|
i.
Abu Sufyaan asilimu:
(Anasema Sayyidina Al-Abbas-Allah amuwiye radhi): Nikaenda
nae khemani kwangu, akalala kwangu. Kulipo pambazuka nikadamkia nae kwa
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Mtume alipo muona akasema: “Ole
wako ewe Abu Sufyaan! Hivi bado haujafika wakati wewe kujua kwamba hapana
Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Allah?” Akajibu (Abu Sufyaan): “Nakuapia
kwa baba na mama yangu. Wallah kwa yakini nimeyakinisha lau kungekuwa na
mungu mwingine pamoja na Allah, basi hakika angelinitosheleza kwa cho
chote”. Mtume akasema: “Ole wako ewe Abu Sufyaan! Hivi bado tu haujafika
wakati wewe kutambua kwamba mimi ni Mtume wa Allah?” Akajibu (Abu Sufyaan):
“Ama hili, wallah mpaka sasa bado kuna kitu ndani ya nafsi yangu”. Al-Abbas
akasema: “Ole wako! Silimu na ushuhudie kwamba hapana Mola apasaye kuabudiwa
kwa haki ila Allah na kwamba Muhammad ni Mtume wa Allah, kabla hujapigwa
shingo yako”. (Anasema Al-Abbas): Basi akatoa shahada ya haki. Nikasema:
“Ewe Mtume wa Allah! Hakika Abu Sufyaan ni mtu apendaye fakhri, basi mpe
kitu cho chote”. Akasema (Mtume): “Naam, atakaye ingia nyumbani kwa Abu
Sufyaan, huyo yuko katika amani na atakaye jifungia mlango wake huyo (pia)
yuko katika amani na atakaye ingia msikitini huyo nae yuko katika amani”.
Alipo kwenda ili aondoke, Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akasema: “Ewe Abbas, mzuie kwenye njia panda nyembamba ya
bondeni, mpaka yampitie majeshi ya Allah apate kuyaona”. (Anasema):
Nikatoka nae mpaka nikamzuilia pale alipo niamrisha Mtume wa Allah
kumzuilia. Yakapita makabila na bendera zao, basi halikupita kabila lo lote
ila aliniuliza kuhusiana nalo. Mpaka akapita Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-pamoja na kikosi chake cha kijani kikiwa na Muhajirina na
Answaari-Allah awawiye radhi. Akasema (Abu Sufyaan): “Sub-haanallah ewe
Abbas! Hawa ni kina nani?” nikamjibu: “Huyo ni Mtume wa Allah pamoja na
Muhajirina na Answaari”. Akasema: “Hapana ye yote mwenye ubavu wa kusimama
na hawa! Wallah ewe Abal-Fadhli, kwa yakini asubuhi ya leo ufalme wa mwana
wa nduguyo umekuwa mkubwa!” Nikasema: “Ole wako! Hakika huo ni utume (na
wala sio ufalme)”. Akasema: “Haya na iwe hivyo, halafu...”. nikasema:
“Uokovu kwa watu wako”.
ii.
Abu Sufyaan
awatahadharisha Makureishi na awatolea wito wa kujisalimisha:
Akaenda mpaka
alipo wafikia akapiga ukelele kwa sauti ya juu: “Enyi kusanyiko la
Makureishi! Huyoo Muhammad amekujilieni na jeshi msilo na ubavu nalo. Basi
ye yote ataye ingia nyumba ya Abu Sufyaan, huyo yuko katika amani”. Hind
Bint Utbah akamuinukia akamshika ndevu zake na kusema: “Muueni mzee huyu
mpumbavu”. Akasema (Abu Sufyaan): “Ole wenu! Huyu (mwanamke) asikughurini,
kwani ni kweli kabisa amekujieni Muhammad na nguvu msiyo iweza. Basi ye yote
atakaye ingia nyumba ya Abu Sufyaan, huyo yuko katika amani”. Wakasema”
Allah akuhilikishe! Nyumba yako itatusaidia nini sisi?” Akaendelea kusema:
“Na atakaye jifungia mlango wake, huyo (pia) yuko katika amani na atakaye
ingia msikitini naye yuko katika amani”. Basi watu wakatapanyikia majumbani
mwao na msikitini.
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo fika “Dhiy
Twuwaa” na akawa karibu kuingia Makah. Akalitawanya jeshi kwenye njia zote
zitokazo na kuingia Makah na akawa ameifunga kwa pande zake zote. Akamuamuru
Zubeir Ibn Al-Awwaam aingie na kikosi chake upande mmoja na Sa’ad Ibn
Ubaadah aingie na kikosi chake kwa upande mwingine. Na akamuamuru Khalid Ibn
Al-Waleed kuingia na kikosi chake kwa upande mwingine na akamtanguliza mbele
yake yeye (Mtume) Abu Ubaidah Ibn Al-Jarraah. Na Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaingia kwa upande wa “Adhaakhira” mpaka
akashukia nyanda za juu za Makah, hapo akapiga khema.
iii.
Mtume wa Allah alipupia
mno kutokumwagika damu kusiko kwa lazima:
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie alikuwa na
pupa mno kuhakikisha kuwa damu haimwagiki Makah, akakataza vita. Pupa yake
hii ikamfikisha kumng’oa Sa’ad Ibn Ubaadah madarakani na kumpa madaraka hayo
mwanawe; Qays Ibn Sa’ad. Alichukua khatua hiyo pale ilipomfikia khabari
kwamba Sa’ad amesema akiwakamia Makureishi alipo kuwa akielekea kuingia
Makah: “Leo ni siku ya malanyama! Leo itahalalishwa haramu!” Lakini Allah
Taala zitukukie hekima zake, alitaka katika siku hii ya “ufunguzi – mweupe”
kumwagika baadhi ya matone ya damu. Kwani Khalid Ibn Al-Waleed alipata
upinzani upande wake kutoka kwa baadhi ya Makureishi, akalazimika
kukabiliana na nguvu kwa kutumia nguvu. Hapo wakauawa waislamu wawili na
Makureishi ishirini na kitu. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo
liona tukio hilo alighadhika na kusema: “Mimi sikukataza vita?”,
akaambiwa: Ewe Mtume wa Allah, hakika Khalid alipigwa naye akapigana.
Akasema (Mtume): “Hukumu ya Allah ni kheri”.
|