Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

MTUME WA ALLAH AINGIA MAKKAH KWA UNYNENYEKEVU MKUBWA

 Faida

         Hivi ndivyo majeshi ya waislamu yalivyo ingia Makah bila ya mapambano na ukatimia ufunguzi wa mji wenye amani bila ya mapigano makubwa. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaingia Makah akiwa amempanda ngamia wake. Na hakuingia kama wanavyo ingia washindi kwa mbwembwe na jeuri kuu, bali yeye aliingia katika hali ya unyenyekevu mkubwa akiwa ameinamia chini. Kichwa chake kikirubia kumgusa ngamia wake, hiyo ikiwa ni alama ya shukrani kwa Allah kwa neema hii ya ufunguzi mkubwa aliyo mpa. Mtume akaendelea kuisoma Suratil-Fat-hi [48] mpaka akafika kwenye Al-Ka’abah akiwa pamoja na waislamu. Akaigusa nguzo ya Al-Ka’abah kwa kifimbo chake kidogo, akapiga takbira na waislamu nao wakaiitikia takbira yake. Takbira zao hizi zikautikisa mji mzima wa Makah mpaka Mtume akawaashiria wanyamaze. Halafu Mtume akatufu Al-Ka’abah mbio mbio akiwa amempanda ngamia wake na katika kila mzunguko akiligusa “Hajarul-Aswad” kwa kifimbo chake mpaka akaikamilisha Twawaafu yake.

Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo maliza Twaafu yake akashuka juu ya ngamia wake akaenda “Maqaamu Ibraahim”, hapo akaswali rakaa mbili. Kisha akaenda kwenye maji ya Zamzam akayanywa na kutawadha huku waislamu wakiwa wamemzunguka wakigombea maji yake ya udhu wakijimwagia nyusoni mwao. Mushrikina wakiyaangalia yote hayo kwa mshangao mkubwa wakisema: “Hatujapatapo kamwe kuuona wala kuusikia ufalme kama huu!”

 

         iii.          Mtume wa Allah atoa msamaha mwa maadui zake, msamaha usio na kifani katika Historia:

         Kisha Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akakaa kwenye pembe ya msikiti mtakatifu na Sayyidina Abu Bakri akiwa amesimama nyuma yake na upanga mkononi. Halafu Mtume akamuita Uthman Ibn Twalhah, akaja akamfungulia Al-Ka’abah, akaingia ndani na akaswali humo rakaa mbili. Alipo maliza akasimama mlangoni mwa Al-Ka’abah akasema: “Hapana mola afaaye kuabudiwa kwa haki ila Allah pekee, ameisadikisha ahadi yake, amemnusuru mja wake na ameyashinda makundi peke yake”. Halafu akatoa khutba ndefu, akataja ndani yake jumla ya hukumu za sheria, kisha akasema: “Enyi kusanyiko la Makureishi! Hakika Allah amekuondosheeni ushupavu wa kijahili na kujitukuza kwa mababa. Watu wote wanatokana na Adamu na huyo Adamu anatokana na udongo”. Halafu akaisoma aya hii: “ENYI WATU! HAKIKA SISI TUMEKUUMBENI KUTOKANA NA MWANAMUME NA MWANAMKE. NA TUMEKUJAALIENI KUWA MATAIFA NA MAKABILA ILI MJUANE. HAKIKA ALIYE MTUKUFU ZAIDI KATI YENU KWA ALLAH NI HUYO ALIYE MCHAMNGU ZAIDI KATIKA NYINYI. HAKIKA ALLAH NI MWENYE KUJUA MWENYE KHABARI”. [49:13] Kisha akasema: “Enyi kusanyiko la Makureishi! Mnasemaje na mnadhania mimi nitakufanyeni nini?”. Wakajibu: “Kheri, wewe ni ndugu mwema mwana wa ndugu mwema!”, Mtume akasema: “Ninasema kama alivyo sema ndugu yangu Yusuf: Leo hapana lawama juu yenu. Allah atakusameheni, naye ni Mwingi wa kurehemu kuliko wote wanao rehemu. Enendeni zenuni ilhali mkiwa huru!”

Unaonaje, hivi watu wa Makah walitarajia msamaha huu lau kama mfunguzi wa Makah angelikuwa ni mmoja wapo wa makamanda au wafalme? Naamini kwamba lau tutapekua kurasa za Historia tangu mwanzo wake hadi mwishgo wake, tusingelimpata hata mtu mmoja aliye chukua msimamo huu mtukufu kwa adui zake. Naam, ni ukweli ulio dhahiri kwamba hakuna katika Historia yote msamaha ulio fikia msamaha huu walio upata watu wa Makah. Hii ni kwa sababu hakuna katika watu wote, mwanadamu aliye fikilia ukamilifu wa kiutu kiasi alicho fikia Muhammad; Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Kwa ukweli huu basi, sio ajabu kwa Mtume wa Allah kuchukua msimamo huu wa pekee katika Historia nzima kwa adui zake. Mtume wa Allah hakuwa mmojawapo wa makamanda au wafalme, wala hakuwa akiyalenga yale wayalengayo wafalme; yaani kushibisha matamanio ya nafsi zao. Hakika si vinginevyo, hiyo ilikuwa ni rehema kutoka kwa Allah Taala aliyo ipeleka kwa waja wake na hapo ndipo unapo dhihirika ukweli wa kauli yake Taala: “NASI HATUKUKUTUMA ILA UWE NI REHEMA KWA WALIMWENGU WOTE”. [21:107] Kwa hivyo basi, po pote anapo kuwepo Mtume na rehema ya Allah huwepo pamoja naye, ikamuenea rafiki na adui, muumini na kafiri. Kila mmoja akapata fungu lake katika rehema hiyo, kama vitongoji vya ardhi vinavyo chukua baraka ya mvua, basi ikatoa matunda rutuba yake au ikapoa hewa yake.

 



 | Tuandikie |