Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

UKWELI HALISI WA KUDUMU UNAOPASA KUJULIKANA 

 Faida

    iii.               Ukweli halisi wa kudumu unao pasa kujulikana na waislamu wa leo:

         Naam, namna hivi waislamu walizitegemea nafsi zao kwa kipindi cha mchana na Allah akawatupa mkono. Hapo ndipo ukapatikana ushindwa pamoja na wingi wa idadi na zana za kivita. Walipo tanabahi wakarejea kwa Bwana Mlezi wao na kumtaka msaada, ukawajia msaada huo, kuungwa mkono na kutiwa nguvu. Hapo ndipo ikapatikana nusra na ushindi mtukufu: “HAKIKA ALLAH AMEKUNUSURUNI KATIKA MAPIGANO MENGI, NA SIKU YA HUNAYNI AMBAPO WINGI WENU ULIKUPANDISHENI KICHWA, LAKINI HAUKUKUFAENI KITU. NA ARDHI IKWA DHIKI KWENU JUU YA UPANA WAKE. KISHA MKAGEUKA MKARUDI NYUMA. KISHA ALLAH AKATEREMSHA UTULIVU WAKE JUU YA MTUME WAKE  NA JUU YA WAUMINI. NA AKATEREMSHA MAJESHI AMBAYO HAMKUYAONA, NA AKAWAADHIBU WALE WALIO KUFURU. NA HAYO NDIO MALIPO YA MAKAFIRI”. [9:25-26]

         Hivi ndivyo Allah anavyo ielezea hali ya waumini ilivyo kuwa katika vita vya Hunein ambamo aliwapa somo la kiamalia, nao wakawaidhika nalo na kujifunza kutokana nalo. Basi je, waislamu leo wanajua uhalisia wa hali yao? Na je, wanakihisi kiwango cha udhaifu wao mbele ya adui yao? Na je, wanaijua siri ya udhaifu walio nao pamoja na wingi wao kiidadi ukiwalinganisha na adui yao? Hakika siri hii, iko wazi uwazi wa jua kwa kila aonaye, lakini waislamu wa leo wanaifumbia macho. Na wanavizika vichwa vyao mchangani mithili ya mbuni ili wasiione, kwani ni kweli kabisa kwamba leo waislamu wameigura dini yao. Wamemsahau Allah wakayatupa mafundisho ya Mtume wake, naye akawasahaulisha nafsi zao hata wakashindwa kujitambua. Wakawa mithili ya mmea ulio kauka maji yake, kikakosekana chakula chake, ukawa bua linalo peperushwa na upepo. Kwa yakini waislamu leo ni wengi mno duniani ukiwalinganisha na wale wa wakati wa Mtume na baada yake kidogo. Lakini wingi wao hauwasaidii kwa cho chote ila kuzidi udhalili na unyonge na kukhasimiana wao kwa wao. Po pote unapo waona utakuta na kugundua kuwa wanatawaliwa na maadui wa dini yao ama moja kwa moja au kwa mkono wa siri. Hao ndio waendeshaji wa mambo yao yote kiasi hata cha kufikia kuingilia dini yao, hao ndio wezi na wafaidika wa rasilimali za nchi zao. Udhalimu na ukandamizaji wao huo huupangia mikakati ya wazi na kuipitishia maazimio na mikataba katika makongamano na mikutano yao. Namna hivi ndivyo inavyo thibitika kauli ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa waislamu wa leo: “Mataifa yanakurubia kuitana dhidi yenu kama walaji wanavyo itania sahani (ya chakula)…” Maswahaba wakauliza: Je, huko ni kutokana na uchache wetu zama hizo, ewe mtume wa Allah? Akajibu: “Hapana, bali nyinyi zama hizo mtakuwa wengi, lakini mtakuwa takataka mithili ya povu la bahari”.

Hakika hali ya waislamu leo pamoja na wingi wao, inashabihiana na hali waliyo kuwa nayo waislamu wa mwanzo katika vita vya Hunein. Wingi wao ulipo wavimbisha kichwa, halafu usiwasaidie kwa lo lote. Tofauti pekee iliyopo baina ya waislamu sisi wa leo na wale wenzetu walio tutangulia katika kuiweka misingi ya dini hii. Ni kwamba waislamu wa Hunein walitanabahi na kuzinduka, haraka wakarejea kwa Bwana Mlezi wao nae akawaletea haraka nusra na msaada wake. Ama waislamu wa leo, bado wanaendelea kukoroma usingizini  na wanajitenga mbali na njia ya sawa itakayo waondosha katika udhalili na unyonge ulio wagubika gubigubi. Je, bado haujafika wakati kwa waislamu kuamka usingizini mwao na wakazinduka kutokana na mghafala ulio wapata?! Na wakaiunga hali yao hii na ya wakale wao watukufu na masiku yao yale ya mng’aro?! “JE, WAKATI HAUJAFIKA BADO KWA WALIO AMINI ZIKANYENYEKEA NYOYO ZAO KWA KUMKUMBUKA ALLAH NA HAKI ILIYO TEREMKA? WALA WASIWE KAMA WALIO PEWA KITABU KABLA YAO, MUDA WAO UKAWA MREFU, KWA HIVYO NYOYO ZAO ZIKAWA NGUMU NA WENGI WAO WAKAWA WAPOTOVU”. [57:16]

Huenda wakati sasa ndio umefikia, na pengine wimbi hili la mwamko lililo anza kusambaa katika ulimwengu wa Kiislamu ni bishara ya mapambazuko mapya kwa uma huu. Na ni miongoni mwa chomozi za nuru njema kwa uma huu ulio hemewa, nuru itakayo utoa kutoka vizani kuuongozea kwenye njia ya sawa. Na kuuweka juu ya khazina ya nguvu na utukufu alio utia Allah ndani ya dini yao. Hapo uma ukapata nguvu baada ya udhaifu/unyonge, utukufu baada ya udhalili na kunadi saada baada ya dhiki.

 

    iv.               Mtume wa Allah awarudishia Hawaazin mali na watu wao:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo maliza kugawa mateka na mali, ukamjia ujumbe wa waislamu wa Hawaazin, wakitarajia kurudishiwa mali na watoto wao. Mtume akawakhiarisha kuchagua baina ya mateka na mali, nao wakakhitari watoto  na wake zao. Mtume akawaambia maswahaba wake: “Hakika watu hawa wamekuja ilhali wakiwa ni waislamu, nami nilikuwa nimechelewesha ugawaji wa mateka wao. Nikawapa khiari kuchagua, hawakuchagua mali juu ya wake na watoto, basi ye yote mwenye cho chote cha mateka wao na nafsi yake ikawa njema kukirudisha, basi njia i wazi. Na atakaye kataa, basi awarudishie tu na huo uwe ni mkopo ametukopesha sisi, nae atapata mafungu sita kwa kila mmoja wetu katika mali atakayo tupa Allah”. Maswahaba wakasema: “Tumeridhia na tumesalimu amri”. Wakawarudishia wake na watoto wao na wala hakuna aliye sita kufanya hivyo ila Uyainah Ibn Hiswn. Yeye huyu alikataa kumrejesha kikongwe aliye angukia mikononi mwake kama mgao na fungu lake kutokana na ushiriki wake vitani, halafu baadae akamtoa. Kisha Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akauuliza ujumbe wa Hawaazin khabari za aliye kuwa kiongozi wao; Maalik Ibn Auf. Akaelezwa kuwa bado yuko Twaif  pamoja na kabila la Thaqiyf , akawataka wamfikishie khabari kwamba iwapo atamjia ilhali yu muislamu, atamrejeshea mali na watu wake. Na ziada ya hivyo, atampa na ngamia mia, Maalik alipo fikiwa na ahadi hiyo ya Mtume wa Allah, akawatoroka Thaqiyf na kumuendea Mtume wa Allah ilhali akiwa tayari ni muislamu. Mtume akamtekelezea ahadi yake na akamsimika kuwa amiri wa watu wake walio silimu, akawa anawaongoza kupigana na Thaqiyf na kuishambulia mifugo yao mpaka wakasongeka.

 

      v.               Mtume arejea Madinah:

         Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo maliza suala la ngawira, akaondoka hapo Ji’iraanah kwenda kufanya Umrah. Na huo ulikuwa ni usiku wa Jumatano, mwezi kumi na mbili, Dhul-Qa’adah (Mfunguo Pili). Akahirimia umrah, akaingia Makah akatufu, akafanya Sa’ayi na akanyoa, halafu akarejea Ji’iraanah usiku ule ule.

Mtume wa Allah alimuachia ukhalifa wa Makah Attaab Ibn Usayd na akamuacha pamoja nae Muaadh Ibn Jabal awafundishe watu dini pamoja na kuwasomesha Qur-ani. Attaab huyu alikuwa kijana mbichi wa umri upatao miaka ishirini hivi, lakini alikuwa mcha-Mungu mno, sifa iliyo mstahikisha kuwa amiri wa Makah pamoja na umri wake huo mdogo. Mtume wa Allah akamuandikia kupata dirham moja kila siku, Attaab akawa anasema: “Allah asilishibishe ini la mwenye kusikia njaa pamoja na kupata dirham moja! Kwa yakini Mtume wa Allah ameniruzuku dirham moja kila siku, kwa hivyo mimi sina haja kwa ye yote”.

Halafu Mtume wa Allah-Rehema na amani zimshukie-akaondoka kurejea Madinah, akawasili huko mwishoni mwa Dhul-Qa’adah au mwanzoni mwa Dhul-Hijjah (Mfunguo Tatu), mnamo mwaka wa nane Hijriah. Hivi ndivyo mwaka wa nane ulivyo tamatia kwa fat-hi (ushindi) Makah na kuondosha kikwazo kikuu kilicho kuwa kimeziba njia ya da’awah. Kwa kuondoka kwake, chemchem ya Uislamu ikachimbuka katika ardhi ya Ghuba na kuzifunika janibu zake zote. Ukaingia mwaka wa tisa, zikaja jumbe za Waarabu kutokea pande zote za Ghuba, zikaja Madinah kwa khiari zao. Ili kuutangaza Uislamu na utiifu wao kwa Mtume na wakaingia katika dini ya Allah kwa radhi ya nafsi zao bila kutenzwa nguvu.

 



 | Tuandikie |