|
iii.
Warumi waliufuatilia
kwa karibu mno mwenendo wa da’awah:
Kutokana na maelezo yaliyo tangulia itakubainikia kwamba Dola ya Kirumi
iliufahamu mlingano (da’awah) wa Uislamu. Na ilikuwa ikiuona kama khatari
kubwa iliyo milangoni mwao na ilitambua kwamba mlingano huu utayagusa
maslahi yake kwa kiasi kikubwa. Na kwa ajili hii basi, inatakiwa isijisahau
au kujilaza. Na pengine vita vya Mu’utah ilikuwa ndio hatua ya kwanza iliyo
fanywa na Warumi katika kuiondoshea dola yao khatari hii. Na kwa ajili ya
kuuzima mlingano huu ambao waliudhania kuwa ni cheche za moto ambazo
kuzimika kwake hakuna muda. Walipo waona waunga mkono wake hawako katika
unyonge kama walivyo sawirisha, wakaanza kuiangalia da’awah kwa mtazamo
makini. Wakaanza kutafuta khabari zake na kufuatilia nyendo zake kwa makini
na karibu. Na walikuwa na majasusi wanao waletea khabari juu ya harakati za
da’awah, wakiwaelezea kila kinacho jiri baina ya Mtume wa Allah na maswahaba
wake.
Huyu hapa
Ka’ab Ibn Maalik-Allah amuwiye radhi-anasimulia kisa chake pale alipo kuwa
hakwenda katika vita vya Tabuuk pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie. Na Mtume akawakataza watu kuzungumza nae, anasema: Kwamba mfalme
wa kabila la Ghassaani alimtumia barua akimwambia: “Ama baad, hakika
imetufikia khabari kwamba mtu wako (Mtume) amekukata pande. Na wala Allah
hakukuweka katika nchi ya unyonge wala dhiki, basi njoo kwetu tutakuliwaza”.
Na ikumbukwe kwamba wakati huo dola ya Ghasaani ilikuwa ni mshirika wa dola
ya Kirumi. Lau si kuwa Warumi walikuwa wakifuatilia khabari za Mtume na
maswahaba wake, basi isingelikuwa lazima khabari hii ya Ka’ab kuwafikia. Na
wala si kawaida hata kama ingewafikia kwa sadfa, mfalme wa Ghassaani
kuishughulikia kwa kiasi hiki.
iv.
Msikiti wa Dhwiraari:
Na katika kisa
cha msikiti Dhwiraari, kuna sehemu/upande mwingine unao ashiria uhusiano
ulio kuwepo baina ya Warumi na wanafiki miongoni mwa wenyeji wa Madinah.
Riwaya zimetaja kwamba Padri Abu Aamir hakuweza kubakia Madinah, baada ya
dini ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kudhihiri humo. Akaenda kwa
Qayswari mfalme wa Urumi kumuomba msaada dhidi ya Mtume huyu, mfalme akampa
ahadi ya kumsaidia na akampa hifadhi kwake. Abu Aamir akaliandikia barua
kundi la kaumu yake katika watu wanafiki akiwaahidi kwamba yeye atakuja na
jeshi kukabiliana na Muhammad. Na atawashinda na kuizuia itikadi yake hiyo
ya Mungu mmoja. Na akawaamuru kumtengenezea ngome atakayo fikia mjumbe wake
anaye uleta waraka wake kwao. Na ngome hiyo itakuwa malindizo (mavizio) yake
na wao atakapo kuja kwao baadae, ndipo walipo anza kujenga msikiti jirani na
msikiti wa Qubaa mpaka wakakamilisha ujenzi wake. Halafu wakamuendea Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-nae akijiandaa kuelekea Tabuuk,
wakamwambia: “Ewe Mtume wa Allah! Hakika sisi tumejenga msikiti kwa ajili ya
wagonjwa na wenye haja na usiku wa mvua, nasi tunapenda wewe utuswalishe
humo (utufungulie msikiti wetu)”. – wakikusudia kwa kitendo hicho, Mtume
awakubalie ujenzi wao huo na kuuthibitsha msikiti wao. Mtume wa Allah
akawaambia: “Hakika sisi tumo safarini na katika hali ya mshughuliko,
tutakapo rudi tutakujilieni na kuwaswalisha humo, Inshallah”.
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo anza msafara kurejea kutoka
Tabuuk na haukubakia umbali baina yake na Madinah ila mwendo wa siku moja
tu, ukamshukia wahyi juu ya msikiti wa Dhwiraari. Ukielezea juu ya dhamira
mbaya ya wajenzi wake katika kuwakufurisha na kuwafarakanisha waumini na
mavizio kwa walio mpiga vita Allah na Mtume wake hapo kabla. Mtume wa
Allah-Rehema na amani zimshukie-akawatuma watu kuubomoa msikiti huo kabla ya
kuwasili kwake Madinah. Na kuhusiana na tukio hili, Allah Taala anasema: “NA
WAPO WALIO JENGA MSIKITI KWA AJILI YA MADHARA NA UKAFIRI NA KUWAFARIKISHA
WAUMINI, NA PA KUVIZIA KWA WALIO MPIGA VITA ALLAH NA MTUME WAKE HAPO KABLA.
NA BILA YA SHAKA WATAAPA KWAMBA: HATUKUKUSUDIA ILA WEMA TU. NA ALLAH
ANASHUHUDIA KUWA WAO NI WAONGO. USISIMAME KWENYE MSIKITI HUO KABISA. MSIKITI
ULIO JENGWA JUU YA MSINGI YA UCHAMNGU TANGU SIKU YA MWANZO UNASTAHIKI ZAIDI
WEWE USIMAME NDANI YAKE. HUMO WAMO WATU WANAO PENDA KUJITAKASA NA ALLAH
ANAWAPENDA WANAO JITAKASA”. [9:107-108]
|