|
Jeshi la waislamu
likatoka likiwa na zawadi ya wasia wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie. Likisindikizwa na kila aina ya dua za waislamu, Bwana Mtume
akalisindikiza mpaka katika jangwa la Wadaa, hapo akaagana nalo na kurejea
Madinah. Na mkakati ulio kuwa umepangwa na jeshi ni kumshambulia adui kwa
kumshtukiza kabla hajajiandaa. Lakini khabari za kutoka kwa jeshi hili
zikavuja na kumfikia adui, akaanza kujiandaa. Maandalizi yao yakawa ya kutisha
kwa idadi ya askari na zana za vita kwa kiwango kinacho tunduwaza na
kuduwaisha. Kiwango kinacho onyesha nguvu, utajiri, fahkri na mamlaka kiasi
cha kuwastaajabisha waislamu.
Amepokea Al-Waaqidiy-Allah amrehemu-kwa isnadi ya Abu Hurayrah-Allah amuwiye
radhi-amesema: Nilihudhuria Mu'utah, mushrikina walipo tukaribia tuliona
maandalizi ya silaha na watu yasiyo weza kukabiliwa na ye yote. Macho
yakakodoka, Thabit Ibn Arqam akaniambia: Ewe Abu Hurayrah, kama wewe unaona
makusanyo kathiri. Nikamjibu: Naam, akasema: Hakika wewe hukuhudhuria (vita
vya) Badri pamoja nasi, kwa yakini sisi hatunusuriwi (kwa sababu ya) wingi (wa
watu/zana)!
Riwaya zinakurubia kujumuika kwamba Warumi waliwapokea waislamu kwa askari
laki mbili; laki moja ikiundwa na Warumi wenyewe na nyingine ikiundwa na
manasara wa Kiarabu. Waislamu kupokewa na idadi hii ya kutisha, hakika
inahisisha kwamba Warumi walifadhaika mno pale walipo tambua kwamba waislamu
wamewatokea. Na kwamba walikuwa wakijaribu kuufikiria upeo wa nguvu ya
waislamu isiyo ya kawaida. Nguvu iliyo eneza khofu pande zote za Peninsula ya
Kiarabu, nguvu ambayo majeshi shirika yameshindwa mbele yake. Nguvu ambayo
ngome madhubuti za Mayahudi pamoja na nguvu yao kubwa, havikuweza kuthibiti
mbele yake. Nguvu ambayo ilimpa Muhammad ujasiri wa kumlingania Uislamu
Hiraqli pamoja na mamlaka na nguvu zake alizo kuwa nazo. Naam, hapana budi
kwamba wao walianza kuusawirisha upeo wa nguvu hii na kuiona kuwa ni kitu
kisicho wezwa. Ndipo walipo anza kuiandalia nguvu zote waziwezazo na kama huu
si ukweli, basi je ni jambo la kawaida watu laki mbili kujikusanya kwa ajili
ya kupigana na watu alfu tatu?!
SOMO LA PILI.
i.
Ibn Rawaahah awashajiisha
waislamu kupambana na warumi:
Waislamu hawakuwa wakiifikiria nguvu na maandalizi ya
adui yao, walipo fika "Maan"; hii ni ngome kubwa katika nchi ya Palestina
umbali wa mwendo wa siku tano kwa ngamia kutokea Damascus (Syria). Hapo ndipo
walipojua maandalizi ya idadi na zana yanayo wangojea, wakapiga kambi hapo
siku mbili wakishauriana juu ya suala hili. Kisha wakapata wazo la kumuandikia
barua Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wamueleze hali halisi waliyo
ikuta huko. Ili ama awaongezee nguvu au awape shauri la kufanya walitekeleze,
lakini Abdullah Ibn Rawaahah akazidiwa na mori wa imani, akainuka
akiwashajiisha wenzake akiwaambia: "Enyi kaumu yangu! Hakika kile mnacho
kichukia, kwa yakini ni kufa shahidi ambako mmetoka mkikutafuta. Wallah sisi
hatukuwa tukipigana na watu kwa wingi wa idadi wala silaha wala wingi wa
farasi. Hatupigani nao ila ni kwa sababu ya dini hii ambayo Allah ametutukuza
kwayo. Enendeni, wallah mmeona siku ya (vita vya) Badri hatukuwa ila na farasi
wawili na siku ya Uhud hatukuwa ila na farasi mmoja tu! Enendeni, hakika si
vinginevyo, hilo ni mojawapo ya mazuri mawili; ama kuwashinda na hilo ndilo
alilo tuahidi Allah na Mtume wake na miadi ya Allah haina kukhalifiwa. Au kufa
shahidi, basi tukutane na ndugu zetu (katika imani) tuambatane nao peponi".
Maneno haya ya Ibn Rawaahah yakatenda ndani ya nafsi za watu
kile kitendwacho na uchawi, wakasonga mbele kukutana na adui wakiwa hawajali
cho chote. Wakaenda mpaka wakafika baada ya mwendo wa siku mbili "Al-Balqaa"
katika nchi ya Shamu. Hapo wakayakuta makundi makubwa ya adui yakiwa
yamejikusanya katika kijiji kinacho itwa "Mashaarif". Vikosi vya adui vikaanza
kuwajongelea, waislamu wakajikusanya katika kijiji cha Mu'utah ili wapate
ngome hapo. Lakini Warumi wakawashukia mithili ya mumbwi wa maji, wakasonga
mbele na farasi wao katika mandhari inayo kodosha macho na kudumaza akili.
Waislamu wakaikabili hali hiyo ya kutisha kwa kuzikusanya pamoja nguvu zao na
wakapigana katika utaratibu wa "shinikizo mkusanyiko kwa katikati". Wakaweka
pande zote mbili nguvu inayo zuia kuzungukwa na adui, upande wa kulia akawepo
Qutwbah Ibn Qataadah na ule wa kushoto alikuwepo Ubaadah Ibn Maalik. Majeshi
haya mawili yakapambana katika mpambano mkali kabisa kuwahi kutokea katika
historia ya mapambano ya waislamu dhidi ya makafiri.
ii.
Mpambano ulikuwa ni mkali
mno:
Zayd Ibn Haarithah akaongoza mapambano chini ya
bendera ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Waislamu nao wakapigana
pamoja nae wakiwa wamekamatana barabara katika safu zao mpaka damu ya Zayd
ikachuruzika mithili ya maji na viungo vyake vikatapanyika. Zayd alipouawa,
bendera ya waislamu ikashikwa na Ja'afar Ibn Abu Twaalib kama alivyo agiza
Mtume wa Allah. Akaongoza mapambano ya kufa na kupona chini ya bendera hiyo,
hata mpambano ulipo mmaliza nguvu kabisa na akazungukwa na adui. Alimrukia
farasi wake na kumchinja kwa upanga wake, kisha akajitosa katikati ya maadui
akipigana nao akienda kwa miguu na bendera akishika kwa mkono wake wa kulia.
Ukapigwa upanga mkono wake wa kulia ukakatwa, akaishika bendera kwa mkono wake
wa kushoto, nao pia ukakatwa. Akaikumbatia bendera kwa vifupa panya vyake
mpaka akauwa, mwili wake ukakutwa na michomo ya mikuki kiasi cha tisini. Baada
ya kuuawa Ja'afar, bendera ikatwaliwa na Abdullah Ibn Rawaahah. Kinacho
dhihirika hapa ni kwamba mpambano katika vita hivi ulikuwa ni mkali mno kiasi
cha kuwafanya waislamu kujisahau, wasikumbuke hata kula na kunywa. Ibn
Is-haaq-Allah amrehemu-amepokea riwaya kwamba Abdullah Ibn Rawaahah alipo
shuka mpambanoni, binamu yake alimletea mfupa wa nyama, akamwambia: "Hebu utie
nguvu uti wa mgongo wako kwa kula mfupa huu, kwani hakika wewe umekutana na
hali nzito katika siku zako hizi". Akautwaa mfupa ule na kung'ata pande,
halafu akasikia mzongo upande wa mahasimu wao, akasema: "Na wewe uko duniani?,
akautupa mfupa ule, akautwaa upanga wake akasonga mbele akipigana mpaka
akauawa.
|