ka’abah:
Kisha Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaingia ndani ya Al-Ka’abah na
kukaa humo mpaka ukaingia wakati wa swala ya Adhuhuri. Akamuamuru Sayyidina
Bilali-Allah amuwiye radhi-kuadhini juu ya Al-Ka’abah. Kitendo cha Bilali, mtu
mweusi tena mtumwa kupanda juu ya Al-Ka’abah tukufu na kutoa wito mtukufu
(adhana) kiliwaudhi na kuwaghadhibisha upeo Makureishi. Kiasi cha kufikia
Suhail Ibn Amrou na wenziwe aliokuwa nao kufunika nyuso zao pale waliposikia
adhana. Ikrimah Ibn Abu Jahli yeye akashindwa kabisa kuvumilia, akasema: “Kwa
yakini Allah amemkrimu Abul-Hakam (baba yangu) kwa kumfisha mapema, hakufika
kumsikia mtumwa huyu akiyasema haya ayasemayo!” Na Swafwaan Ibn Umayyah
akasema: “Kila himda njema zinamstahikia Allah aliyemfisha baba yangu kabla ya
kuyaona haya!” Na Khalid Ibn Useid yeye akasema: “Kila himda njema ni milki
yake Allah aliyemfisha baba yangu kabla ya kuiona siku hii (ya aibu), mpaka
(mtumwa) Ibn Ummu Bilali anapiga ukelele wa punda juu ya Al-Ka’abah!”
|