Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SOMO LA NNE-MSAMAHA WA MTUME

 Faida

             i.          Msamaha wa Mtume wa Allah wazifungua nyoyo za watu wa Makah kuuelekea Uislamu na kuzijaza mahaba ya Mtume:

         Kwa yakini msamaha huu mtukufu uliteremsha baridi na salama ndani ya nyoyo zile kukutavu ambazo muda mrefu ziliunguzwa na uadui kuielekea nafsi teule hii (Mtume). Na ambazo kwa kipindi kirefu zilipofushwa na hasadi zikashindwa kuuitika moyo – huruma huu (Mtume). Kwani Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliendelea kuwalingania kheri (Uislamu) watu hawa kwa zaidi ya miaka ishirini. Na akijaribu kwa kila njia kuwaelekezea na kuwapondokeshea kwenye kheri hiyo, lakini wao wakawa vipofu wasiione kheri hiyo na viziwi wasiisikie: “NA WAKASEMA: NYOYO ZETU ZIMO KATIKA VIFUNIKO KWA HAYO MNAYO TUITIA, NA MASIKIO YETU YANA UZIWI NA BAINA YETU NA WEWE LIPO PAZIA...” [41:05] Na wakawa wakimbadilishia uadui kwa mapenzi na uovu kwa wema na wakamkadhibisha, wakamkata pande na wakamfukuza Makah. Isitoshe wakampiga vita na kumkusanyia washirika wa kumpiga na wakawa kipindi chote hicho wakiingojea kwa hamu kuu fursa ya kumuangamiza. Sasa Allah alipo mpa ushindi dhidi yao na akammakinisha shingo zao, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akayasahau yote yaliyo pita; yaani uovu na uadui walio mtendea. Na si hivyo tu, akawazawadia msamaha mwema enevu, eeh ni nafsi tukufu iliyoje hii, nafsi inayo lipa uovu kwa wema kwa adui mtenzwa nguvu! Hakika hiyo ni nafsi ya Mtume mtukufu ambaye katu hakuweka nafsini mwake ila kheri na hakuwa akitaka ila utengenevu tu. Na ambaye kamwe hakuwa jabari, dhalimu wala mlipa kisasi na wala hakuwa katika ghadhabu na uradhi wake ila kama asemavyo Allah Taala: “HAKIKA AMEKWISHA KUJIENI MTUME KUTOKANA NA NYINYI WENYEWE (wanadamu), YANAMUHUZUNISHA YANAYO KUTAABISHENI ANAKUHANGAIKIENI SANA. KWA WAUMINI NI MPOLE NA MWENYE HURUMA”. [9:128]

Kwa yakini msamaha huu ulikuwa ni ufunguzi (fat-hi) mwingine ambao kupitia huo Allah alizifungua nyoyo kanushi hizi. Na kupitia ufunguzi huo akakikunja kiwingu cha nafsi kibri hizi, kwa ajili hiyo basi zikawa zinafurikwa na mahaba na ikhlasi. Na zikifuata twaa na zikijiunga chini ya bendera ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa khiari zikiwa nyenyekevu. Na amesema kweli Allah Taala pale alipo sema: “MEMA NA MAOVU HAYALINGANI. PINGA UOVU KWA LILILO JEMA ZAIDI. HAPO YULE AMBAYE BAINA YAKO NAYE PANA UADUI ATAKUWA KAMA RAFIKI JAMAA WA KUKUONEA UCHUNGU. LAKINI HAWAPEWI WEMA HUU ILA WANO SUBIRI, WALA HAWAPEWI ILA WENYE BAHATI KUBWA”. [41:34-35] Hivi ndivyo Makah ilivyo ifungulia milango yake da’awah (ulingano) na ikatupa dini-mapokeo yake na kumfuata Mtume wake aliye muaminifu mwenye kuaminiwa. Kwa hatua/kitendo chao hicho, ngome ya shirki ikawa imebomoka na kuanguka pwaa na kikaondoka kile kikwazo madhubuti kilicho kuwa kikiizuia da’awah kwa zaidi ya miongo miwili. Na tangu siku hiyo, Makah ikawa ndio Ka’abah ya Uislamu na Qiblah cha waislamu wa mashariki na magharibi ya dunia. Na itaendelea kuwa hivyo mpaka hapo Allah atakapo irithi ardhi na vilivyoko juu yake, inshallah.

 

           ii.          Watu wa Makah wala kiapo cha utii kwa Uislamu mbele ya Mtume:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliingia Makah mwezi 20-Ramadhani, mwaka wa nane wa Hijrah (Januari 630 A.D.) Na akabakia humo kwa takriban siku ishirini akipanga na kutengeneza mambo yake (Makah) na kuitoa katika anga la shiriki kuileta katika anga la Uislamu na Tauhidi. Akamuamuru Bilali kuadhini juu ya Al-Ka’abah akapanda juu yake na akaanza kuianikiza sauti yake pande zote: “ALLAAHU AKBAR ALLAAHU AKBAR, ALLAAHU AKBAR ALLAAHU AKBAR. ASH-HADU AN LAA ILAAHA ILLAL-LAAH, ASH-HADU AN LAA ILAAHA ILLAL-LAAH. ASH-HADU ANNA MUHAMMADAN RASUULULLAAH, ASH-HADU ANNA MUHAMMADAN RASUULULLAAH. HAYYA ‘ALAS-SWALAAH, HAYYA ‘ALAS-SWALAAH. HAYYA ‘ALAL-FALAAH, HAYYA ‘ALAL-FALAAH. ALLAAHU AKBAR ALLAAHU AKBAR. LAA ILAAHA ILLAL-LAAH”. Halafu swala ikakimiwa, akainuka Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kuwaswalisha watu katika “Haram” ya nyumba tukufu ya Allah. Na watu nao wakasimama pamoja nae katika safu zao, wakirukuu kwa rukuu yake na wakisujudu kwa sijida yake na wakiinuka kila alipo inuka na wakikaa kila alipo kaa.

Mandhari nzuri hii ikawa na athari yake tendaji ndani ya nafsi za mushrikina miongoni mwa wazalendo wa Makah. Wakaupokea Uislamu kwa khiari zao na wakamkusanyikia Mmtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakila kiapo cha utii kwa Uislamu. Mtume akakaa kuwangojelea katika kilima Swafaa, Sayyidina Umar-Allah amuwiye radhi-akasimama kwenye majlisi ya Mtume akipokea kiapo cha watu kwa niaba ya Mtume. Akawa anachukua kiapo kwao juu ya usikivu na utii kwa Allah na Mtume wake katika yale wayawezayo. Alipo maliza kuchukua kiapo cha wanaume, wakaja wanawake wakila kiapo juu ya kutomshirikisha Allah na cho chote, wala hawataiba, hawatazini. Na wala hawatawaua watoto wao, hawatazua uzushi wanao uzua tu wenyewe baina ya mikono yao na miguu yao na wala hawatamuasi katika jambo jema. Mtume akawapokelea kiapo chao hicho cha utii na akawaombea maghufira kwa Allah. Kwa ajili hiyo basi, Makah ikaingia katika kundi la Uislamu na ikawaenea watu wote roho mpya ya uhuru, udugu na usawa. Na ikawa miongoni mwa mambo yaliyo wasukuma watu wa Makah kuingia katika Uislamu, ni kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-hakumtenza nguvu ye yote kuukubali Uislamu. Pamoja na ukweli kwamba alikuwa na nguvu na mamlaka ya kufanya hivyo, lakini katu hakutumia nguvu yake hiyo kumlazimishia mtu Uislamu. Bali aliwaacha huru kuchagua dini waitakayo; atakaye kuwa muislamu na asilimu na atakaye kubakia na dini yake na abakie. Kiasi kwamba hata Swafwaan Ibn Umayyah alipo kuja kutaka kusilimu, alimwambia Mtume wa Allah: “Nipe khiari miezi miwili”, Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akamwambia: “Wewe una khiari miezi minne”. Pamoja na kwamba huyu Swafwaan alikuwa miongoni mwa wale ambao Mtume wa Allah aliruhusu wauawe, kwa sababu ya uadui wao mkubwa na maudhi yao kwa waislamu. Lakini bado alipewa uhuru wa kuchagua na kuamua, msamaha huu wa Mtume kwa watu alio kwisha toa ruhusa ya kuuawa siku ya Fat-hi Makah ukiuachilia mbali msamaha wake enevu kwa watu wa Makah. Ulikuwa ni miongoni mwa vishawishi na vichocheo vya kukubalika kwa Uislamu Makah, basi haukupita muda mrefu ila wazalendo wote wa Makah walisilimu. Wakaridhia Allah kuwa ndiye Bwana Mlezi wao badala ya masanamu, Uislamu ndio dini yao badala ya ushirikina na Muhammad ndiye mtume wao.

Watu hawa ambao Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliruhusu kumwagika patupu damu yao, walikuwa kiasi cha watu kumi na watano hivi; wanaume na wanawake. Miongoni mwao akiwemo huyu Swafwaan Ibn Umayyah, Ikrimah Ibn Abu Jahli, Wahshiy Ibn Harb; muuaji wa Sayyidina Hamzah na Hind Bint Utbah; mlaji wa ini la Hamzah. Walikuwa ni adui dhahiri aliye fikilia upeo wa uadui na maudhi kwa waislamu. Mtume wa Allah aliwasamehe wengi miongoni mwao, hakuua miongoni mwao ila wanaume watatu na mwanamke mmoja.

 



 | Tuandikie |