Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

MTUME AFUTILIA MBALI ATHARI ZA SHIRKI KATIKA MJI WA MAKKAH

 Faida

 

iii.      Mtume wa Allah azifutilia mbali athari za shirki katika mji wa Makah na vitongoji jirani:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaanza kuzifuta athari za shirki katika mji wa Makah. Akatoa amri ya kuvunjwa masanamu yote yaliyo kuwa yamewekwa kuizunguka Al-Ka'abah. Kama wasemavyo wapokezi wa Sira, yalikuwepo masanamu mia tatu na sitini katika mzingo wa  Al-Ka'abah. Kila kitongoji miongoni mwa vitongoji vya Waarabu kilikuwa na sanamu lake maalumu, basi masanamu yote hayo yakavunjwa kwa amri ya Mtume. Kwa kitendo hicho, athari ya ibada ya miungu sanamu ikawa imefutwa kabisa kwenye Al-Ka'abah tukufu. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo maliza kuitwaharisha  Al-Ka'abah kutokana na athari ya kuabudiwa asiye Allah. Alimuamrisha mlinganiaji kuwalingania watu wa Makah ya kwamba:   "Ye yote mwenye kumuamini Allah na siku ya mwisho, basi asiliache nyumbani kwake sanamu ila amelivunja". Na haikuwepo nyumba yo yote Makah ila ndani yake kulikuwa na sanamu ambalo hutabaruku nalo watu wa nyumba hiyo na wakijipangusa nalo wanapo ingia au kutoka nyumbani. Watu wa Makah wakaupokea munada wa Mtume kwa utii ulio tukuka, wakayaendea masanamu waliyo kuwa wakiyaabudu na kuyavunja vunja. Hind Bint Utbah akawa analipiga shoka sanamu lake hata akalivunja vipande vipande ilhali akisema: "Tulikuwa ghururini kwako".

Halafu Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akavituma vikosi kwenda kwa makabila ya Waarabu yaliyo izunguka Makah. Waende huko kuyavunjilia mbali masanamu ya huko, akamtuma Khalid Ibn Al-Waleed kukiongoza kikosi cha watu thelathini kwenda "Batwn Nakhlah" kulivunja "Uzzah". Hili ndilo lililo kuwa kubwa la masanamu ya Makureishi, akalivunja kama alivyo amrishwa. Akamtuma Amrou Ibn Al-Aaswi na kundi la waislamu kwenda kwa kabila la Hudheil ili kulivunja sanamu lao "Swuwa'a", akalivunja. Akamtuma Sa'ad Ibn Zayd kwenda Mushallal katika mwambao wa pwani na watu ishirini kulivunja "Manaata"; sanamu la kabila la Kalbi na Khuzaah, akalivunja. Namna hivi ndivyo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alivyo kuwa akizifuta sura/alama na athari za shirki katika mji wa Makah na vitongoji vyake. Hadi athari zake ziondoke kabisa ndani ya nafsi na mpaka akili zihajiri mawazo/fikra za mapokeo na ada na nyoyo zitakate na kila kinacho zizuia kufungamana na Allah Mola pekee asiye na mshirika.

SOMO LA TANO – VITA VYA HUNEIN

i.      Kabila za Hawaazin na Thaqiyf zajiandaa kumshambulia Mtume, lakini Mtume awawahi:

         Makabila mawili; Hawaazin na Thaqiyf yalichelea kunyolewa na wembe ulio wanyoa Makureishi, wakavunjiwa masanamu yao na kubadilishiwa dini yao ya tangu na tangu. Ukaondoshwa utukufu na fakhri yao na wakawa chini ya mamlaka ya kijana mdogo; Muhammad, wakachelea kufikwa na haya yaliyo wafika Makureishi. Kabila la Thaqiyf lilikuwa na makazi yake Twaif, likijiranikiana na Hawaazin walio ishi kwenye majabali yanayo kizunguka kitongoji cha Twaif. Twaif ndicho kilicho kuwa kitongoji chenye ardhi yenye rutuba kuliko vitongoji vyote vya rasi ya Waarabu. Na ndio iliyo kuwa makao ya "Laata"; sanamu kubwa la Waarabu baada ya "Hubal". Wazalendo wa Twaif wakadhania kwamba Muhammad akisha wamaliza Makureishi, lazima atakuja kwao. Watu wenye busara na sauti kutoka katika makabila mawili haya; Hawaazin na Thaqiyf wakakutana na kushauriana. Baada ya mashauriano yao hayo, wakawafikiana kwa kauli moja kumshambulia Mtume kabla hajawashambulia wao. Yakajiunga nao makabila ya Naswru, Jusham, Sa'ad Ibn Bakri na baadhi ya watu wa kabila la Baniy Hilaal. Wakapata watu wengi, washirika hawa walipo kusanyika wakampa uongozi Maalik Ibn Auf; mtu wa kabila la Naswru awaongoze katika mapambano yao dhidi ya Muhammad.

Huyu Maalik Ibn Auf alikuwa ni kijana mbichi, mwingi wa jazba, akaona asiwapeleke watu wake katika medani ya vita ila kwa hamasa/jazba na mori mkubwa. Akawatoa watu wake kwenda medanini wakiwa pamoja na mali, wake na watoto wao ili kuwatia hamasa na kuwafanya kuwa tayari kufa kwa ajili ya kuilinda heshima yao. Miongoni mwa watu wake alikuwemo Duraid Ibn Swimah ambaye alikuwa mzee aliye komazwa na uzoefu na vita, akawa na uoni wa mbali. Lakini wakati huo alikuwa ni mtu mzima sana, kwa hivyo hakuwa tena na uwezo wa kuongoza jeshi. Alipo sikia juu ya mpango huu wa kamanda kijana; Maalik Ibn Auf, akamuuliza sababu ya kufanya hivyo, Maalik akamjibu: "Hakika si vinginevyo, nimetaka niweke nyuma ya kila mtu mke na wanawe na mali yake ili awapiganie". Duraid akamuuliza: "Je, mtu aliye shindwa ana matashi? Hakika kama ushindi ni wako, basi hatokunufaisha ila mtu na upanga na mkuki wake basi. Na fungu lako likiwa ni ushindwa utakuwa umefedheheshwa kwa ahali zako na mali yako". Lakini Maalik akawa mkaidi asimsikilize mtu mzima huyu mwenye busara, uoni na uzoefu wa kutosha. Akaishikilia rai yake, akatoka na watu wake kwenda kwenye medani ya vita, wakiwa na familia zao na mali yao.

Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasikia juu ya maandalizi kabambe yaliyo fanywa na Hawaazin na Thaqiyf dhidi yake. akamtuma jasusi miongoni mwa majasusi wake akampelelezee ukweli wa khabari hii iliyo mfikia. Ulipo mbainikia ukweli wa azma yao juu yake, Mtume akapanga kuwashambulia kwa kuwashtukiza kabla wao hawajamuwahi. Akatoka Makah siku ya Jumamosi, mwezi 6-Shawaal {28/January/630 A.D.} akiwakusudia Hawaazin na Thaqiyf akiwa na watu alfu kumi na mbili; watu alfu kumi alio kuja nao Makah na alfu mbili katika watu wa Makah. Watu wa Makah walishiriki katika vita na wakampa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-msaada wa mali na silaha alio utaka. Swafwaan Ibn Umayyah alimwazima Mtume nguo mia moja za vita (dir-u) na baadhi ya watu watukufu wa Makah walimkopesha mali zao ili kumuwezesha kufanikisha vita. Na wakatoka pamoja naye watu wengi katika mushrikina, jeshi likatoka katika mandhari ya nguvu kubwa likiwa na alama zote za ushindi. Kiasi cha kuwafanya waislamu kudhania kwamba katu hawatoshindwa kwa wingi wao huo mpaka yasemekana kwamba wanawake na watoto wa Makah walitoka nyuma ya jeshi hili kwa tamaa ya kupata ngawira. 

 



 | Tuandikie |