|
i.
Warumi wafanya
maandalizi kabambe kuifyekelea mbali dola ya Kiislamu:
Kutokana na maelezo yaliyo tangulia, itakubainikia
kwamba Urumi haikuipuuzia hata kidogo da’awah ya Kiislamu. Allah alipo
mfungulia Mtume wake Makah na da’awah ya Kiislamu ikaanza kutapanyika na
kuenea pande zote za Peninsula ya Kiarabu. Warumi wakawa na yakini kwamba
khatari inakaribia kuwagubika na kwa hivyo basi hapana budi zichukuliwe
hatua za haraka ili kuiepusha khatari hiyo. Na ni vema ikakumbukwa kwamba
dola ya Urumi wakati huo ilikuwa na nguvu kubwa na sauti katika ulimwengu
ule kama ilivyo Marekani katika ulimwengu wetu huu wa leo. Na ni miaka
michache tu ilikuwa imepita tangu itoke vitani na dola nyingine kubwa;
Uajemi na kufanikiwa kuishinda. Urumi ilikuwa na nguvu kubwa ya kijeshi
kuliko dola yo yote ya enzi hizo, nguvu iliyo ipa kiburi cha kuamini kuwa
ina uwezo wa kuuponda ponda uma wa Kiislamu kama itakavyo. Kwa imani hiyo,
Warumi wakaanza maandalizi kwa ajili ya kuufyeka uma huu mchanga unao anza
kujiunda. Na pengine walikusudia kuushambulia ndani ya mipaka yake ili
waukate kabisa mzizi wake na kuifutilia mbali dini yake. Wakakusanya majeshi
wayatakayo na wakaandaa zana za vita wazitakazo na wakaanza maandalizi ya
kuyakata masafa marefu ili kuwapiga waislamu kwao.
Khabari zikamfikia Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-kwamba Warumi wamekusanya chungu ya majeshi huko Shamu. Na kwamba
mfalme Hiraqli amewapa watu wake chakula cha mwaka mzima. Na amekusanya
washirika kutoka katika makabila ya Kiarabu ya Lakhum, Judhaam na Ghassaan
na wametanguliza vikosi vyao vya mwanzo mahala paitwapo “Al-Balqaa”. Kwa
khabari hizi, ikamlazimu Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kufikiria
namna ya kukabiliana na uadui huu. Na mbele yake zilikuwepo njia/hatua mbili
za kukabiliana na uchokozi huu; ya kwanza ni kuwaacha Warumi wakitangatanga
katika uwanda wa nchi yake, kisha akabiliane nao pale panapo mfalia. Na ya
pili yeye aende kuwashambulia huko huko katika mipaka yao. Na njia ile ya
kwanza ikawa ndio nyepesi zaidi, lakini inaweza kumpelekea yeye kuzikosa
baadhi ya kabila ambazo ameingia nazo ushirika hivi karibuni. Kwa ajili hii
basi, akachagua ile njia/hatua ya pili.
ii.
Mtume wa Allah awaita
maswahaba wake kupambana na Warumi na watu wanyoofu wa nia washindana katika
kutoa gharama za vita:
Na kikawaida, mzigo/jukumu la kuilinda Peninsula ya
Kiarabu (wakati huo ilikwisha kuwa ngome ya dola ya Kiislamu) libebwe na
wazalendo wa Peninsula hii, miongoni mwa walio silimu. Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-akawatolea watu wito wa kutoka na akawatuma wajumbe
kufikisha wito wake huo Makah na kwa makabila ya Kiarabu. Na akawafahamisha
mapema anako kukusudia ili wapate kufanya maandalizi yanayo lingana na
safari hiyo ndefu. Mtume wa Allah akawakhutubia watu, akawahimiza jihadi na
akawaamrisha kutoa sadaka na akawaraghibisha matajiri kufanya kheri na wema.
Na akawahimiza wenye uwezo kuwaandaa wasio na uwezo, hapo waislamu
wakaangupiza kutoa katika mali zao, wakishindana katika kulitayarisha jeshi
lao hilo.
Sayyidna Uthmaan Ibn Affaan-Allah amuwiye radhi-akatoa
dinari alfu kumi, ngamia alfu tatu na farasi khamsini. Sayyidna Abu Bakri
akaleta dirham alfu nne, zikiwa ndio mali yake yote na Sayyidna Umar Ibn
Al-Khatwaab akaleta nusu ya mali yake. Sayyidna Abdur-Rahmaan Ibn Auf
akaleta wakia mia mbili za fedha na Sayyidna Abbaas Ibn Abdul-Mutwalib
akabeba mali inayo kisiwa kufikia dirham alfu tisini. Na Twalhah Ibn
Ubeidillah, Sa’ad Ibn Ubaadah na Muhammad Ibn Maslamah, wakabeba mali nyingi
na Aaswim Ibn Adiy akatoa sadaka makorobasi (aina ya makapu makubwa) tisini
ya tende. Na wanawake wakachangia kila walicho kiweza katika mapambo yao,
wakawa wakitupia katika nguo iliyo tandikwa mbele ya Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie. Mapambo yao waliyo vaa mikononi mwao, miongoni mwa
bangili, pete na kadhalika. Na mapambo waliyo vaa miguuni mwao na yale ya
masikioni mwao na shingoni mwao. Waislamu wakashindana kutoa, mpaka ikafikia
mtu kumletea mtu mmoja au wawili ngamia, akiwaambia: “Ngamia huyu mtampanda
kwa kupokezana”. Na mwingine akileta masurufu na kumpa baadhi yake mtu anaye
toka kwenda katika jihadi.
Kama hivi ndivyo watakasifu wa nia walivyo kuwa wakifanya
ukarimu kwa kutoa mali zao na wakishindana katika kuliandaa jeshi, kila
mmoja kulingana na uwezo wake. Aliye weza kujigharamia yeye mwenyewe na mtu
mwingine, alifanya hivyo kwa kadri alivyo weza. Na asiye weza alijigharamia
yeye mwenyewe na ikatosha. Kundi la waislamu mafakiri likashindwa kujiandaa
lenyewe, wakamuendea Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-wakimuomba
awape vipando vya ziada alivyo navyo. Akawaondosha kwa kuwaambia: “...SINA
KIPANDO CHA KUKUCHUKUENI (kwenda jihadini)...” [9:32] Wakaondoka na ilhali
macho yao yakifurika machozi kwa huzuni ya heshima ya jihadi waliyo ikosa.
Kwa sababu tu ya ufakiri wao na kushindwa kwao kujiandaa wao wenyewe kwa
gharama zao.
|