|
Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akakadiria kwamba Makureishi watadiriki
ubaya wa kitendo walicho kitenda. Na kwamba hapana budi watamtumia ujumbe
ili kutengeneza hali/uhusiano ulio haribiwa na khiana yao, ndipo Mtume
akawaambia maswahaba wake: "Kama kwamba Abu Sufyaan amekujilieni ili kuutia
nguvu mkataba na kuongeza muda". Yote aliyo yakadiria na kuyatazamia Mtume,
yakatokea kama alivyofikiria, kwani Makureishi walihisi mwisho mbaya utakao
ifuatia khiana yao. Wakamtuma Madinah kiongozi wao Abu Sufyaan Ibn Harb ili
pengine yeye anaweza kuyadiriki na kuyasahihisha matokeo ya kosa hili baya.
Na Abu Sufyaan alikuwa anauhisi uzito wa suala hili analo liendea, kwa hivyo
hakupendelea kwenda moja kwa moja kuonana na Mtume, mpaka kwanza aandae njia
na mazingira ya kukutana nae. Akaanzia kwa binti yake Ummu Habibah; mke wa
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ili apate kumuombea kwa Mtume.
Alipo taka kukalia tandiko la Mtume, Ummu Habibah akalikunja, Abu Sufyaan
akastaajabishwa na kitendo hiki alicho fanyiwa na binti yake mwenyewe.
Akamuuliza: "Ewe kijibinti changu wee! Umechukizwa mimi kulikalia tandiko
hili?", binti akamjibu wazi usoni akisema: "Lakini hilo ni tandiko la Mtume
wa Allah na wewe mtu mshirikina ni najisi, kwa ajili hiyo sikupenda ulikalie
tandiko la Mtume wa Allah". Jawabu hilo likawa ni pigo lenye mshindo mkuu
moyoni mwa Abu Sufyaan ambalo hakulitazamia tena kutoka kwa mtu wake wa
karibu mno kama binti yake. Akajikuta hawezi kujimudu, akamwambia binti yake
akimueleza fedheha na udhalili ulio mpata: "Wallah ewe binti yangu imekupata
shari baada yangu".
Kisha huyoo akatoka nyumbani kwa Mtume akiwa mvunjifu wa
moyo na majeruhi wa kifua, mpaka akaingia msikitini aliko kuwepo Mtume wa
Allah. Akamsemeza, Mtume hakumjibu kitu, kutojibiwa na Mtume lilikuwa ni
pigo kubwa zaidi kuliko lile la kwanza alilo lipata kwa binti yake. Akatoka
msikitini akiwa mnyonge mno na mwenye uso wa kukata tamaa, akaenda kutaka
msaada na uombezi kutoka kwa maswahaba wa Mtume. Basi hakupata hata mtu
mmoja aliye tayari kuipokea haja yake na kuiwasilisha kwa Mtume. Alimuendea
Sayyidina Abu Bakri-Allah amuwiye radhi-yeye akamtaka udhuru wa kutoliweza
hilo kwa lugha ya upole. Akatoka, huyoo mpaka kwa Sayyidina Umar-Allah
amuwiye radhi-huko akakaripiwa na kutolewa maneno makali, akaambiwa: "Mimi
ndio nikuombeeni nyinyi kwa Mtume wa Allah, mimi?! Wallah, lau nisingelipata
ila chembe ndogo tu basi ningepigana nanyi kwayo". Baada ya kugonga mwamba
kwa Umar akamuendea Sayyidina Aliy Ibn Abiy Twaalib-Allah amuwiye
radhi-akamwambia: "Ewe Aliy, hakika wewe ndiye mtu mwenye udugu wa karibu
zaidi nami na kwa yakini nimeletwa na haja fulani. Basi nisirejee patupu
kama nilivyo kuja, basi nakuomba uniombee". Aliy akamwambia: "Ole wako ewe
Abu Sufyaan! Wallah, Mtume wa Allah amekwisha azimia jambo, ambalo sisi
hatuwezi kumzungumza katika hilo". Na yasemekana kwamba Abu Sufayaan
alikwenda pia kwa Sayyidina Uthman Ibn Affaan, Sa'ad Ibn Ubaadah na wengineo
miongoni mwa maswahaba wakubwa katika Muhajrina na Answaari, na kila mmoja
wao akimwambia: "Dhima/amani yangu iko katika dhima ya Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-na wala hapana ye yote achukuaye dhima juu yake". Alipo
kata tamaa kupata alilo litaka kwa wote hawa, ndipo alipofikia uamuzi wa
kwenda kwa Bi. Fatimah; binti ya Mtume. Nae akiwa na mwanawe; Al-Hassan
akiwa anatambaa tambaa mbele yake, akamwambia: "Ewe binti Muhammad! Je,
kunakuelea kuchukua dhima baina ya watu hawa?", akamjibu: "Hakika si lo
lote, mimi ni mwanamke", Abu Sufyaan akamwambia: "Muamrishe mwanao huyu
achukue dhima baina ya watu, nae atakuwa bwana wa Waarabu hadi mwisho wa
ulimwengu". Bi. Faatimah akamwambia: "Wallah mwanangu huyu bado hajafikilia
kuchukua dhima baina ya watu, na hapana ye yote awezaye kuchukua dhima juu
ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie".
Baada ya jitihada zake hizo kushindwa, ndipo alipo rejea kwa
Sayyidina Aliy, akamwambia: "Ewe babie Hassan, hakika mimi nayaona mambo
yananiwia ugumu sana, hebu basi nipe nasaha zako". Aliy akamwambai: "Wallah
sijui cho chote kitakacho kusaidia, lakini jambo moja wewe ni bwana wa
Kinaanah. Basi cha kufanya, wewe inuka uchukue dhima mwenyewe baina ya watu,
kisha ushike njia uondoke kwenu". Abu Sufyaana akauliza: "Hivi wewe unaona
hilo litanisaidia cho chote?", Aliy akamjibu: "Wallah, hapana sidhanii
hivyo, lakini mimi sina ushauri mwingine zaidi ya huo". Abu Sufyaan akainuka
msikitini mle akasema: "Enyi watu nyie! Hakika mimi nimechukua dhima baina
ya watu". Halafu akampanda ngamia wake, huyoo akaondoka kurejea Makah, huku
akimeza machungu ya kurejea patupu na unyonge. Alipo fika kwa Makureishi
wakamuuliza: "Kuna nini huko utokako?", akajibu: "Nimemuendea Muhammad
nikamsemsha, basi wallah hakunijibu cho chote! Kisha nikamuendea Ibn Abu
Quhaafah (Abu Bakri) na kwake sikupata kheri yo yote. Halafu tena
nikamuendea Ibn Al-Khatwaab, huyo nikamkuta adui mkubwa kuliko wote. Kisha
nikamuendea Aliy, huyu akawa laini kuliko wote na akaniashiria jambo nililo
lifanya. Basi wallah sijui litasaidia cho chote au la". Wakamuuliza: "Haya
ni jambo gani hilo? Akajibu: "Aliniamuru kuchukua dhima baina ya watu, nami
nikafanya hivyo". Wakauliza: "Je, Muhammad amelipitisha hilo? Akajibu:
"Hapana", wakamwambia: "Ole wako! Wallah mtu huyo hakuzidi ila kukuchezea
tu".
|