Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

MTUME AWAFUATILIA MAADUI HADI TWAIF

 Faida

 

         iv.          Mtume wa Allah awafuatilia maadui mpaka Twaif baada ya kuwasambaratisha Hunein:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaamuru mateka na mali zikusanywe na kupelekwa katika bonde la “Ji’iraanah”. Halafu Mtume na maswahaba wake wakaenda Twaif, ambako Maalik Ibn Auf na baadhi ya watu wake na wale wa Thaqiyf walio ponyoka walikimbilia huko. Thaqiyf walikuwa wamejihifadhi ngomeni mwao na kufunga milango yake na wakawa wamechukua chakula na silaha za kutosha muda mrefu. Hayo yakiwa ni maandalizi ya botari (mzingiro) ndefu, iwapo Mtume ataamua hivyo. Na Thaqiyf walikuwa na umahiri mpevu kwa mapigano ya ndani ya ngome, wakakongamana kuzilinda ngome zao kwa nguvu zao zote. Na kuzuia kila jaribio litakalo fanywa na waislamu kwa lengo la kuzifikia na hatimaye kuzifungua ngome zao.

Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alipo fika Twaif na akaona watu wake wamejitia ngomeni, akataka kuwangojelea kidogo akitumai huenda wakajisalimisha wenyewe bila ya vita. Lakini alipo karibia tu ngome za Twaif, ikamnyeshea mvua ya mishale, likauawa kundi la waislamu na lingine kujeruhiwa. Mtume na naswahaba wake wakarudi nyuma umbali ambao mishale haiwezi kufika, hapo akapiga kambi kuzizunguka ngome zile. Akawapiga botari kwa takriban siku sihirini na moja.

 

SOMO LA SITA.

 

             i.          Waislamu watumia njia zote kuwatoa maadui ngomeni mwao bila mafanikio:

         Ndani ya kipindi chote hicho, waislamu wakawa wanatumia njia/mbinu mbali mbali kuwatoa maadui ngomeni mwao bila mafanikio. Wakawataka watoke baadhi yao kuja katika mapambano ya wawili wawili (mubaarazah), wakakataa, wakawaibisha kwa uoga na kutimua mbio, hilo pia lisiwatoe. Wakafunga kombeo kubwa na kuwarushia mawe makubwa ili kubomoa maingilio ya ngome, mawe hayo hayakufikia lengo. Baadhi ya waislamu wakaingia katika kifaru (tank) cha mbao, wakasonga mbele ili kwenda kuutoboa ukuta wa ngome. Thaqiyf wakawarushia vipande vya chuma vilivyo tiwa motoni vikawa vyekunduu, hivi vikawaunguza na kuwalazimisha waislamu kutoka ndani ya kifaru chao cha mbao. Hapo wakarushiwa mawe na kuuawa baadhi yao, baada ya jaribio hilo la kubomoa ukuta kukwama waislamu wakaanza kukata mizabibu yao. Thaqiyf wakamtumia ujumbe Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakimuomba asiikate, aiache kwa ajili ya Allah na ndugu, Mtume akawakataza waislamu wasiendelee kuikata.

Naam, hivi ndivyo waislamu walivyo jaribu kwa kila njia/mbinu zao kuwatoa mushrikina ndani ya ngome zao au kuwaingilia humo, wasiweze. Mtume wa Allah akaamrisha upigwe munada kwa watumwa wa Thaqiyf ya kwamba: “Ye yote atakaye toka kuja kwetu, basi huyo yuko huru”. Watumwa wale walipo usikia munada huo, wakapenya miongoni mwao kiasi cha watu kumi na kitu, Mtume akawaacha huru kama alivyo ahidi.

 

           ii.          Mtume wa Allah asitisha mzingiro wa adui:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akajua kupitia kwa wale watumwa alio waacha huru, kwamba Thaqiyf wamejitia ngomeni na chakula cha kutosha mwaka mzima. Na kwamba wao wameazimia kubakia ngomeni mwao humo mpaka hapo chakula chao kitakapo malizika, hapo ndipo watatoka na kupigana hadi mtu wa mwisho. Mtume akaona kwa taarifa hii aliyo ipata, hakuna faida ya kuendelea na botari na kwamba hivi sasa nguvu ya adui imekatika hatoweza kuleta madhara tena. Na kwamba katika maficho yake hayo amekuwa mithili ya kicheche ndani ya shimo lake; akimngojelea atamkamata na akimuacha hatamdhuru. Na miezi mitukufu ambayo vita vimeharimishwa ndani yake ilikuwa inakaribia, Mtume akaonelea afunge msafara na maswahaba wake wamuache adui huyu kwa muda. Huenda Allah akawaongoa, wakamjia ilhali wakiwa waislamu watiifu na hivyo ndivyo ilivyo kuwa. Yakamthibitikia Mtume wa Allah yale aliyo yatamani, kwani haikupita ila miezi michache tu, Thaqiyf wakaukubali Uislamu na wakaingia katika dini ya Allah kwa uradhi wa nafsi zao, wakiwa wanyenyekevu.

 



 | Tuandikie |