Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SURA YA KUMI NA MOJA
SARIYYA YA MU'UTAH

 Faida

 SOMO LA KWANZA.

 

         i.        Vita vya Mu'utah vilikuwa ni matokeo ya barua za da'awah zilizo pelekwa kwa wafalme:

         Vita hii ilikuwa katika mwezi wa Jumaadal-Uula (Mfungo Nane) mwaka wa nane wa Hijrah sawa na mwezi Septemba/629 A.D., kiasi cha miezi mitano tu baada Umrah ya Qadhaa. Imamu Bukhaariy na Ibn Is-haaq-Allah awarehemu-wameviita vita hivi kwa jina la "vita (ghazwah) vya Mu'utah" badala ya "sariyah ya Mu'utah" kutokana na wingi wa jeshi la waislamu katika vita hivi. Hata kama Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-hakushiriki na "Mu'utah" ni kimojawapo ya vijiji/vitongoji vya           "Al-Bulqaa" katika mipaka ya Shamu kwa upande wa Hijaaz. Kiasi cha umbali wa mwendo wa makambi mawili kutokea Baytul-Maqdis (Jerusalem), mashariki mwa bahari iliyo kufa (dead sea).

Sariyah hii ilikuwa ni natija ya da'awah (ujumbe wa Uislamu) ulio elekezwa na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa wafalme wa Peninsula ya Kiarabu na maeneo ya pembezoni mwake. Wajumbe wa Mtume waliwapelekea barua zake wafalme hao, basi wako miongoni mwao walio upokea  vema ujumbe huo wa Mtume na wakasilimu. Wengine walizuiwa na mazingira yaliyo wazunguka kuuitikia ujumbe huo, lakini hilo halikuwa pelekea kutokuwapokea vema wajumbe walio tumwa kwao. Wako pia walio upokea ujumbe kwa ugumu na ukukutavu wa moyo lakini bila ya kumdhuru mjumbe, hilo lilitokana na mazoea/kanuni ya kisiasa baina ya mataifa. Kanuni inayo hukumu kuheshimiwa mjumbe kwa hali yo yote, kwani dhima ya mjumbe ni kufikisha tu ujumbe aliotumwa kwa mlengwa. Kwa msingi huu basi, hakumuelei mlengwa kumdhuru vyo vyote utakavyo kuwa ujumbe aliompelekea. Hii ilikuwa na bado inaendelea kuwa ndio kanuni ya msingi katika mahusiano ya kidplomasia baina ya mataifa. Na kwa msingi huo ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliwapelekea ujumbe wafalme na viongozi walio mzunguka. Nao kwa kuuheshimu msingi huo huo, wakawapokea vema wajumbe walio tumwa kwao bila ya kuwadhuru au kuwadhalilisha. Isipokuwa mtu mmoja tu; Shurahbiyla Ibn Amrou Al-Ghasaaniy-mmojawapo wa magavana wa Urumi walio tawala Shamu.  Huyu hakui heshimu kanuni hii, akaivunja, yeye alikutana na Al-Harith Ibn Umeir mjumbe wa Mtume kwa gavana wa Basrah, akamuuliza anaelekea wapi. Alipo tambua kwamba yeye ni mmojawapo wa wajumbe wa Mtume, akaamuru afungwe na aletwe mbele yake, akamkata kichwa.

 

       ii.        Kuuawa kwa mjumbe wa Mtume aliye mtuma kwa mtawala wa Basrah ulikuwa ni uchokozi wa wazi na uadui wa moja kwa moja kwa Uislamu:

         Kuvunjwa kwa kanuni za Kidplomasia na kuuawa kwa mjumbe wake,  kulimkasirisha mno Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Na akalichukulia hilo kuwa ni uchokozi wa wazi na ni suala ambalo si vema kulinyamazia na kuliacha kupita hivi hivi tu. Khususan ikizingatiwa kwamba Uislamu bado ulikuwa ukiendelea kusimika nguzo zake katika Peninsula ya Kiarabu. Kwa hivyo bado kulikuwa na haja kubwa ya kuhifadhi na kulinda haiba yake na fikra iliyo kuwemo ndani ya nafsi za watu wakati huo ni kwamba Uislamu ni nguvu isiyo shindika. Na kwamba unapata msaada kutoka kwa Allah Taala na chini ya taathira ya itikadi hii walisilimu watu wengi kwa kupenda au kwa khofu, khusasan mabedui. Wengi wao walikuwa wakisilimu chini ya nyenzo ya khofu ya nguvu ya Uislamu au chini ya msukumo wa tamaa ya kupata ngawira. Na wala kuingia kwao Uislamuni hakukutokana na kusadiki na kuamini itikadi ifaayo na adabu tukufu zilizomo ndani ya Uislamu. Hakika si vinginevyo, kusilimu kwao kulikuwa ni kwa mtu mwenye pupa ambaye anavizia fursa na kuangalia mazingira. Na wakawa kama anavyo sema Allah Taala: "MABEDUI WAMESEMA: TUMEAMINI. SEMA: HAMJAAMINI, LAKINI SEMENI: TUMESILIMU. KWANI IMANI HAIJAINGIA KATIKA NYOYO ZENU..." [49:14] Na kama asemavyo: "NA KATIKA MABEDUI HAO WAKO WANAO FIKIRI KUWA WANAYO YATOA NI GHARAMA YA BURE, NA WANAKUNGOJEENI MAMBO YAKUGEUKIENI. MAGEUKO MAOVU YATAKUWA JUU YAO! NA ALLAH NI MWENYE KUSIKIA MWENYE KUJUA". [9:98]

Kwa ajili hii, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akawa na pupa mno ya kuhakikisha kuwa haiba ya Uislamu haipungui upande wo wote. Ili hilo lisipelekee kuteteresha itikadi iliyomo mioyoni mwa watu kuuelekea Uislamu kwa hali yo yote. Na kuyanyamazia mauaji ya    Al-Haarith Ibn Umeir lilikuwa ni jambo linalo pomosha utukufu/heshima ya Uislamu na kupunguza haiba yake. Kwa hivyo basi, ikawa hapana budi kufanya kitendo ambacho kitailinda haiba ya Uislamu. Na kuwahisisha watu ndani ya Peninsula ya Kiarabu na nje yake kwamba Uislamu sio nguvu ya kuchezewa na kudharauliwa. Ni kutokana na kuyazingatia yote haya kwa kina, ndipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipofikia uamuzi wa kutuma kikosi cha askari huko Shamu. Mahala ambapo aliuliwa kwa dhulma mjumbe wake; Al-Haarith Ibn Umeir ili kuwatia adabu wachokozi wale. Na kuuondoshea Uislamu jeuri na udhalili ulio fanyiwa.

 

     iii.        Uandazi wa jeshi na upangaji wa mikakati:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akapiga mbiu, watu wakatoka mbio mbio kuitika wito wake. Wakaja wakapiga kambi mahala paitwapo "Al-Jurfu" mpaka idadi yao ikafikia watu alfu tatu. Mtume alipo kwisha waandaa na kuwaweka tayari kwa vita, akawaambia: "Amiri-Jeshi wenu ni Zayd Ibn Haarith, akiuawa atashika uamiri Ja'afar Ibn Abu Twaalib, nae akiuawa atashika Abdullah Ibn Rawaahah. Huyu nae akiuawa, basi waislamu waridhiane baina yao mtu watakayempa uamiri". Na akawaamuru waende mahala alipouliwa Al-Haarith Ibn Umeir, wawalinganie Uislamu watu wa huko, wakiitika wawakubalie na wawachie. Na kama hawakuitika, basi takeni msaada kwa Allah juu yao na piganeni nao na akawausia kutofanya usaliti wala wasimuue mtoto wala mwanamke. Wala wasimuue mzee kikongwe, wala mtu aliye jihifadhi katika nyumba yake ya ibada, wala wasikate mti  wala kubomoa nyumba.

 



 | Tuandikie |