Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

V. AL-ABBAS AFANYA JITIHADA ZA MAKUSUDI KUWAPA AMANI MAKUREISHI

 Faida

 

         v.        Al-Abbas afanya jitihada za makusudi kuwapa amani Makureishi:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo fika katikati ya safari yake, alikutana na Al-Abbas Ibn Abdil-Mutwalib akihajiri Makah kuja Madinah na familia yake. Kukutana huku kukawa ni sadfa yenye baraka, kwa kukutana huku Allah Taala alizihifadhi damu zisimwagike na akayawepesisha mambo. Na kwao, Allah akaisakhirisha njia ya Fat-hi Makah kwa namna aliyo kuwa akiitazamia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Kwani Al-Abbas alimtuma mtu kuipeleka Madinah familia yake na yeye akarejea Makah na jeshi la Mtume. Jeshi lilipo kuwa umbali wa mwendo wa siku moja tu kuingia Makah, Mtume na maswahaba wake wakapiga kambi na wakati huo ulikuwa ni usiku. Mtume wa Allah akaamrisha iwashwe mioto eneo lote kuzunguka kambi, wakawasha mienge alfu kumi ya moto. Mwangaza wake ukaanza kuzagaza katika giza la jangwani mpaka ukaufanya usiku ule mithili ya mchana kutokana na mwangaza wake. Hili likamuogofya mno Al-Abbas na akawachelea watu wa Makah kufikwa na matokeo ya mshtukizo huu khatari, na akakadiria mpambano wa Makureishi na jeshi hili kubwa. Na khasara ya mali na nafsi itakayo patikana kutokana na mpambano huo, kwa kuyakadiria yote haya akaanza kufikiria mbinu/njia itakayo wapatia amani Makureishi na kuwaokoa dhidi ya hilaki hii inayo karibia kuwashukia.

Al-Abbas mwenyewe anahadithia: “Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo piga kambi (Mar-radhwahraan), nafsi yangu iliwaonea sikitiko watu wa Makah na nikajiambia: Eeh asubuhi mbaya iliyoje kwa Makureishi! Wallah lau Mtume wa Allah ataingia Makah kwa nguvu kabla hawajamjia na kumtaka amani, hakika hapana shaka hiyo ni hilaki ya Makureishi mpaka mwisho wa dunia! (Anaendela kusimulia): Basi nikakaa juu ya nyumbu wa Mtume wa Allah, nikatoka nae mpaka sehemu iitwayo (Al-Araak), nikajiambia: Huenda nitawapata baadhi ya watafuta kuni au wauza maziwa au mtu mwenye haja anaye kwenda Makah. Ili awape khabari watu wake juu ya mahala alipo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wapate kuja kumtaka amani kabla hajaingia kwa nguvu. Na ikawa katika qadari na hukumu ya Allah ni kutokea kwa Abu Sufyaan Ibn Harbi, Hakim Ibn Huzaam na Budeil Ibn Warqaa wakiwa katika harakati za kupekua khabari. Wakitafuta kupata au kusikia khabari, basi wallah nami nikienda juu ya nyumbu wa Mtume wa Allah nikilitafuta nililo litokea. Mara tahamaki nikasikia mazungumzo ya Al-Abbas na Budeil nao wakijibizana, Abu Sufyaan akisema: “Sijapatapo katu kuona mioto wala kambi kama hii ya usiku wa leo!”, hapo Budeil akamwambia: “Wallah hao ni Khuzaah (kabila) wameunguzwa na moto wa vita (wamepandwa na mori wa vita)”. Abu Sufyaan akamjibu: “Khuzaah ni madhaifu na wachache mno hii kuweza kuwa kambi na mioto yao”.

(Al-Abbas anaendelea): Basi nikaitambua sauti yake, nikaita: “Ewe babie Handhwalah”, akaitambua sauti yangu akasema: “Babie   Al-Fadhli (wewe)!” Nikaitika: “Naam”, akauliza: “Una nini wewe, nakufidia baba na mama yangu (uniambiae)”, nikamwambia: “Ole wako ewe Abu Sufyaan! Huyo ni Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akiambatana na maswahaba wake. Wallah asubuhi mbaya iliyoje kwa Makureishi! Akauliza: “Basi itumiwe hila gani, nakufidia baba na mama yangu?” Nikajibu: Wallah iwapo atakushinda ataipiga shingo yako! Basi panda nyuma ya nyumbu huyu nikupeleke kwa Mtume wa Allah nikakuombee amani”. (Anasema Al-Abbas): Akapanda nyuma yangu na wale wenzake wakarejea, nikaja nae. Kila nilipo upitia moto miongoni mwa mioto iliyo washwa na waislamu, waliuliza: Nani huyo? Wanapo muona nyumbu wa Mtume wa Allah nami nikiwa nimempanda, husema: Huyo ni ami wa Mtume wa Allah amempanda nyumbu wake (Mtume). Mpaka nilipo upitia moto wa Umar Ibn Al-Khatwaab-Allah amuwiye radhi-akauliza: “Nani huyo?” na akaniinukia. Alipo muona Abu Sufyaan nyuma ya mnyama, akasema: “Abu Sufyaan adui wa Allah! Kila himda njema zinamstahikia Allah ambaye amekumakinisha kwetu bila ya mkataba wala ahadi”. Kisha huyoo akatoka wangu wangu kuelekea aliko Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-nami nikampeleka shoti nyumbu nikamtangulia kufika. Nikachupa kutoka juu ya nyumbu na nikaingia kwa Mtume nikifuatiwa na Umar, akasema: “Ewe Mtume wa Allah! Huyoo Abu Sufyaan, adui wa Allah, Allah amemmakinisha kwetu bila ya ahadi wala mkataba. Basi niachie niipige shingo yake nimuulie mbali”. Mimi nikasema: “Ewe Mtume wa Allah! Hakika mimi nimekwisha mpa hifadhi”. Halafu nikakaa kwa Mtume wa Allah nikamshika kichwa chake nikasema: “Wallah usiku wa leo (Abu Sufyaan) asizungumze na mtu ye yote ila mimi tu”.

Al-Abbas na Umar wakaendelea kujibizana mbele ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa suala la Abu Sufyaan, mpaka Mtume akasema: “Ewe Abbas nenda nae katika khema lako na uje nae kutakapo pambazuka”.

 



 | Tuandikie |