|
i.
Khalid na Amrou ndio
waliokuwa mashujaa wa Makureishi na tegemeo lao vitani na walikuwa miongoni
mwa maadui wakubwa wa Mtume:
Huenda Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-hakupata kuwafurahikia watu waliosilimu
baada ya Hijrah, kama alivyowafurahikia Khalid Ibn Al-Waleed na Amrou Ibn
Al-Aaswi. Watu wawili hawa walisilimu baada ya Umrah ya Qadhaa, katika mwezi
wa Safar (Mfunguo nne) wa mwaka wa nane. Furaha ya Mtume wa Allah kwa kusilimu
kwa watu hawa ilikurubia kulingana na furaha yake wakati waliposilimu Umar Ibn
Al-Khatwab na Hamzah Ibn Abdul-Mutwalib kabla ya Hijrah.
Watu wawili hawa; Khalid na Amrou walikuwa na daraja na utajo
mkubwa kwa upande wa Makureishi, walikuwa ni miongoni mwa nguzo zao madhubuti.
Ama huyu Amrou, yeye alikuwa ni katika kile kizazi bora cha Waarabu katika
uelekevu na siasa na wepesi katika kushughulikia masuala tata. Khalid yeye
alikuwa ni miongoni mwa weledi na mabingwa katika masuala ya vita nae ndiye
aliyepewa dhima ya kuongoza kikosi cha farasi katika enzi za jahilia.
Waliposilimu, nguvu ya Makureishi ikadhoofika kwa kiwango kikubwa mno kiasi
cha kulitia ufa wa kutisha jengo lao. Jengo hili la Makureishi likaelekea
kuanguka na hatimaye kuanguka kabisa baada ya miezi sita tu. Kama ambavyo
kusilimu kwa mashujaa wawili hawa-Allah awawiye radhi-kulivyo idhoofisha
janibu ya Makureishi, ndivyo kulivyoiimarisha janibu ya waislamu.
ii.
Kila mmoja; Khalid na
Amrou alikuwa anafikiria kuhama Makah na kwenda kuishi ughaibuni:
Tukirejea nyuma kila mmoja wa watu wawili hawa
alikuwa amejawa na chuki kuu dhidi ya Mtume-Rehema na Amani zimshukie-kiasi
cha kufikia kutamani kumtafuna akiwa hai. Walikuwa ni wapinzani wake wakuu,
wakiipinga dini yake sana kuliko Makureishi wengine. Chuki na upinzani huu,
ukamfikisha Khalid kushindwa kukaa Makah wakati Mtume akiwa humo akifanya
Umrah ya Qadhaa. Akatoka Makah akiwa hana muelekeo maalumu ili muradi asiweze
kuona wala kusikia khabari zo zote za Mtume. Tangu katika suluhu ya
Hudaybiyah, yeye alianza kufikiria mahala pa kuhamia pale Makah itakapoingia
mikononi mwa mtume. Kwani yeye kutokana na hali ya mambo ilivyokuwa ikijiri,
alikuwa na yakini kabisa kwamba hatimaye ushindi utakuwa ni fungu la Mtume,
Khalid mwenyewe anasimulia: “...(Mtume) alipofanya suluhu na Makureishi pale
Hudaybiyah, nilijisemea nafsini mwangu: Kimebakia kitu gani? Niende wapi sasa?
Je, niende kwa mfalme Najaashi, kwani huko Muhammad na maswahaba wake walipewa
amani. Au niende kwa Hiraqli na huko niiache dini yangu na kuufuata unaswara
au uyahudi? Au niende nje ya Bara Arabu au nijifungie nyumbani kwangu muda wa
kusalikia uhai wangu?” Hakika huu ulikuwa ni mtosheo mkuu uliomkumba Khalid
kiasi cha kumuhemeza asijue la kufanya wala pa kwenda.
Amrou nae kwa upande wake, alikuwa akifikiria kuhama kabisa
Arabuni kwa sababu tu ya kumchukia Mtume. Na kuikimbiza nafsi yake, heshima na
dini yake visije angukia chini ya utawala/mamlaka ya Muhammad. Amrou nae
anasimulia, anasema: “...Ilipo fanyika suluhu ya Hudaybiyah na Mtume
akaikubali na kuipitisha, nikawa najisemea: Mwaka ujao Muhammad anaingia Makah
na maswahaba wake! Makah hapafai tena kukaa wala Twaif na wala hapana kitu
bora kama kuondoka! Nami bado ni mbali na Uislamu na naona hata lau Makureishi
wote watasilimu, mimi sitasilimu. Nikawakusanya watu wanaonikubali na
kunisikiliza katika kaumu yangu na wakinitanguliza katika mambo yao,
nikawauliza: Nyinyi mnajua kwamba mimi wallah kwa yakini naona jambo (dini)
hili la Muhammad linaelekea kuyashinda mambo yote kwa kiasi cha kutisha. Basi
mimi naonelea ni vema tukaungana na mfalme Najaashi, ikiwa Muhammad atashinda
sisi tutabakia huko huko. Kwani kuwa chini ya mamlaka ya Najaashi ni bora
kwetu kuliko kuwa chini ya Muhammad. Na iwapo itashinda kaumu yetu, sisi
wanatujua kwa hivyo haitatujia kutoka kwao ila kheri. Wakasema: “Hiyo ndio
fikra ya sawa sawa”.
Hivi ndivyo watu wawili hawa walivyokuwa wakifikiria kuhama kutoka katika
ardhi ya Waarabu, pale ilipowabainikia kwamba nyota ya Muhammad inaelekea
kunga’ara. Na kwamba nyota ya Makureishi inaendea kuzimika na kwamba hapana
shaka wala nguvu ya kuizuia dini ya Muhammad kuishinda dini ya Makureishi.
Lakini Allah ambaye funguo za nyoyo anazitamalaki yeye, alikwisha waandaalia
sababu zilizofungua nyoyo zao kuuelekea Uislamu kwa namna wasiyoitazamia.
|