|
ii.
Vita hivi vimewasajilia
waislamu darsa gani?
Riwaya zinakhitilafiana katika kueleza khatima ya
vita hivi: Je, vita hivi vilimalizika kwa waislamu kupata ushindi au
kushindwa? Ibn Sa’ad-Allah-amrehemu-amepokea riwaya kutoka kwa Abu
Aamir-Allah amuwiye radhi-ambaye alihudhuria kwa maana ya kushiriki vita
hivyo: “Kwamba waislamu walisambaratishwa vibaya sana baada ya kuuawa kwa
(kamanda wao) Ibn Rawaahah na wakatapanyika kiasi cha kutoonekana wawili
wakiwa pamoja. Kisha akaitwaa bendera mmoja katika Maasnwaari akaisimika
mbele ya watu, akaanza kuwapigia ukelele nao wakikusanyika. Hata walipo kuwa
wengi akaenda na bendera mpaka kwa Khalid Ibn Al-Waleed akamkabidhi. Khalid
alipo itwaa bendera aliwaendesha mbio watu wale (Warumi) vibaya mno kiasi
cha kufikia waislamu kuziweka (kuwapiga) panga zao watakapo”.
Na al-Waaqidiy-Allah amrehemu-amepokea kutoka kwa
Al-Utwaaf Ibn Khalid-Allah amuwiye radhi: “Kwamba alipo uawa Ibn Rawaahah
jioni, alilala Khalid Ibn Al-Waleed, kulipo pambazuka alidamka akiwa tayari
amekipeleka mbele kikosi cha nyuma na kukirudisha nyuma kile cha mbele. Cha
kulia akakipeleka kushoto na kile cha kushoto akakileta kulia, hapo ndipo
makafiri walipo sema: Bila ya shaka umewajia msaada (nguvu mpya zaidi),
wakaogofywa wakatapanyika hali ya kushindwa. (Waislamu) wakaua miongoni mwao
idadi kubwa ambayo watu wale hawakupata kuua kwa waislamu”.
Na Musa Ibn Aqabah-Allah amrehemu-yeye anasema: “Waislamu
waliridhiana baada ya (kuuawa kwa) maamiri jeshi (walioteuliwa) na Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-kumteua Khalid Ibn Al-Waleed Al-Makhzuumiy
(kuwa amiri jeshi wao). Hapo Allah akamtimua adui na kuwapa ushindi
waislamu”.
Ibn Is-haaq-Allah amrehemu-anasema: “Thabit Ibn Aqram
alichukua bendera akasema: Enyi kusanyiko la waislamu ridhianeni juu ya mtu
miongoni mwenu (awe amiri wenu). Wakasema: Wewe (tumekuridhia), akasema:
Mimi siliwezi jukumu hilo. Ndipo watu walipo ridhiana kumteua Khalid Ibn
Al-Waleed, alipo itwaa bendera (ya uongozi) aliwarudisha nyuma watu wale
(Warumi), kisha wakatawanyika hata akaweza kuondoka na watu (maswahaba)”.
Ibn Kathir-Allah
amrehemu-amenukuu katika kitabu chake [AL-BIDAAYATU WAN-NIHAAYAH] maneno ya
Ibn Ishaaq, Al-Waaqidiy na Musa Ibn Uqbah, halafu akasema: “Kunamkinika
kujumuisha baina ya kauli ya Ibn Is-haaq na wengineo na mjumuisho huo ni
kwamba zama Khalid alipo itwaa bendera aliwanasua waislamu mpaka akawaokoa
kutoka mikononi mwa makafiri wale wa Kirumi. Kulipo pambazuka na
akabadilisha mpango wa jeshi (katika medani ya vita), kulia na kushoto,
mbele na nyuma-kama alivyo litaja hilo Al-Waaqidiy. Warumi wakadhania kwamba
hilo linatokana na nguvu mpya iliyo wajia waislamu, Khalid alipo warudisha
nyuma, wakawashinda kwa idhini ya Allah”...Ibn Kathir-Allah
amrehemu-akaitilia nguvu rai yake kwa kauli ya Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-iliyomo katika hadithi iliyo pokelewa na Imamu
Bukhaariy-Allah amrehemu-kutoka kwa Anas Ibn Maalik-Allah amuwiye radhi:
“Halafu ukaitwaa bendera upanga miongoni mwa panga za Allah, Allah akaleta
ushindi kupitia mikono yake”. Kama alivyo toa ushahidi kwa kauli iliyo tajwa
na Al-Waaqidiy na Musa Ibn Uqbah na alivyo taja Ibn Is-haaq ya kwamba
Qutwbah Ibn Qataadah – nae ndiye aliyekuwa kiongozi wa kikosi cha kulia cha
waislamu. Alimrudisha nyuma Ibn Rawaahah – nae ndiye (aliye kuwa) amiri –
jeshi wa (kundi la) Waarabu wa Kinaswara, akamuua.
iii.
Ushindi na ushindwa
katika medani ya vita hupimwa na malengo yaliyo fikiwa:
Ni mamoja kuwa
yaliyo tokea ni yale yalipokewa na Ibn Is-haaq au na wengineo, hakika si
hali ya kawaida watu alfu tatu kuwashinda watu laki mbili na kufanikiwa
kuchukua mateka. Au kuwaua hadi kuwafagia kabisa, inatosha tu kwamba wao
pamoja na uchache wao kuweza kusimama mbele ya idadi hii ya kutisha kwa siku
moja au zaidi katika mapambano makali kabisa. Kisha wakaweza kutoka ilhali
hawakuuawa miongoni mwao ila watu kumi na mbili tu. Lau kama waislamu
wangelitoka kwenye vita hivi bila ya kumuua adui hata mmoja, bado huo
ungekuwa ni ushindi kwao. Basi ni hali gani na kwa yakini imepokewa katika
baadhi ya riwaya kwamba wao waliua miongoni mwao (hao Warumi) idadi ambayo
wao (Warumi) hawakuua kwao (Waislamu)?! Na kwamba mushrikina walisambaratika
mbele yao kiasi cha waislamu kuwafyeka kwa panga watakavyo?!
Na huenda pakasemwa: Hakika maneno haya yametiwa chimvi.
Lakini sura zilizo onyeshwa na waislamu katika vita hivi dhidi ya Warumi,
zinaya thibitisha madai haya kwa kiwango kikubwa kabisa. Kwani waliuawa
mfululizo maamiri jeshi wote watatu (walio teuliwa na Mtume) katika siku ya
kwanza tu ya vita. Na hili lilitosha kuwapelekea waislamu kukimbia au
kusambaratika, kwani ada/desturi ya zama hizo ilikuwa ni jeshi kutimua mbio
pale anapo uawa amiri jeshi wao. Na huenda hili ndilo lililo mfanya adu
kuzielekeza hujuma zake kwa maamiri, lakini pamoja na yote hayo bado
waislamu hawakutimua mbio. Bali walithibiti na kuendelea kusimama kidete
mbele ya adui yao mpaka ukaingia usiku ambapo kila kundi lilirejea kambini
kwake kujiandaa na mpambano wa kesho. Na lilikuwa ni jambo mumkini kwa
waislamu kukimbia wakaenda zao salama chini ya pazia la usiku huu, lakini
katu hawakufanya hivyo. Bali walidamka mapema kwenda mpambanoni katika
namna/mtindo ulio waogofya na kuwatetemesha Warumi mpaka wakakosa kujiamini,
wakashindwa kuwashambulia waislamu. Hapo waislamu wakafurahi kwa kurudi kwao
nyuma, basi hii ni taswira miongoni mwa taswira jumla za vita zilizo
onyeshwa na waislamu katika vita hivi. Ama taswira binafsi, aliyo ionyesha
kila mtu miongoni mwao. Hii hapa iliyo onyeshwa na Ja’afar Ibn Abi
Twalib-Allah amuwiye radhi-pale alipo shuka kitatangeni akiwa juu ya farasi
wake akiwachoma panga adui. Mpambano ulipo muhemea akashuka juu ya farasi
wake, akamchinja kwa upanga wake, kisha akaanza kupigana akitembea na ilhali
kaishika bendera kwa mkono wake wa kulia. Ulipo katwa mkono huu wa kulia,
akaibeba bendera kwa mkono wa kushoto, nao ulipo katwa akaikumbatia kwa
vifupa panya vyake hadi akauawa.
Taswira nyingine pia inaonyeshwa na Khalid Ibn
Al-Waleed-Allah amuwiye radhi-pale aliposema kama ilivyo pokewa na Imamu
Bukhaariy-Allah amrehemu: “Ulipogongwa mkono wangu mapanga tisa siku ya vita
vya Mu’utah, basi haukubakia mkononi mwangu ila ubapa wa kulia”. Haya wewe
unaonaje, Khalid aliua watu wangapi hata akasibiwa na panga hizi zote?! Na
wenzake miongoni mwa mashujaa walio hifadhi Qur-ani waliua watu wangapi
katika kundi kubwa la adui?! Na tunainyaka kwa haraka sura nyingine miongoni
mwa sura za kusonga mbele na kuyavaa mauti bila ya kujali. Sura hii tunaiona
kupitia idadi hii ya chomo za panga zilizo elekezwa kwa Sayyidina
Ja’afar-Allah amuwiye radhi-mpaka ikasemwa kuwa ilikuwa michomo zaidi ya
tisini. Hakika ikiwa michomo hii inafahamisha kitu, basi inafahamisha juu ya
upeo wa muislamu katika kuifia dini yake na upeo wa kujitoma kwake ndani ya
safu za adui bila ya kujali wingi na nguvu ya adui huyo.
iv.
Vita vya Mu’utah
vilibakisha athari gani katika nafsi za Warumi?
Hakika sura
hizi na nyinginezo tunazo farijika nazo katika vita hivi, zinatujengea
taswira-jumla iliyo achwa na waislamu ndani ya nafsi za adui yao siku ya
Mu’utah. Kwa hivyo basi ni israfu ya maneno na sisi kutia chumvi
kuwakalifisha waislamu kutenda zaidi ya hayo waliyo yatenda. Na tunasema
kuwa kwa hayo waliyo yatenda, wao waliwashinda mushrikina katika vita hivi.
Na iwapo mambo huzingatiwa kutokana na natija (matokeo) zake na matendo
huzingatiwa kwa khatima yake. Ikiwa hivyo ndivyo, basi inatosha kuwa ni
ushindi kwa waislamu kwamba wao waliacha athari ya khofu ndani ya nafsi za
adui yao. Khofu iliyo wafanya kuacha mapambano na kuogopa kuwafuata pale
waislamu walipo kuwa wakirudi nyuma kwa umahiri mkubwa. Na kwamba athari hii
ilitosha kabisa kuipa amani mipaka ya dola ya Kiislamu kwa upande wa Shamu.
Si Warumi wala washirika wao miongoni mwa Waarabu walio jasiri kuwashambulia
waislamu baada ya vita hivi. Na athari hii iliendelea mpaka siku ya vita vya
“Tabuuk”, pale Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo waongoza
maswahaba wake kwenda kupambana na Warumi baada ya mwaka. Siku hiyo Warumi
hawakuweza kusimama na waislamu na badala yake wakakhiari amani kuliko
kupambana na hasimu huyu ambaye ameitoa nafsi yake katika kuilinda na
kuitetea dini yake. Adui asiye jali mauti wala kuogopa vita hata kama adui
ana nguvu kubwa zilizoje.
Vita
hivi si tu viliacha athari kwa Warumi na washirika wao peke yao, la hasha,
bali athari hii ilivuka mipaka na kupindukia katika nafsi za makabila.
Makabila yaliyo kuwa yakiishi nchani nchani mwa Shamu na Iraq, yalibakia na
athari kubwa ya kushangazwa na waislamu. Athari iliyo wapelekea wengi
miongoni mwa makabila ya Baniy Suleim, Ash-jaa, Ghatwfaan, Absi, Dhubyaan na
Fazaarah kuingia katika Uislamu kwa khiari zao wenyewe.
|