|
iii.
Hila/mbinu ya kamanda
Khalid yaliokoa jeshi la waislamu:
Baada ya kuuawa
kwa kamanda Ibn Rawaahah, waislamu wakawafikiana kumteua Khalid Ibn Al-Waleed
kuwa kamanda wao mpya atakaye waongoza katika mapambano yao dhidi ya jeshi
kubwa la Warumi. Alipoitwaa bendera ya vita, akaongoza mapambano ya kumrudisha
nyuma adui na kumzungusha mpaka giza likaingia na kila kundi kurudi kambini
kwake kujiandaa na mpambano wa siku ifuatayo. Ni chini ya pazia la usiku huu,
ndipo kamanda huyu shujaa alipo ibuka na mbinu ya kubadilisha mpango mzima wa
jeshi katika medani ya vita. Kikosi kilicho kuwa kikipigana upande wa kulia
akakipeleka kushoto na kile cha kushoto akakihamishia kulia. Cha mbele
akakihamishia nyuma na kile cha nyuma akakileta mbele na akaandaa kundi
maalumu nyuma ya jeshi kutimua vumbi na kupiga makelele wakati wa maawio.
Majeshi mawili haya yalipo kutana asubuhi, kila kikosi cha adui kikaziona
nyuso ngeni tofauti na zile ilizo ziona jana yake na wakaona bendera nyingine
sio zile walizo ziona. Hili likawadhanishia kwamba waislamu wamepata nguvu
mpya, wakaogopa kuingia mpambanoni, kwani bado walikuwa na fikra za mpambano
mkali wa jana yake. Ambapo waislamu walikuwa wachache lakini waliwapeleka
mchakamchaka na kuua idadi isiyo kidogo, haya leo tayari wameongezeka hali
itakuwaje?! Hila/mbinu hii ya kamanda mahiri Khalid-Allah amuwiye
radhi-ikafanikiwa kumukhadaa adui. Nae akaitumia vema khofu yao hiyo, akawa
anawazungusha askari wake na kurejea nyuma kwa umahiri makini. Mpaka Warumi
wakadhania kuwa hiyo ni mbinu ya kuwavutia jangwani ili wakawasagesage huko,
kwa hivyo hawakuwafuata. Khalid nae akaendeleza mapambano mepesi dhidi ya
makundi makubwa ya adui mpaka akafanikiwa kuliponyosha jeshi lake mikononi mwa
adui mwenye uchu wa kuangamiza. Kwa mbinu yake hii akawa amefanya kinacho
paswa kufanywa na kamanda mahiri mwenye uoni wa mbali katika hali/mazingira
kama hayo. Na bora ya kinacho fanywa katika hali kama ile ni kurejea nyuma kwa
amani, kitu ambacho pengine ni kigumu zaidi kuliko kupata ushindi. Hii ni kwa
sababu kupata ushindi ni jambo linalo wezekana kwa nyenzo ya wingi wa zana,
watu na kustahamili. Lakini kurudi nyuma kwa salama mbele ya adui mwenye zana
na watu si suala liwezwalo na kila mtu ila awe mtu huyo na ujuzi wa masuala ya
uongozi katika medani ya vita.
iv.
Mtume atangaza kuuawa kwa
maamiri jeshi na kuusifia ushujaa wa Khalid:
Hivi ndivyo Khalid alivyo weza kuliokoa jeshi lake
dhidi ya hilaki dhahiri na kurudi nalo bila ya kupoteza ila roho kumi na mbili
tu. Kabla jeshi halijakanyaga ardhi ya Mu’utah, Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akawatangazia maswahaba wake Madinah khabari za kuuawa kwa maamiri
jeshi wake. Alitoa tangazo hilo ilhali macho yake yakifurika machozi kwa
kuwahuzunikia. Imamu Bukhaariy-Allah amrehemu-amepokea kwa Isnadi ya Anas Ibn
Maalik-Allah amuwiye radhi-kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-aliwatangazia watu kuuawa kwa Zayd, Ja’afar na Ibn Rawaahah kabla ya
ujio wa khabari hiyo, akasema (mithili ya mtangazaji wa redio): “Bendera
imetwaliwa na Zayd, ameuawa, kisha akaichukua Ja’afar nae akauawa,
ikachukuliwa na Ibn Rawaahah nae akauawa – (na macho yake yakibubujika
machozi) – mpaka ukaichukua bendera upanga miongoni mwa panga za Allah, hadi
Allah akaleta ushindi juu yake”.
Khabari za tukio hili zilileta mshindo mkuu ndani ya nafsi za
waislamu mpaka watu wa Madinah wakubwa kwa wadogo wakatoka kwenda kulilaki
jeshi. Watoto wadogo nao hawakubakia nyuma, wakatoka wakikaza mwendo mpaka
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akiwaonea huruma kutokana na umbali
mrefu walio kimbia, akasema: “Watwaeni watoto, muwabebe na mimi mnipe mtoto
wa Ja’afar”. Mtume akamtwaa Abdullah Ibn Ja’afar akambeba mbele yake juu
ya mnyama wake mpaka wakakutana na jeshi mahala paitwapo “Al-Jurfu”. Watu
wakadhania kwamba jeshi limeshindwa, wakaanza kuwamwagia mchanga wa uso huku
wakisema: “Enyi watimua mabio nyie! Hivi mmekimbia katika njia ya Allah?!”,
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akiwaambia: “Wao si watimua mabio, lakini wao
ni wenye kuswaga, insha-Allah”.
SOMO LA TATU
i.
Msimamo wa Ibn Rawaahah:
Riwaya/mapokezi
yanatofautiana katika kutaja msimamo wa Ibn Rawaahah pale alipotwaa bendera ya
uongozi wa jeshi baada ya kuuawa kwa kamanda Ja’afar. Ibn Is-haaq-Allah
amrehemu-yeye amepokea kwamba zama Abdullah Ibn Rawaahah alipo itwaa bendera
alisonga nayo mbele akiwa juu ya farasi wake. Akawa anajitoma medanini na huku
anasita kidogo, kisha ndipo akajitoma mzima mzima, akapigana hata akauawa. Na
Al-Waaqidiy-Allah amrehemu-anasema: Ibn Rawaahah alipigana na adui kwa muda
kidogo kisha tim akatimua mbio. Akailaumu nafsi yake kwa nini amekimbia,
akashuka kutoka katika farasi wake akapigana na adui mpaka akauawa shahidi
kama mtangulizi wake. Na wala Imamu Al-Baihaqiy na Musa Ibn Uqbah-Allah
awarehemu-hawakutaja cho chote kuhusiana na msito huu kama walivyo nukuliwa na
Ibn Kathir-Allah amrehemu. Kadhalika Al-Muqriziy-Allah amrehemu-hakulitaja
hilo katika kitabu chake [IMTAAUL-ASMAAU], wala Ibn Sa’ad katika
[ATTWABAQATIL-KUBRAA].
Na Abdullah Ibn Rawaahah-Allah amuwiye radhi-kama anavyo sema
Ibn Is-haaq mwenyewe na Wanasira wengine, ndiye aliye washajiisha na
kuwahamasisha waislamu kupigana na Warumi pale waliposita kufanya hivyo. Nae
ndiye aliye tajwa na Ibn Is-haaq katika riwaya yake kwamba alikitema kipande
cha nyama kilicho kuwa kinywani mwake wakati alipoona vita vinauma. Na akaona
vibaya kubakia duniani hata kwa kipindi kidogo nae akiwa mbali na medani ya
vita. Hivi haiwi kuwa kuna mgongano kwa mtu mwenye ari na yakini kama hii
kuingia katika medani ya vita akiwa anasita na kukhofu?! Kisha haiwi ni
kukinzana yeye kuwashajiisha wenzake kupigana na Warumi, halafu yeye mwenyewe
akawa muoga?! Basi ni wapi alikuwa Ibn Rawaahah wakati vilipo anza vita baina
ya waislamu na Warumi?! Hivi yeye hakuwa akipigana katika vita hivyo kama
mmojawapo wa jeshi la waislamu?! Na je, kweli inaingia akilini kuwa shujaa
mstari wa mbele kama askari, halafu awe mwenye kusita na khofu akiwa
kamanda?!!!
|