Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

AMROU : KUTOKA DHAMIRA YA USALITI KWENDA KWENYE UISLAMU

 Faida

 iii.               Amrou abadilika kutoka katika dhamira ya usaliti na kuukumbatia Uislamu:

           Ama Amrou, yeye alihajiri kwenda kwa mfalme Najjaashi wa Uhabeshi akiwa na kundi la wenzake walio ambatana nae. Kufika kwake huko kukasadifiana na kufika kwa Amrou Ibn Umayyah; mjumbe maalumu wa Mtume kwa Najaashi. Mjumbe huyu alikuwa ameleta barua ya Mtume aliyo muandikia Najaashi, hapo ndipo Amrou Ibn     Al-Aaswi akadhania kwamba hiyo ndio fursa adhimu ya kumshambulia mjumbe wa Mtume. Kwa mashambulizi hayo, atakuwa ameiponya chuki/ghadhabu ya moyo wake na atakuwa ametoa msaada usio sahaulika milele kwa Makureishi. Amrou mwenyewe anahadithia: “Basi nikawaambia wenzangu: Huyoo ni Amrou Ibn Umayyah! Lau ningeingia kwa Najaashi nae akanipaye, basi ningeliipiga shingo yake, kwa yakini Makureishi wangeliona kuwa mimi nimewatoshea kwa kumuua mjumbe wa Muhammad. Basi nikaingia na kumsujudia kama nilivyokuwa nikifanya (hapo kabla), akasema: Karibu rafiki yangu! Je, umeniletea hadiya (zawadi) yo yote kutoka nchini mwako? Nikamjibu: Naam, nyingi mno. Nikampa zikamstaajabisha na akazipenda, nilipoona uzuri wa nafsi yake, nikasema: Ewe mfalme wee! Hakika mimi nimemuona mtu mmoja akitoka kwako nae ni mjumbe wa adui yetu aliye tudhulumu. Akaua watukufu wetu, basi naomba unipe mtu huyo ili nipate kumuua. Akaghadhibika, akaunyanyua mkono wake na kuipiga pua yangu pigo ambalo nilidhania kuwa kaivunja. Mionzi/tundu za pua yangu zikachuruzika damu, basi nikawa naifuta damu hiyo kwa nguo yangu. Basi ukanipata udhalili ambao lau ardhi ingenipasukia ningeliingia ndani yake kwa kumchelea, halafu nikasema: Ewe mfalme wee! Wallah, lau ningeliyakinisha kuwa wewe unalichukia hili, basi nisingeliomba. Akasema: Hivi wewe unaniomba nikupe mjumbe wa mtu ambaye anajiwa na malaika mleta wahyi ambaye alikuwa akimjia Musa-Amani iwashukie-ili umuue?”

Amrou anaendelea kusimulia: “Basi Allah akaubadilisha moyo wangu kutoka katika dhamira mbaya niliyo kuwa nayo na nikajisemea: Huyu ameitambua haki na Waarabu na wasio waarabu nawe unaikhalifu? Kisha nkauliza: Ewe mfalme unalishuhudia hilo? Akajibu: Naam, ninalishuhudia hilo mbele ya Allah ewe Amrou,basi nakuomba unitii na umfuate. Wallah, kwa yakini yeye yuko katika haki na bila ya shaka atawashinda wapinzani wake wote kama Musa alivyo mshinda Firauni na jeshi lake. Nikamuuliza: Je, unanipa kiapo cha utii kwake juu ya Uislamu? Akajibu: Naam, akaukunjua mkono wake na akanipa ahadi ya utii kwa Uislamu, kisha akaagiza tasa la maji, akanisafisha damu na kunivika nguo nyingine. Halafu tena nikatoka nikimkusudia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-basi nikakutana na Khalid Ibn Al-Waleed. Na hiyo ilikuwa ni kabla ya Fat-hi Makah, nikasuhubiana nae mpaka tukafika Madinah”.

 

                   iv.               Khalid abadili azma ya kuukimbia Uislamu na badala yake aukimbilia:

           Ama Khalid, yeye aliendelea kubakia katika hali ya kutoshewa na kuhemewa, akifikiria upande wa kuelekea. Alibakia katika hali hiyo mpaka Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaingia Makah katika Umrah ya Qadhaa, akatoka nje ya Makah asishuhudie kuingia kwa Mtume wa Allah, Khalid anahadithia: “Na ndugu yangu Al-Waleed alikuwa amengia pamoja nae (Mtume), akanitafuta asinipate, akaamua kuniandikia ujumbe, tahamaki kumeandikwa: Kwa jina la Allah Mwingi wa Rehema Mwenye kurehemu. Ama baad, hakika mimi sijapatapo kuona ajabu zaidi kuliko kuukataa kwako Uislamu na ilhali wewe una akili kubwa. Na mithili ya Uislamu hajingikiwi nao mtu ye yote na Mtume wa Allah ameniuliza kuhusu wewe, akasema: Yu wapi Khalid”, nikamjibu: Allah atamleta, akasema: Mtu kama yeye si wa kujingikiwa na Uislamu, lau angeli ziunganisha nguvu zake pamoja na waislamu dhidi ya mushrikina, ingelikuwa ni kheri kwake, nasi tungelimtanguliza mbele. Basi nakusihi ewe ndugu yangu uzidiriki kheri zilizo kufutu (pita). Uliponifikia ujumbe wake huo, nikapata nguvu ya kutoka na ukanizidishia raghba ya Uislamu na yakanifurahisha mno maneno ya Mtume wa Allah. Basi nikaota usingizini kama kwamba niko kwenye mji finyu wenye ukame, nikatoka kwenda kwenye mji wenye neema na wasaa”.

 

                     v.               Sadfa yenye kunadi saada:

             “Nilipo azimia kutoka kwenda Madinah, nikakutana na Swafwaan Ibn Umayyah, nikamwambia: Ewe babie Wahbi, hivyo wewe huoni kuwa Muhammad amewashinda Waarabu na wasio waarabu? Basi lau tungelimuendea na tukamfuata, kwani heshima yake ndio heshima yetu! Akanikatalia vikali kabisa na akasema: Hata kama watu wote watamfuata mimi sitamfuata abadan. Nikajisemea: Huyu ni mtu aliye changanyikiwa, baba na kaka yake waliuliwa katika vita vya Badri. Na nikakutana na Ikrimah Ibn Abu Jahli, nae nikamwambia maneno kama niliyo mwambia Swafwaan. Nae akanijibu kama nilivyojibiwa na Swafwaan, nikajisemea: Yafiche niliyo kwambia, akasema: Sitayataja. Halafu nikakutana na Uthman Ibn Twal-hah, nikajisemea: Huyu kwangu mimi ni rafiki; basi nikapenda nimwambie. Kisha nikakumbuka kuuawa kwa baba yake; Twal-hah na ami yake Uthman na nduguze wanne, kwani wote hao waliuliwa katika vita vya Uhud. Kwa ajili hiyo, nikaona vibaya kumwambia, kisha nikamwambia hali halisi ilivyo: Hakika si vinginevyo, sisi hivi sasa ni mithili ya mbweha aliye shimoni, lau atamwagiwa ndoo ya maji basi bila ya shaka atatoka nje. Halafu tena ndipo nilipomwambia yale niliyo waambia akina Swafwaan na Ikrimah. Akaniitika haraka kinyume na matarajio yangu, basi haikuchomoza alfajiri mpaka tukakutana “Baiajaj”, tukadamka mpaka “Al-Haddah”. Hapo tukamkuta Amrou Ibn Al-Aaswi, akasema: Karibuni watu nyie! Tukamjibu: Nawe karibu! Akatuuliza: Mnakwenda wapi? Tukamjibu: Tunakwenda kuingia katika Uislamu, akasema: Nami hilo ndilo lililo nileta. Tukaambatana sote mpaka tukaingia Madinah”.

 

                   vi.               Mtume wa Allah afurahishwa mno na kusilimu kwa mashujaa wawili hawa:

            Walipowasili Madinah, wakashukia nje ya mji, Mtume akapashwa khabari yao, akafurahi mno na akawaambia maswahaba wake: “Makah imekupeni bora ya watoto wake”. Khalid anasema: “Basi tukavaa nguo zetu zilizo nzuri kabisa, kisha tukatoka kwenda kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Nikakutana na ndugu yangu; Al-Waleed, akaniambia: Harakisha, kwani Mtume wa Allah amefurahishwa na ujaji wenu na anakungojeeni. Tukachapusha mwendo, nikamchomozea Mtume, basi aliendelea kutabasamu mpaka tukasimama mbele yake. Nikamwamkua kwa maamkuzi ya utume, nae akaiitikia salamu yangu kwa uso mkunjufu. Nikasema: Hakika mimi ninashuhudia kwamba hapana afaaye kuabudiwa kwa haki ila Allah na kwamba wewe ni Mtume wa Allah. Akasema (Mtume): “Himda zote njema zinamstahikia Allah aliye kuongoa”. Mimi nilikuwa naona kuwa una akili kubwa sana, nikataraji haita kusalimisha ila kwenye kheri”. Nikasema: Ewe Mtume wa Allah wee! Niombee Mungu anisamehe mapambano niliyo yaendesha dhidi yako! Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Uislamu unayakata yote yalio kuwa kabla yake”. Amrou na Uthman nao wakaenda mbele na kula kiapo cha utii kwa Mtume wa Allah”.

Amrou Ibn Al-Aaswi nae anasema: “Wallah, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-hakutulinganisha mimi na Khalid katika masuala muhimu na ye yote miongoni mwa maswahaba wake tangu tuliposilimu. Na tulikuwa na daraja hiyo hiyo katika ukhalifa wa Abu Bakri. Na nilikuwa katika hali hiyo zama za Umar na Umar kwa Khalid alikuwa kama ni mtu mwenye kulaumu”.

Kwa yakini Uislamu ulijipatia nguzo kuu mbili na mashujaa wawili kutokana na kusilimu kwa Khalid na Amrou. Mashujaa hawa walitoa mchango mkubwa sana katika historia nzima ya ushindi wa Uislamu. Na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliendelea kumtawalisha Khalid kikosi cha farasi kama alivyo kuwa akitawalia katika zama za jahilia. Na akamuita: “panga la Uislamu”, nae akawa ni upanga uliotolewa na Allah kuwafyeka makafiri-Allah amuwiye radhi na maswahaba wote pia. 

 



 | Tuandikie |