Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

MTUME ATUMIA ZAWADI NONO KUWASHAWISHI VIONGOZI

 Faida

 

         iii.          Mtume wa Allah atumia zawadi nono kuwashawishi viongozi wa Makureishi kusilimu:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-na maswahaba wake-Allah awawiye radhi-wakaondoka kurejea “Ji’iraanah; mahala ambapo ngawira ya Hunein ilihifadhiwa. Huko Mtume akaamuru ngawira hiyo ihesabiwe, wakakutikana ngamia ishirini na nne alfu, mbuzi/kondoo arobaini alfu. Wakia alfu nne za madini ya fedha, na wanawake na watoto alfu sita. Mtume wa Allah akawaweka kando mateka wale (wanawake na watoto), akaanza kugawa mali baina ya maswahaba wake. Fungu la mpiganaji wa miguu likawa ni ngamia wanne na mbuzi/kondoo arobaini na fungu la mpanda farasi likawa ni mara tatu ya hivyo.

Na zilivyo kuwa nafsi kwa mujibu wa maumbile yake ni zenye kuchomozea mali na kukawa kutoa ni ufunguo miongoni mwa funguo za nyoyo na mlango miongoni mwa milango ya nafsi. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akazidisha mgao kwa kundi la watukufu katika Makureishi, viongozi na maamiri wa Waarabu. Akikusudia kwa yote hayo, kuzivutia nyoyo zao kwenye Uislamu. Mtume alitambua kwamba wengi miongoni mwa walio silimu katika kundi hili la viongozi, bado wana pepeso za jahilia. Na kwamba wengi miongoni mwa ambao hawajasilimu, walitoka katika vita hivi kwa tamaa tu ya kupata ngawira. Kwa ajili hii basi, Mtume akaona ni vema azitie nguvu nyoyo zao kwa kuwamegea fungu nono la mali. Hili likapelekea kusilimu kwa wale ambao walikuwa si waislamu na kuzidi imani ya Uislamu kwa wale walio kwisha silimu.

Imeandikwa katika kitabu [IMTAA’UL-ASMAA] kwamba Abu Sufyaan Ibn Harb alikuja mbele ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-na ilhali fedha ikiwa mbele yake, akasema: “Ewe Mtume wa Allah wee! Umekuwa mwingi wa Makureishi kwa mali!” Mtume akatabasamu, Abu Sufyaan akasema: “Nipe katika mali hii ewe Mtume wa Allah, Mtume akasema: “Ewe Bilaali, mpimie Abu Sufyaan wakia arobaini za fedha na mpe ngamia mia moja”. Abu Sufyaan akasema: “Na mwanangu Yazid je?”, Mtume akasema: “Mpimie Yazid wakia arobaini na mpeni ngamia mia moja”. Abu Sufyaan akasema: “Na mwanangu Muaawiyah, ewe Mtume wa Allah”. Mtume akasema: “Ewe Bilali mpimie wakia arobaini na umpe ngamia mia moja”. Abu Sufyaan baada ya kupewa vyote hivyo akasema: “Hakika kwa yakini wewe ni karimu, nakufidia baba na mama yangu. Wallah nilikupiga vita, basi neema/bora ya mpigwa vita ni wewe! Kisha nikakupa amani, basi bora ya mpewa amani ni wewe! Allah akujaze kheri!”

Na imepokewa kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-siku hiyo alimpa Swafwaan Ibn Umayah ngamia mia moja, kisha mia wengine na mia tena. Halafu akamuona akilikodolea macho bonde lililojaa mifugo, akamuuliza: “Limekupendeza bonde hili ewe Abu Wahab?”, akajibu: “Naam”. Mtume akamwambia: “Hilo ni lako na vyote vilivyomo humo”. Swafwaan akasema: “Hakika wafalme hawawi na nafsi njema kiasi hiki, nafsi ya ye yote haikuwa njema kiasi hiki ila mtu huyo ni mtume. Nashuhudia kwamba hapana afaaye kuabudiwa kwa haki ila Allah na kwamba wewe ni Mtume wa Allah.

 

         iv.          Baadhi ya maswahaba walishindwa kuiona falsafa ya Mtume katika hili na kuanza kumdhania dhana mbaya:

         Ilifichikana kwa wengi miongoni mwa maswahaba hekima ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-katika upaji na utoaji huu kwa makundi fulani ya watu. Mpaka baadhi ya watu wakafikia kusema: “Hakika wallah mgao huu si wa uadilifu na wala haukukusudiwa kwao dhati ya Allah”. Mtume wa Allah alipo yasikia maneno hayo, alighadhibika mno akasema: “Ni nani basi atakaye fanya uadilifu ikiwa Mtume wa Allah hakufanya uadilifu? Allah amrehemu Musa aliudhiwa kwa maudhi makubwa kuliko haya, akasubiri”. Na hata ikafikia mabedui kuchelea mali zote kuchukuliwa na watukufu/viongozi hao, wakamfuata Mtume wa Allah wakisema: “Ewe Mtume wa Allah, tugawie fungu letu”. Wakamshikilia na kumng’ang’ania hadi wakamshurutisha kukaa penye mti, wakampokonya shuka lake la kujitandia. Mtume akasema: “Enyi watu nyie, nirejesheeni shuka langu, wallah lau mimi ningelikuwa na mifugo kwa idadi ya miti ya Tihaamah, kwa yakini ningelikugawieni wote. Kisha msinikute mimi kuwa ni bakhili, wala muoga wala muongo”. Halafu akaung’oa unywele kutoka katika nundu ya ngamia, akauinua baina ya vidole vyake akasema: “Wallah mimi sina katika mgao wenu hata unywele huu ila khumsi (1/5) na hiyo khumsi yenyewe imerejeshwa kwenu”.

Hekima/falsafa hii ilifichikana hata kwa Answaari, kiasi cha kufikia kunong’ona baina yao. Imepokewa kutoka kwa Abu Said Al-Khudriy-Allah amuwiye radhi-amesema: “Zama Mtume wa Allah alipo wapa kile alicho wapa Makureishi na kabila za Waarabu katika mali ile. Na Answaari hawakupata cho chote katika mali hiyo, kikundi hiki cha Answaari kikatokota kwa ghadhabu nafsini mwao, mpaka akafikia kusema mmoja wao: “”Wallah Mtume wa Allah amekutana na jamaa zake”. Sa’ad Ibn Ubaadah akaingia kwa Mtume wa Allah akasema: “Ewe Mtume wa Allah, hakika kikundi hiki cha Answaari kinaunguzwa na ghadhabu juu yako ndani ya nafsi zao kwa ajili ya vile ulivyo fanya katika mali hii uliyo ipata. Ukawagawia jamaa zako na ukatoa mali adhimu kwa makabila ya Waarabu na kikundi hiki cha Answaari hakikupata cho chote katika mali hiyo”. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akauliza: “Wewe uko upande gani katika hilo ewe Sa’ad?”, akajibu: “Ewe Mtume wa Allah, mimi siko ila pamoja na jamaa zangu”. Mtume akasema: “Haya nikusanyie jamaa zako hao katika uwanja huu”.

 



 | Tuandikie |