Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SOMO LA PILI

 Faida

            i.          Mtume wa Allah ajiandaa kwa Fat-hi Makkah na achukua hatua za makusudi kuepusha umwagikaji wa damu:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaanza kujiandaa na Fat-hi Makah, akawatumia ujumbe watu wa vitongojini na mabedui walio mzunguka, waje Madinah katika mwezi wa Ramadhani. Makabila yakauutika wito huo wa Mtume na yakaanza kumiminika Madinah na kupiga kambi hapo. Mtume wa Allah akawa makini mno, akawaficha watu makusudio yake, wasijue anaelekea wapi, hilo lilikuwa ni sehemu ya hatua za makusudi kuepusha umwagikaji wa damu. Akaweka walinzi katika njia zote ziingiazo na kutoka Madinah, wamrejeshe atokako kila wanaye mtilia mashaka. Watu walipo kwisha kusanyika, ndipo alipo wafahamisha kwamba anakusudia kwenda Makah na akawaamuru kujiandaa vema na haraka kwa ajili ya safari hiyo. Na akamuomba Allah ajaalie Makureishi wasijue lo lote katika kutoka kwake huku, ikawapelekea wao kujiandaa na vita na hivyo kusababisha umwagikaji wa damu. Aende bila wao kujua wala kuhisi lo lote ili awashtukize, kitendo kitakacho wafanya wasalimu amri.

 

         ii.          Kosa la Haatwib Ibn Abiy Bal-ta’ah:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo kata shauri kwenda kwa Makureishi na akawatangazia watu welekeya wake huo. Haatwib Ibn Abiy Bal-ta’ah akawaandikia barua Makureishi, akiwaeleza juu ya azma hii ya Mtume wa Allah. Akamkodi mwanamke mmoja kutoka katika kabila la Muzaynah, akampa barua ile na akamuamuru afanye kila hila na kila aliwezalo kuifikisha barua hiyo Makah kwa Makureishi. Mwanamke yule akaitwaa barua na kuificha tayari kwa msafara wa Makah, huyoo akashika njia za panya (za uficho) hata akafanikiwa kutoka nje ya Madinah na akawa sasa anashika njia iendayo Makah. Hapo ndipo ikamjia Mtume-Rehema na Amani zimshukie-khabari kutoka mbinguni ikikielezea kitendo alicho kifanya Haatwib. Bila kuchelewa Mtume akamtuma Sayyidina Ali Ibn Abiy Twaalib na Zubeir Ibn     Al-Awwaam kumfuata mwanamke yule, nao wakamdiriki njiani kabla hajaingia Makah. Wakanyang’anya barua ile na kuiwasilisha mbele ya Mtume wa Allah, Mtume akamuita Haatwib na kumuonyesha barua yake ile, kisha akamuuliza: “Ni lipi lililo kupelekea hata ukaamua kufanya hivi?” Haatwib akadhania kwamba tayari amesha hiliki na wala hana njia ya kuihepea hilaki hiyo dhahiri. Kama kuna uokovu basi utatokana na yeye kumwambia ukweli Mtume wa Allah, akasema: “Ewe Mtume wa Allah wee! Tafadhali usinifanyie haraka, wallah mimi ninamuamini Allah na Mtume wake, bado sijabadilisha wala kuiharibu imani yangu hiyo. Lakini mimi nilikuwa ni mtu asiye na mtu wala jamaa kwa Makureishi na watoto na mke wangu wako huko, kwa hivyo nikataka kuonekana mzuri kwao. Na Muhajirina walio pamoja nawe ambao wana watoto na mali Makah, wao hawa wana ndugu watakao walinda watoto na mali zao. Kwa hivyo nikapendelea, kwa kuwa sina nasabu kwa Makureishi, niwe na mkono (wema) ambao kwa huo watawalinda watoto wangu. Na wala mimi sikulifanya hili kwa kuwa nimetoka katika dini yangu na wala si kwa kuuridhia ukafiri baada ya imani”.

 

       iii.          Mtume wa Allah alisawazisha kosa la Haatwib:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaona ukweli wa maneno ya Haatwib na nia yake njema iliyo mpelekea kufanya kosa hilo, akawaambia watu walio mzunguka: “Ama hakika yeye amekuelezeni kweli katika aliyo waambia”. Mtume wa Allah akarudi nyuma kimawazo na kuangalia namna mtu huyu alivyo kuwa katika jihadi huko nyuma na alivyo tumia upeo wa nguvu na ushujaa wake katika kuuhami Uislamu. Kwa kuyaangalia mazuri haya ya nyuma, Mtume akapondokea katika kumsamehe swahaba wake huyu juu ya kosa lake hili. Ama Sayyidina Umar-Allah amuwiye radhi-suala la khiana hii lilikuwa kubwa mno kwake khasa kutokana na kwamba mpika khiana mwenyewe ni mmoja kati yao. Akamuangalia Haatwib, akamwambia: “Allah akuangamize! Unamuona Mtume wa Allah anapita njia za panya (ili watu wasijue), halafu wewe unawaandikia Makureishi (kuwajulisha)? Ewe Mtume wa Allah, hebu niachie niikate shingo ya mnafiki huyu”. Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akatabasamu kutokana na hamasa za Umar na akasema: “Na lipi litakalo kujulisha ewe Umar, huenda Allah aliwacho mozea watu wa Badri (walio pigana vita hivi) akawaambia: Tendeni mlitakalo, kwa yakini mimi nimekwisha wasameheni”.

Kufuatia tukio hili, Allah Taala akashusha aya za mwanzo za Suratil-Mumtahinah akiwatahadharisha waislamu kumfanya adui yao rafiki. Au kumpa baadhi ya siri zao hata kama kuna sababu gani ipelekeayo hivyo, kwani adui ni adui tu vyo vyote atakavyo kuwa. Na kumfanya adui kuwa ndio kipenzi, hiyo ni khiana isiyo na kiasi, akasema Taala: “ENYI MLIO AMINI! MSIWAFANYE ADUI ZANGU NA ADUI ZENU KUWA MARAFIKI MKIWAPA MAPENZI, NA HALI WAO WAMEKWISHA IKATAA HAKI ILIYO KUJIENI, WAKAMFUKUZA MTUME NA NYINYI KWA SABABU MNAMUAMINI ALLAH, MOLA MLEZI WENU. MNAPO TOKA KWA AJILI YA JIHADI KATIKA NJIA YANGU NA KUTAFUTA RADHI YANGU, MNAFANYA URAFIKI NAO KWA SIRI, NA MIMI NAYAJUA MNAYO YAFICHA NA MNAYO DHIHIRISHA. NA MWENYE KUFANYA HAYO KATI YENU BASI AMEIPOTEA NJIA YA SAWA. WAKIKUWEZENI WANAKUWA MAADUI ZENU, MA WANAKUKUNJULIENI MIKONO YAO NA NDIMI ZAO KWA UOVU. NA WANAPENDA MUWE MAKAFIRI. HAWATAKUFAENI JAMAA ZENU, WALA WATOTO WENU SIKU YA KIYAMA, ALLAH ATAPAMBANUA BAINA YENU, NA ALLAH ANAONA MNAYO YATENDA”. [60:1-3]

 

       iv.          Jeshi la Fat-hi Makah:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akampa ukaimu wa Madinah, Abu Dharri Al-Ghifaariy-Allah amuwiye radhi. Akatoka Madinah akiwa na maswahaba wapatao alfu kumi, katika Muhajirina na Answaari na ujumbe wa makabilia ya Kiarabu ulio itikia wito wake. Likaondoka jeshi hili kubwa likilikata jangwa pana kuelekea Makah, si kwa lengo la kwenda kumwaga damu huko na kuwaua watu wasio na hatia, la hasha. Wala si kwa dhamira ya kupora mali na kukalia haki za watu kimabavu, lakini ilikuwa ni kwa ajili ya kufungua makufuli ya mji mtakatifu. Na kuuondoshea mji huu vizuizi na vipingamizi na kuufanya kama alivyo ufanya Allah: “NA KUMBUKENI TULIPO IFANYA ILE NYUMBA (ya Alkaaba) IWE PAHALA PA KUKUSANYIKIA WATU NA PAHALA PA AMANI...” [2:125] Na aineze hapo dini ya haki ambayo kwayo Allah amewaleta mitume wote ili wawatoe watu kutoka katika viza (shirki) kuwatia katika nuru (Uislamu).

 



 | Tuandikie |