|
SOMO LA KWANZA.
i.
Makah ndio ilikuwa
kitovu cha vitongoji vyote vya Hijaazi na ngome kuu ya dini ya masanamu:
Hivyo ndivyo ilivyo kuwa Makah katika Peninsula
nzima ya Kiarabu na Al-Ka'abah ndio iliyo kuwa makao makuu ya
miungu-masanamu na welekeya wa macho ya watu wote. Na ndio iliyo kuwa dango
la matumaini ya makabila yote, yale ya karibu na yale ya mbali. Na
Makureishi ndio walio kuwa walinzi na waangalizi wa Al-Ka'abah na ndio walio
kuwa wameshikilia hatamu za uongozi wa kidini na kisiasa. Na daraja/hadhi ya
makabila mengine kwa Makureishi ilikuwa ni hadhi ya bwana na mtwana au
kiongozi na muongozwa. Kwa mtazamo huu, ndio makabila ya Kiarabu kwa tofauti
zao yalikuwa yakifuatilia kwa makini na karibu kabisa mpambano ulio kuwa
ukiendelea baina ya Muhammad na Makureishi. Na wakifuatilia harakati na
hatua zake mfuatilio – makini, na harakati na hatua zote hizi zilikuwa
zikiacha athari za wazi katika mielekeo ya makabila haya. Mielekeo kwa
upande wa ama kuukubali Uislamu au kuukataa na ama kuunga mkono au kuupinga.
Na pamoja na vita na matukio yaliyo duru baina ya waislamu
na Makureishi kwa upande mmoja, na baina ya waislamu na mayahudi kwa upande
wa pili. Na kwa upande mwingine baina ya waislamu na warumi na makabila ya
Kiarabu ya pande za Peninsula. Yalikuwa na athari katika kudhihiri na kuenea
kwa Uislamu miongoni mwa makabila mengi, hakika Makah kuendelea kubakia
katika ushirikina wake nayo ikiwa ndio kitovu cha vitongoji vyote na ngome
kuu ya dini – sanamu. Ilikuwa ni kizuizi na kikwazo dhidi ya kutawala kwa
Uislamu katika Peninsula nzima ya Kiarabu. Na ili Peninsula iufuate Uislamu
na makabila yauridhie kuwa dini na itikadi yao, ilikuwa hapana budi
Makureishi wauamini kwanza Uislamu na ukumbatiwe na Makah iliyo kitovu cha
vitongoji.
ii.
Suluhu ya Hudaybiyah
ilikuwa ndio mwanzo wa kuanguka kwa ngome hii kongwe:
Suluhu (mkataba) ya Hudaybiyah baina ya Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-na Makureishi mnamo mwaka wa sita Hijiria,
ilikuwa ndio ufunguo wa kwanza wa ngome hii kongwe. Katika suluhu hiyo,
Makureishi walikiri kwamba Muhammad ni kiongozi wa itikadi mpya na kwamba
hapana ubaya kuandikiana nae mkataba utakao zihakikishia amani pande mbili
hizi hasimu. Wakalazimika kufikia azimio/uamuzi huo baada ya jitihada zao za
kuutokomeza Uislamu kugonga mwamba. Makureishi walibakia kwa takriban miongo
miwili wakiwa hawamtambui mtume, wala dini hii anayo itangaza ambayo
inaikhalifu dini na itikadi yao. Wakashikilia utukufu na ukubwa wao huku
wakimzulia mtume uongo mbali mbali na kumvika sifa mbaya mbaya kwa lengo la
kumchafulia jina lake na kuubomoa mlingano wake miongoni mwa Waarabu. Zama
walipo shindwa kwa njia na mbinu zao zote kuutokomeza Uislamu na kumuua
kiongozi wake, ndipo walipo lazimika kuamiliana nae muamala wa mpinzani kwa
mpinzani. Na kufanya suluhu japo kwa muda mchache ili kujikinga na hatari
yake na kupata amani upande wake. Na suluhu hii ikawa ndio ufunguo wa mwanzo
ambao Allah aliutumia kufungulia milango na makomeo ya Makah.
iii.
Umrah ya Qadhaa ikawa
ndio ufunguo wa pili wa ngome hii:
Baada ya mwaka huo, Umrah ya Qadhaa ikawa ndio
ufunguo wa pili wa ngome hii. Kwani mdhihiriko wa waislamu katika Umrah hii
nao wakiwa katika hali ya kupendana na kuhurumiana kwao, kuzoeana na
kushikamana kwao. Nidhamu yao ya hali ya juu kabisa katika kumtii kiongozi
na mapenzi ya kweli na ikhlasi yao kwa Mtume wao. Na hamasa yao kubwa
kuielekea dini yao na kushikamana kwao kidhati na adabu zake, na
kuitakafutiza kwao upeo nyumba tukufu ya Allah na kuyaadhimisha matukufu
yake. na yote waliyo kuwa wakiyatekeleza katika Umrah hii, wakiwa ndani ya
hamasa hii, mshikamno huu, nidhamu hii na kujiweka kwao mbali na kila linalo
tia dosari tabia za mtu. Mdhihiriko wa waislamu katika yote haya,
ulidhihirisha na kutusha mtikisiko adhimu ndani ya nafsi za watu wa Makah.
Na ukagusa tao la imani ndani ya nyoyo zao na kulitikisa mtikisiko mkubwa,
basi wakawa wanawaangalia waislamu mtazamo wa kushangazwa nao na ukubwa. Na
wakauangalia Uislamu mtazamo wa tafakari – mazingatio na wakawa wanajaribu
kufanya mlinganyo baina ya dini hii mpya na itikadi waliyo nayo wao. Na
baina ya mapokeo yasiyo kubaliwa na akili na yasiyo thibitishwa na mantiki
na wakiweka katika mizani matukufu haya yatekelezwayo na waislamu kwa
unyenyekevu mkubwa na moyo mmoja na puo na mchezo waufanyao wao katika ibada
zao, kama tunavyo soma: "NA HAIKUWA IBADA YAO KWENYE HIYO NYUMBA
(Al-Ka'abah) ILA KUPIGA MIUNZI NA MAKOFI..." [8:35]
Naam, wakaanza kuchunguza na kutafakari na wakagundua
tofauti kubwa na ya mbali baina ya itikadi yao na ile itangazwayo na
Muhammad. Hapo nyoyo zao zikaulainikia Uislamu na vifua vyao kuusikiliza,
kwa ajili hii wakasilimu miongoni mwao walio weza kuudhihirisha Uislamu wao.
Na wakausirisha Uislamu wale wasio weza kuutangaza kwa sababu ya unyonge
wao. Na wengi miongoni mwao wakajiandaa kwa nyoyo na nafsi zao kusilimu, lau
kama si pingamizi – mazingira na manufaa ya muda yaliyo wazuia kwa kitambo
tu. Mtikisiko huu ulio ipata itikadi ya watu wa Makah katika Umrah ya
Qadhaa, ukawa ni ufunguo mwingine ambao Allah aliutumia kufungulia makomeo
ya Makah.
iv.
Hatimaye Makureishi
wauvunja mkataba wa amani wa Hudaybiyah;
Kisha baada ya hapo, Allah Taala akataka kufungua
makomeo yote yaliyo bakia ya ngome hii, yakatokea yaliyo tokea katika mwaka
wa nane; yaani Makureishi kuvunja mkataba ule wa Hudaybiyah. Ilivyo kuwa ni
kwamba yalikuwepo machafuko ya umwagaji wa damu baina ya kabila la Bakri na
Khuzaah katika zama za Jahilia. Ilipo fikiwa suluhu ya Hudaybiyah na kabila
la Khuzaah likaingia katika ushirika na Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie. Na lile la Bakri likawa mshirika wa Makureishi, vita vikasita
baina ya makabila mawili haya na kila moja likapata amani upande wa adui
yake. Kisha ikatokezea kwamba siku moja mtu mmoja wa kabila la Bakri
kusimama na kuanza kumfanyia istihizai na kebehi Mtume wa Allah mbele ya
usikivu wa mtu wa kabila la Khuzaah; washirika wa Mtume. Yule Mkhuzaai
akashindwa kustahamili, akainuka na kumpiga mchokozi yule, kitendo hicho
kikauamsha na kuuchochea uadui wa tangu ulio kuwepo baina ya makabila mawili
hayo. Kabila la Bakri ambalo mtu wao kapigwa, likaanza kujiandaa kulipa
kisasi kwa kabila la Khuzaah na wakasadiwa juu ya hili na watu katika
Makureishi. Usiku mmoja watu kadhaa wa kabila la Khuzaah walikuwa katika
eneo lao lenye maji likiitwa "Al-Watiyr", wakavamiwa na watu wa kabila la
Bakri na washirika wao Makureishi. Khuzaah kuona hivyo, wakakimbilia katika
"haram" – eneo takatifu la Al-Ka'abah ili kupata hifadhi hapo, lakini hilo
halikuwazuia Wabakri kuwafuata, wakawashambulia na kuua miongoni mwao kiasi
cha watu ishirini. Hapo ndipo Wakhuzaah walipo muomba msaada Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakatuma ujumbe wa watu Madinah.
Wakamkhabarisha Bwana Mtume khiana waliyo fanyiwa na Wabakri na namna
walivyo saidiwa na Makureishi. Mtume akamwambia kiongozi wao baada ya
kuwasilisha malalamiko yao kwa njia ya ushairi: "Umenusuriwa ewe Amrou Ibn
Salim". Kwa hili Mtume akaona ndio fursa muafaka ya kuifungua Makah, akaanza
kujiandaa kwa ajili ya ufunguzi huu.
|