|
I.
Safari hii iliyo
sheheni kila aina ya taabu ilikuwa ni mtihani ulio wapambanua waumini na
wanafiki:
Kwa yakini kabisa, taabu hii iliyo wafika waislamu
katika safari yao hii ya kwenda Tabuuk, ilikuwa ni mtihani/jaribio kwao
kutoka kwa Allah Mola Muumba wao. Alitaka kupitia mithani huo kuwapambanua
waumini, kuwatakasa na kuwaandaa kustahamilia taabu ya kuipigania dini yake.
Na ili apate kuona kiwango cha subira ya wasubiriao na ukweli wa wakweli
katika njia ya kuihami dini yao. Ikawa hawawezi kuistahamilia tabu hii ila
wale walio na imani ya kweli na itikadi iliyo kita mizizi. Ama wanafiki na
wale walio jionyesha kuwa na imani, hawa walisukwasukwa na kudhoofu azma
zao, wakawa wakipenya nyuma ya safu wakirejea walikotoka.
Ibn Is-haaq-Allah amrehemu-anasema: “Kisha Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaendelea kwenda, ikawa mtu mmoja mmoja
anabakia nyuma asende nae. Maswahaba wakimwambia: Ewe Mtume wa Allah wee!
Fulani amebakia nyuma, nae huwajibu: “Muacheni, ikiwa kuna kheri kwake,
Allah atakukutanisheni nae na akitokuwa hivyo, basi Allah amekupumzisheni
nae”. Abu Dhari akabakia nyuma na ngamia wake, alipo ona anamchelewesha
akachukua mzigo wake akaubeba mgongoni kwake, kisha akatoka akizifuatia
nyayo za Mtume wa Allah kwa miguu. Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akashuka katika baadhi ya mashukio yake, mmoja katika waislamu
akaona kitu kwa mbali, akasema: Ewe Mtume wa Allah wee! Hakika huyo (ajaye)
ni mtu anatembea njiani peke yake. Mtume wa Allah akasema: “Kuwa (ewe ujaye
ni) Abu Dhari!” Watu walipo mtia machoni, wakasema: Ewe Mtume wa Allah wee!
Wallah, ni Abu Dhari kweli! Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akasema: “Allah amrehemu Abu Dhari! Anatembea peke yake kwa miguu,
atakufa peke yake na atafufuliwa peke yake”.
II.
Abu Khaythamah:
Kuna kundi la waislamu lililo kawizwa na kutokuwepo
mjini mpaka likabakia nyuma lisitoke pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-bila ya kuwa na shaka. Miongoni mwao alikuwemo Ka’ab Ibn
Maalik, Muraarah Ibn Rabeea, Hilaal Ibn Umayyah na Abu Khaythamah. Hawa
walikuwa ni watu wakweli, usio tiliwa shaka Uislamu wao. Ama hawa watatu
tulio wataja mwanzo, hawa walikawizwa na azma zao na wakatambaliwa na
unyongevu na kikawaghuri wao kivuli (cha miti yao) na maji hata wakakaa
wasende vitani. Nao walikuwa na jambo pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-Allah akateremsha Qur-ani katika jambo hilo. Ama Abu
Khaythamah, yeye alijidiriki kabla muda haujapita, akaungana na Mtume wa
Allah.
Ibn Is-haaq-Allah amrehemu-anasema: “Halafu tena Abu
Khaythamah akarejea mjini – (baada ya Mtume kuondoka kwa siku kadhaa) – kwa
ahali zake katika siku ya joto kali. Akawakuta wake zake wawili katika
vibanda vyao ndani ya bustani yake ya mitende. Na kila mmoja akiwa
amekinyunyizia maji kibanda chake na kumuwekea maji baridi na kumuandalia
chakula. Alipo fika akasimama mlangoni mwa kibanda, akawaangalia wake zake
na vile walivyo muandalia, akasema: Mtume wa Allah yuko katika unguzo la
jua, upepo na joto na Abu Khaythamah akiwa katika kivuli baridi, chakula
kilicho andaliwa, mwanamke mzuri, akikaa kwenye mali yake?! Hii sio insafu
wala uadilifu! Halafu akasema: Wallah, sitaingia kibandani kwa mmoja wenu
mpaka niungane na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie! Haya niandalieni
pamba (chakula cha njiani). Wakamuandalia, kisha akamleta ngamia wake
akapakia mizigo yake tayari kwa safari. Kisha huyoo akatoka kumfuatia Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-hata akamdiriki pale alipo piga kambi
Tabuuk.
III.
Mtume wa Allah
hakumkuta hata Mrumi mmoja Tabuuk na aamua kutokusonga mbele:
Wakati Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-alipo fika Tabuuk na akawa kwenye mipaka ya dola ya Kirumi,
hakumkuta ye yote katika maadui. Na yawezekana kwamba Warumi walipendelea
kuwa ndani ya nchi ya Urumi ili wapate kujihifadhi na ngome zake pale ilipo
wafikia khabari ya jeshi hili la waislamu na nguvu zake, kama anavyo sema
Daktari Haikal. Na pia inawezekana waislamu waliacha kusonga mbele pale
walipo tambua kinyume na walivyo kuwa wakifikiria, kwamba Hiraqli hajaandaa
jeshi kushambulia Madinah. Mwandishi wa kitabu “Al-imtaau”, anapita mapito
haya, anaona kwamba alivyo khabarishwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie. Kwamba Hiraqli na watu wake wako karibu na Shamu wanakuja
kushambulia Madinah, zilikuwa ni khabari batili na wala Hiraqli
hakulikusudia hilo.
Vyo vyote ulivyo kuwa uhakika wa suala hili, ni kwamba Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alisimama hapo Tabuuk na wala hakuvuka
kwenda mbele. Akavituma vikosi vyake kwa washirika wa Urumi miongoni mwa
manaswara wa Kiarabu waishio katika mzonge wa Tabuuk. Watu wa Aylah,
Adhruhu, Jarbaa, Maqnaa na Duumatul-Jandal wakafanya nae suluhu juu ya kutoa
kodi na waingie katika dhima na amani ya Uislamu. Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-akakaa hapo Tabuuk kiasi cha siku kumi hivi. Halafu
akawataka maswahaba wake ushauri juu ya kuvuka mpaka na kuingia ndani ya
miji ya Shamu. Sayyidna Umar-Allah amuwiye radhi-akamwambia: “Ewe Mtume wa
Allah! Ikiwa umeamrishwa kwenda basi nenda”. Mtume akasema: “Lau ningelikuwa
nimeamrishwa, basi nisingelitaka ushauri”. Umar akasema: “Ewe Mtume wa
Allah! Hakika Warumi wana majeshi shirika mengi na huko Shamu hakuna
muislamu hata mmoja. Nawe umewakurubia na ujio wako tayari umesha
wafadhaisha, basi lau mwaka huu ungelirejea uone au Allah alete amri yake”.
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akaufuata ushauri wa Umar na
akaamuru kurejea. Basi jeshi likarejea Madinah baada ya Mtume kuiweka katika
hali ya amani mipaka ya kaskazini ya dola ya Kiislamu. Kutokana na mikataba
aliyo andikiana na Manaswara wa Kiarabu walio jiranikiana na dola ya Urumi.
Na kurejea kwake Mtume, Madinah kulikuwa ndani ya mwezi wa Ramadhani
[Desemba – 630 A.D.]. Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo karibia
kuingia Madinah, watu walitoka kumlaki. Pamoja nao walitoka watoto, wanawake
na vijakazi. Na wanawake wa tabaka la juu wakapanda juu ya majumba yao
wakiimba na kughani kwa ajili ya kufurahikia kurudi kwa Mtume wa Allah.
|