Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SURA YA KUMI NA TATU
VITA VYA TABUUK 

 Faida

SOMO LA KWANZA.

            i.            Majukumu ya uma wa Kiislamu:

         Fat-hi (ushindi) Makah ilikuwa ni tangazo la kuingia kwa Peninsula ya Kiarabu katika wigo wa Uislamu na Waarabu wote kuwa chini ya bendera yake. Baada ya Fat-hi Makah na kusilimu kwa Makureishi, Waarabu wakatambua kwamba hawana njia ya kuhepa kuingia katika Uislamu sasa au baadae. Hii ni kwamba Waarabu – kama anavyo sema Ibn Ishaq-Allah amrehemu-: “Hakika si vinginevyo, walikuwa wakiungojelea Uislamu suala la kitongoji hiki cha Makureishi ambao walikuwa ndio viongozi na watawala wa watu. Wenyeji wa nyumba tukufu, kizazi cha Nabii Ismail Ibn Ibrahim-Amani iwashukie. Walikuwa (hao Waarabu) hawaupingi Uislamu, ni Makureishi ndio walio anzisha kumpinga na kumpiga vita Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Makah ilipo funguliwa na Uislamu ukawatenza nguvu Makureishi, Waarabu wakatambua kwamba hawana ubavu wa kupambana na Mtume wa Allah. Kwa ajili hii, wakaingia katika dini ya Allah makundi kwa makundi kama alivyo sema Allah Taala, wakitokea kila upande. Wakawa miongoni mwa muislamu aliye ingia Uislamuni akawa muislamu, na mushrikina anaye jiandaa kuingia ndani ya Uislamu ama leo au kesho. Haukupita ila mwaka mmoja tu, Peninsula ya Waarabu ikawa ni kambi ya Uislamu na wenyeji wake wakawa ndio walinzi wake.

Kuanzia hapo, uma wa kiislamu ukaanza kujiunda ndani ya Peninsula muundo wa dola na kuonekana ulimwenguni kama dola yenye nguvu za kuilinda na kudhamini amani/usalama wake. Madhumuni ya uma huu hayakuwa kama nyumati nyingine, bali muradi ni kuwa bora ya nyumati zote dhima yake ikiwa ni kuondosha fisadi, kusawazisha kombo kombo, kuamrisha mema na kukataza maovu. Ukisukumwa kuyaelekea haya na imani yake kwa Allah aliye pekee na raghba yake ya kutaka maisha katika ardhi yawe juu ya msingi ambao Allah amewawekea waja wake. Dola ya Kiislamu ilisimama juu ya msingi huu katika Peninsula hii ya Waarabu. Na kwa lengo hili, ikaiwekea kanuni ambazo zinadhamini usalama/amani ya jamii yake dhidi ya maafa yote. Kuilinda ardhi yake dhidi ya kila adui na kuwaandaa watu wake kubeba majukumu ya uma bora/teule. Na kustahamilia matokeo/natija zitakazo jitokeza kutokana na mapambano dhidi ya dhulma na kusimamisha uadilifu. Na taklifu zinazo ambatana na uondoshaji wa shari/uovu na kueneza kheri/wema na hii ni dhima (kazi) nzito. Lakini ndio dhima ambayo Allah ameutwika uma wa Kiislamu na akaufanya kuwa uma bora kwa ajili tu ya kuitekeleza kwao dhima hiyo. Tunasoma: “NYINYI MMEKUWA BORA YA UMA WALIO TOLEWA WATU, KWA KUWA MNAAMRISHA MEMA NA MNAKATAZA MAOVU, NA MNAMUAMINI ALLAH...” [3:110]

 

         ii.            Kuundwa kwa dola ya Kiislamu kulikuwa ni tishio kwa maslahi ya Urumi katika Rasi ya Kiarabu:

         Wakati ambapo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alikuwa akiuandaa uma wake kwa ajili ya dhima (kazi) hii tukufu. Na kulitwaharisha anga la uma huu kutokana na athari ya ufisadi na shirki na kufuta katika ardhi yake nembo/alama za shirki na ibada za miungu sanamu. Na akipeleka vikosi kwenye makabila ya Kiarabu yanayo mzunguka, kwenda kuyavunjilia mbali masanamu na kuueneza Uislamu mahala pake. Warumi kaskazini mwa Rasi hii,  walikuwa wakiyaangalia matukio yote haya kwa jicho la khofu. Mtazamo wao huo ulitokana na vitega uchumi mbali mbali vyao  walivyo kuwa wakivimiliki katika Rasi hii. Na hapana shaka kwamba maslahi yao hayo yalikuwa yanaathiriwa na matukio haya yanayo jiri katika  Rasi hii. Warumi walikuwa na misafara ya biashara iliyo kuwa ikipita kusini na kaskazini, mashariki na magharibi mwa Rasi hii ya Waarabu. Na walikuwa na washirika miongoni mwa Waarabu walio kuwa wakiishi kaskazini mwa rasi hii, hawa walikuwa wakipokea amri na kuunyenyekea utawala wa Kirumi. Na hali kadhalika walikuwa na washirika katikati ya kisiwa hiki, Warumi waliwategemea washirika wao hawa katika kuihami misafara yao ya biashara. Na unaswara ambao ndio ulikuwa dini rasmi ya dola ya Kirumi, ulikuwa ndio dini ya kabila la Ghassaani; washirika wa Warumi. Dini hii pia ilifuatwa na Waarabu waungwana walio kuwa wakiishi kaskazini na kusini mwa Rasi hii.

Maslahi yote haya, Warumi waliwania kuyabakisha na miongoni mwa vitendakazi ambavyo vilisaidia kusalikia kwa maslahi haya kwa Warumi. Ni kwamba Waarabu kwa mazingira ya maisha yao, walikuwa ni makabila mtapanyiko ambayo hayakuwa na umoja wala sauti moja. Na kila kabila lilikuwa likishughulikia mambo yake lenyewe au mambo ya washirika wao tu basi. Kutokana na mazingira haya, Waarabu waliishi katika mfarakano daima na ili maslahi ya dola la Kirumi yaendelee kudumu hapana budi mfarakano huu baina ya Waarabu uendelee. Uislamu ulipo dhihiri katika Rasi hii ya Waarabu na ukaanza kuwaunganisha Waarabu na kuzikusanya safu zao chini ya bendera yake. Na sauti yake ikaanza kupaaza na kupaaza mpaka ikagonga masikio ya wafalme wa jirani yake na mzingo wake ukatanuka na kutanuka mpaka ukakurubia kuzichanganya pande za Rasi hii ya Waarabu. Hapo Warumi wakaanza kuitanabahi khatari itokanayo na tukio jipya hili linalo jiri katika mkondo wa historia. Na huenda cha mwanzo kilicho wazindua ni ule mlingano (da’awah) – jasiri ulio elekezwa na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa mfalme Qayswari wa Urumi. Akimlingania kumuamini Allah pekee na kumfuata katika anacho kilingania na awalinganie wafuasi wake miongoni mwa Warumi na wasio Warumi kuingia katika Uislamu. Na akimbebesha jukumu la kuzembea kuutangaza na kuufikisha mlingano huu kwa wafuasi na washirika wake.

Tarekh (historia) inatuonyesha kwamba Qayswari hakuipuuzia khatari ya mlingano huu, bali yeye ndiye wa mwanzo aliye itangaza khatari hiyo kwa masultani na wafalme wenzake. Hiraqli alipo fikiwa na ujumbe wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaanza kuulizia juu ya Muarabu anaye tokana na kaumu ya Mtume huyu ili apate kumuuliza khabari zake. Akauliza mpaka akakwaana na Abu Sufyaan Ibn Harb, akaanza kumuuliza maswali ya mtu mjuzi mpelelezi kuhusiana na kila alilo taka kujua juu ya mtume huyu mpya. Hata alipo tosheka na kujua hakika yake, akamwambia Abu Sufyaan: “Ikiwa uyasemayo ni kweli, basi atamiliki mahala hapa ilipo kanyaga miguu yangu hii”.  

 



 | Tuandikie |