Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

III. MANDHARI YA WAISLAMU YAWAOGOPESHA MAKURAYSHI DHIDI YA DINI YAO :

 Faida

           Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-na maswahaba wake-Allah awawiye radhi-wakakaa siku tatu walizo shurutiana na Makureishi. Wakienda na kurudi katika pande zote za mji wa Makah kwa amani na salama. Ndani ya siku tatu hizi, watu wa Makah waliona mandhari ya nguvu na mshikamno baina ya waislamu. Na wakaona kila dalili za wema, mahaba na ukweli wa hali ya juu baina ya waislamu na Mtume wa Allah. Kiasi cha kuwakodosha macho na kuwatunduwaza na nyoyo zao zikijaa mshangao wa dini hii ambayo imeanza kupata nguvu kubwa baada ya unyonge/udhalili wa kutupwa. Ikaanza kupendwa baada ya kuchukukiwa upeo na ikatoka katika kukimbiwa na kupewa mgongo ikaingia katika mshikamano na umoja. Na wakashangazwa mno na Mtume huyu asiyejua kusoma wala kuandika kuweza kuunda umoja wenye nguvu kutokana na makundi tapanyika haya. Nguzo za umoja huo zikiwa ni kuoneana huruma na kushikamana, lengo lake likiwa ni kheri na kutengenea na msingi wake ni kumuabudu Allah asiye na mshirika.

Kutokana na yote haya, watu wa Makah wakachelea kufitinishwa dini yao na waislamu, kabla kidogo ya kumalizika siku tatu za mkataba, akaja Suhail Ibn Amrou na Huwaytwib Ibn Abdil-Izzaa, wakamwambia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Muda wako umekwisha, tuondokee”. Mtume wa Allah akataka kuzizoesha nyoyo za Makureishi na alikwishahisi kazi iliyofanywa na Uislamu ndani yao, akawaambia wawili wale: “Mtakuwaje lau mtaniachia nikaingia kwa Bi. Harusi hapa kwenu nasi tukakuandalieni chakula mkakila?” – Ikumbukwe kwamba Bwana Mtume wakati akiwa Makah alikuwa amemposa Maimunah Bint Al-Haarith na alikuwa bado hajaingia nyumbani – Watu wawili wale wakadiriki khatari inayowajongelea wao na dini yao pindi wakiendelea kuzungumza na Muhammad. Na kwamba watakapojumuika nae katika walima wa harusi na katika hali ya kuliwazika na mkwe mpya anayetaka kuweka kigingi cha mafungamano. Basi hapana shaka kwamba wao watashindwa nae na hapana wasiwasi juu ya uwezo wake katika kuwamiliki wao kutokana na nguvu ya nafsi yake na utamu wa maneno yake. Na kwamba anaweza kabisa kuvivunjilia mbali vizuizi vyote walivyo jiwekea na khususan ni baada ya athari yake waliyoiona watu na baada ya watu wengi kuvutika na Uislamu.

Haya ndio mawazo yaliyokuwa yakijiri katika fikra za watu wawili hawa, wakasema kwa upesi: “Sisi hatuna haja na chakula chako. Tuondokee, tunakuomba kwa ahadi iliyo baina yetu utoke katika ardhi yetu, hizi siku tatu tayari zimemalizika”. Ugumu na ukali huu wa maneno ulioonyeshwa na watu hawa, ukaziamsha hasira za Sa’ad Ibn Ubaadah; kiongozi wa Answaar, akamuinukia Suhail Ibn Amrou akiwa ameghadhibika na kumwambia: “Umesema uwongo wewe, huna mama wewe! Hii sio ardhi yako wala ya baba yako. Wallah hataacha kuwa hapa ila ataondoka kwa radhi yake”. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akatabasamu, kisha akasema: “Ewe Sa’ad! Usiwaudhi wageni waliotutembelea kambini kwetu”. Halafu Mtume akaamrisha watu wajitayarishe kwa msafara wa kurudi Madinah, watu wote wakaondoka kuelekea “Sarifa”. Hili ni mojawapo ya maeneo ya vitongoji vya Makah, lililo karibu na “Tan-eem” kiasi cha maili tisa kutoka Makah. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa  amemposa Maimunah Bint Al-Haarith, aliyekuwa miongoni mwa wanawake watukufu wa Kikureishi. Dada yake; Ummul-Fadhli Bint Al-Haarith alikuwa ni mke wa Al-Abbas Ibn Abdul-Mutwalib. Kwa hivyo Sayyidina Al-Abbas ndiye aliyetawalia kumuoza kwa Mtume, nae Bwana Mtume akaingia nyumbani hapo “Sarifa”.

 

                   iv.          Umrah hii ya Qadhaa ilikuwa ni vita ya moyo kwa watu wa Makah:

           Naam, hivi ndivyo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alivyoondoka Makah, akiacha nyuma athari kubwa. Zikaifungukia dini yake nyoyo kukutavu, kundi miongoni mwao likistaajabishwa na utekelezaji ahadi wa Mtume pamoja na kuwa na uwezo wa kuvunja au kubadili. Na kundi jingine lilivutiwa na mtindo wa dini hii na huruma ya Uislamu kwa wafuasi wake. Na utii na utulivu mzuri baina ya waislamu na Mtume wao. Na kundi jingine likaona kuwa nyota njema inaelekea kuwa ni fungu la Uislamu, kwa hivyo wakaonelea ni vema wakajiegemeza mapema kwenye njia ya salama na amani. Ikutoshe kwamba Umrah hii ya Qadhaa imekuwa ndio sababu ya kusilimu kwa Khalid Ibn Al-Waleed na Amrou Ibn Al-Aaswi.

 



 | Tuandikie |