Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

MALEZI MATUKUFU

 Faida

 

SOMO LA SABA.

 

        i.               Malezi matukufu:

         Sa’ad akatoka akawakusanya Answaari katika uwanja ule alioagizwa na Mtume, Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akawaendea. Akamuhimidi Allah na kumsifia kwa sifa stahiki zake, halafu akasema: “Enyi kusanyiko la Answaari! Ni maneno gani haya yaliyo nifikia kutoka kwenu?! Na ghadhabu mliyo nayo juu yangu ndani ya nafsi zenu?! Je, mimi sikukujilieni ilhali mu wapotofu, Allah akakuongozeni! Na ilhali mkiwa mafakiri, Allah akakupeni ukwasi, na ilhali mkiwa maadui Allah akaziunganisha nyoyo zenu?!” Wakasema: “Kwani ndivyo hivyo hivyo usemavyo, Allah na Mtume wake wana fadhila na neema kuu juu yetu”. Halafu Mtume akaendelea kusema: “Je, hamnijibu enyi kusanyiko la Answaari?, wakauliza: “Tukujibu nini ewe Mtume wa Allah? Fadhila na neema ni zake Allah na Mtume wake”. Mtume akasema: “Ama wallah, lau mngelitaka mngelisema na mngekuwa mmesema kweli na mngesadikiwa (mngesema hivi): Ulitujilia ilhali ukiwa mwenye kukadhibishwa, sisi tukakusadiki. Na ukiwa huna wa kukunusuru, sisi tukakunusuru. Na ilhali ukiwa umefukuzwa, sisi tukakupa makazi na ukiwa fakiri tukakukwasia kwa mali zetu. Hivi enyi kusanyiko la Answaari mmeghadhibika nafsini mwenu kwa sababu tu ya kitu kidogo cha dunia nilicho zitia nguvu kwacho nyoyo za watu ili wapate kusilimu na nyinyi nikakuachieni Uislamu wenu? Hivi hamridhii enyi kusanyiko la Answaari, watu waondoke na mbuzi na kondoo nanyi mkarejea na Mtume wa Allah kambini kwenu?! Naapa kwa yule ambaye nafsi ya Muhammad i mkononi mwake, lau si Hijrah basi mimi ningekuwa mtu miongoni mwa Answaari. Na lau watu wangelipita katika njia moja na Answaari wakapita njia nyingine, basi mimi ningelipita njia ya Answaari. Ewe Mola wa haki wee! Warehemu Answaari na watoto wa Answaari na wajukuu wa Answaari”. Kwa maneno haya ya Mtume, watu wakalia kiasi cha kuzilovya ndevu zao machozi na wakasema: “Tumeridhia Mtume wa Allah kuwa ndiye mgao na fungu letu”.

Hili likawa ni somo la kina miongoni mwa masomo ya malezi matukufu alilolitoa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa maswahaba wake khususan na uma jamia. Tena limetolewa katika wakati munasibu kabisa na unaofaa khasa kwa mtu kuweza kufaidika na kunufaika na somo. Somo hilo likawainua na kuwaweka daraja ya juu katika daraja za utukufu wa kibinadamu. Daraja iliyo wafanya kuwa juu ya mali, cheo na juu ya kila wanacho kigombea watu miongoni mwa starehe na mapambo ya dunia.

 

      ii.               Imani ndio silaha ya kwanza ya muumini:

         Kama ilivyo kuwa ngawira katika vita vya Hunein ni somo miongoni mwa masomo ya malezi matukufu kwa waislamu makhsusi. Ndivyo ambavyo kushindwa katika vita hivyo kumekuwa ni katika jumla ya masomo ya malezi matukufu kwa waislamu wote. Kwani waislamu walitoka kwenda katika vita hivi baada ya kuwa Allah amewafungulia makomeo ya Makah. Na baada ya kuwadhalilishia wao kiburi na jeuri ya Makureishi na baada ya kuwamilikisha suala la nyumba tukufu (Al-Ka’abah). Na akawamakinishia tosi za Waarabu na Ghuba yote ikakurubia kuifuata dini yao na kuwa chini ya mamlaka yao. Walitoka wakiwa katika mlipuko wa ushindi kwa sababu ya yote haya na wakiwa katika majiono makubwa kutokana na wingi wa idadi yao na nguvu ya zana za vita walizo kuwa nazo. Wakauangalia wingi wao wakajiona na wakatulizana kwao na wakadhania kwamba wingi wao huo ndio kila kitu. Basi Allah Taala akataka kuwafundisha kwamba wakati mwingine wingi hughuri na kwamba nguvu mara nyingine hukhini. Na kwamba nusra/ushindi u mikononi mwa Allah na kwamba njia na msingi wake, hakika si vinginevyo ni imani ya kweli kwa Allah na wema wa kumtegemea yeye. Na kwamba wingi, zana, maandalizi, mkakati wa vita na vinginevyo vyote ambavyo waislamu wanatakiwa kuwa navyo kama sababu ya nguvu. Hakika vyote hivyo vinasimama juu ya msingi huo na vinahitaji nguvu kutoka kwa msaidizi huyu (Allah).

Katika vita hivi waislamu walifikilia wingi ambao haukuwahi kufikiwa kabla, basi je wingi wao huo uliwasaidia kwa cho chote? Hawakuwa wao pamoja na wingi wao huo ila washindwa, wakipaparika mbele ya adui yao mpapariko wa mumbwi hadi kufikia kuchekwa na wachekao, akanena mneni wao: “Ehee hivyo uchawi umebatilika leo, basi na ushindwa wao ukomelee baharini”. Lakini kitu kimoja tu ndicho kilicho okoa hali hiyo, nacho ni hili kundi dogo ambalo lilikamatana na imani yake na likamzunguka Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Nae akaanza kukitia nguvu kwa ukweli na yakini yake na akazielekeza nyoyo na nafsi zao kwa Allah aliye na nguvu ili zipate msaada na nguvu kutoka kwake. Kundi dogo hili lilipo zitakasa nyoyo na nafsi zao kwa Allah na zikawa na mafungamano mema nae, likajiwa na msaada kwa haraka ya ajabu. Hapo ndipo udhaifu wake ukageuka kuwa nguvu na ushindwa wao ukawa ni nusra/ushindi.

 



 | Tuandikie |