Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

MKAKATI WA MAADUI ULIKUWA NI KUWASHAMBULIA KWA GHAFLA

 Faida

 

           ii.          Mkakati wa adui ulikuwa ni kuwashambulia waislamu kwa ghafla kutokea kila upande wakati wa alfajiri:

         Hawaazin na Thaqiyf na washirika wao miongoni mwa makabila ya Kiarabu walikuwa tayari wamesha toka na watu wao kuelekea bonde la Hunein. Hili ni mojawapo ya mabonde ya Tihaamah, bonde lenye mteremko mkali, lililo tandawaa katika njia nyembamba za majabalini. Maalik Ibn Auf akaonelea apige kambi katika maingilio ya bonde hili na aitumie hali – maumbile ya mahala hapo  katika kuzivunja nguvu za waislamu. Akakipanga kimoja cha vikosi vyake juu ya zile njia finyu za majabalini na vikosi vilivyo salia akavipanga pembeni mwa jangwa na fichifichi zake. Na akawapa amri warusha mishale wake kukishambulia kwa nguvu zote kikosi cha mwanzo cha waislamu mara tu kitakapo tokezea. Wawamwagie mvua ya mishale kutokea pande zote mpaka waingiwe na kiwewe, mashambulizi haya makali na ya kushtukiza yatauharibu mpango wao mzima wa vita. Hapo ndipo jeshi litawavaa nao wakiwa katika hamkani na kutoa pigo takatifu litakalo wamaliza kabisa na kuwafanya wasalimu amri.

Hivi ndivyo Maalik Ibn Auf alivyo upanga mkakati wake wa vita, kama kwamba alitambua mkakati wa adui yake nae akaanzia hapo hapo. Riwaya mbali mbali zimetaja kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alifika Hunein jioni ya siku ya Jumatatu, mwezi 10-Shawwal. Ulipo ingia usiku, Maalik Ibn Auf akawaendea watu wake na kuwapanga katika medani ya vita; bonde la Hunein. Akawapa amri ya kumshambulia Mtume na maswahaba wake mashambulizi ya mtu mmoja. Mtume kwa upande wake, akawapanga maswahaba wake kivita wakati wa maladaku (karibu na alfajiri). Akawapanga safu safu na kuwapa bendera za vita wanao stahiki miongoni mwa Muhajirina na Answari na kabila za Waarabu. Akamuweka Khalid Ibn Al-Waleed mbele ya kikosi cha farasi, kama kwamba mkakati wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ulikuwa ni kumshtukiza adui wakati wa kabla ya alfajiri. Wakati ambao watu huwa wamelala fofofo na si Mtume wala maswahaba wake aliye kuwa anajua kuwa tayari adui yao kesha watangulia. Wakiwa wamejificha kuwangojelea katika vichochoro na finyu za majabalini.

 

         iii.          Adui awashtukiza waislamu na kuwafanya kutapanyika hovyo:

         Katika kiza cha alfajiri, waislamu wakasonga mbele, kikaenda kikosi chao cha mbele cha wapanda farasi chini ya uamiri wa Khalid Ibn Al-Waleed. Nyuma yake vikifuatia vikosi vingine vya jeshi na nyuma ya jeshi hili akafuata Mtume wa Allah akiwa amempanda nyumbu wake mweupe. Akiwa amevaa vazi rasmi la vita, akizungukwa na maswahaba kadhaa mongoni mwao akiwemo ami yake Abbas Ibn Abdul-Mutwalib. Kikosi cha mbele kilipo kanyaga tu maingilio ya bonde, kikashtukizwa na mvua ya mishale inayo washukia katika kiza kutokea kila upande. Kiasi cha kutotambua mvua hiyo inatokea mbinguni au ardhini, ardhi pamoja na ukunjufu wake ikawawia finyu na hawakuwa na budi ila kurejea nyuma. Urejeaji nyuma wao huu ulikuwa ni wa ghafla na usio na mpangilio, adui akaitumia vema fursa hiyo, akashambulia kwa farasi na miguu. Akieneza kwa waislamu michomo ya mishale na mapigo ya panga hata yakafumuka mauaji katika kabila la Baniy Naswri Ibn Muaawiyah kisha yakapindukia kwa Baniy Ruaab. Kizaizai  na kimuhemuhe kikalienea jeshi la waislamu, safu zake zikatambaliwa na khofu ya ushindwa, watu wakaanza kurudi nyuma hovyo bila ya kujielewa.

 

         iv.          Mtume wa Allah athibiti mbele ya adui na awaita watu kurejea katika medani ya vita:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo kiona kitimtim na fazaa hii na akawaona maswahaba wake wakikimbia hovyo hovyo. Akaanza kuwapigia ukelele: “Mnaenda wapi watu nyie! Njooni kwangu, mimi ni Mtume wa Allah! Mimi ndiye Muhammad mwana wa Abdul-Mutwalib!...”

Mimi ndiye Mtume wala si uongo *** mimi ndiye kijana wa Abdul-Mutwalib!

Maswahab wakiwa katika kizaizai chao, hawasikii wala hawafahamu, wala hawatambui cho chote katika vilivyo wazunguka. Mpaka wakachangukana na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakimuacha na watu wachache katika Muhajirina na Answaari na watu wake wa nyumbani (jamaa/ndugu zake). Abbas Ibn Abdul-Mutwalib; ami yake Mtume, alikuwa ni mtu mwenye sauti kali, Mtume akampa amri awakhofishe Muhajirina na Answaari warejee. Abbas akaanza kupiga mayowe: “Enyi kusanyiko la Answaari ambao mlitoa makazi na mkamnusuru Mtume nyiee! Enyi kusanyiko la Muhajirina ambao mlikula kiapo cha utii chini ya mti ule nyiee! Njooni kwa Mtume wa Allah nyieee!” Ukelele ule ulipo gonga tu ngoma za masikio yao, ukawa kama ni dawa iliyo warejeshea fahamu zao wakageuka wakichupiana kwa Mtume wa Allah ilhali wakisema: “Labbayka Labbayka!” Kiasi cha kufikia mmoja wao kushuka juu ya ngamia wake na kukimbia kwa miguu kutokana na kuzuiwa na msongamano wa watu. Akiharakia kwa Mtume, akiwa na upanga na ngao yake, likakusanyika kumzunguka Mtume kundi la watu wakweli katika azma na imani yao. Likasimama kidete mbele ya adui mpaka likafanikiwa kuyazuia mashambulizi yake, halafu tena waislamu wakakamatana barabara. Na wakati huo tayari kulikuwa kumesha pambazuka, wakaweza kuona maficho ya adui, wakamshushia mashambulizi ya mtu mmoja. Makundi ya adui yakatapanywa kama kundi la nzi walio kurupushwa, waislamu wakawa wanawafukuza, wakauawa walio uawa, wakatekwa walio tekwa na wakakimbia walio ponyoka. Ama kiongozi wao; Maalik Ibn Auf, yeye alikimbilia kwenye ngome za Twaif akapata hifadhi humo, huku akiacha nyuma yake kila alicho kiswaga; mali, wanyama, wanawake na watoto. Waislamu wakapata ngawira nono mno ambayo ni dhiki mno kuihesabu ukaisha.

 



 | Tuandikie |