|
III.
Ka’ab amueleza ukweli
Mtume wa Allah:
Ka’ab Ibn Maalik-Allah amuwiye radhi-anaendelea
kusimulia khabari yake, anasema: “Nilipo msalimia Mtume, akatabasamu
tabasamu la mtu aliye ghadhibika, halafu akasema: Njoo. Nikaenda mpaka
nikakaa mbele yake, akaniuliza: “Ni lipi lililo kubakisha nyuma? Hivi wewe
hukuwa umeshanunua kipando chako?” Nikajibu: “Kwani wallah, na hakika mimi
wallah ewe Mtume wa Allah, lau ningelikuwa mbele ya asiye kuwa wewe miongoni
mwa watu wa dunia. Najiona ningeliokoka na ghadhabu yake kwa udhuru, kwani
mimi nimepewa ufundi wa kuzungumza. Lakini mimi wallah, ninajua leo
nikikuongopea ukaniridhia, ninachelea Allah kukufanya unighadhibikie. Na
nikikueleza ukweli utanighadhibikia, hakika mimi ninatarajia ndani ya ukweli
huo kupata msamaha wa Allah hapo baadae. Wallah, hapana mimi sikuwa na
udhuru wo wote! Wallah, katu sikuwa mwenye nguvu zaidi na mwepesi mno kuliko
wakati nilio bakia nyuma nisitoke pamoja nawe”. Mtume wa Allah-Rehema na
Amani zimshukie-akasema: “Ama huyu, hakika amesema kweli, basi nenda zako
mpaka Allah akuhukumu”.
Basi nikainuka nikaondoka, wakanifuata haraka watu katika
Baniy Salamah, wakaniambia: “Wallah, hatukujua kuwa umefanya kosa kabla ya
leo, umeshindwa kutoa udhuru kwa Mtume wa Allah kama walivyo fanya walio
bakia nyuma! Hakika ilikuwa inakutoshea dhambi yako hiyo (ya kusema uwongo),
istighfaari ya Mtume wa Allah”. Basi wallah, hawakucha kunikaripia na
kunikemea mpaka nikataka kurejea kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-nikaikadhibishe nafsi yangu. Halafu nikawauliza: Je, yamemkuta
haya pamoja nami mtu mwingine au ni miye tu? Wakajibu: “Naam, watu wawili
wamesema kama ulivyo sema wewe na wao wakaambiwa kama ulivyo ambiwa wewe”.
Nikauliza: Ni kina nani hao? Wakasema: “Muraarah Ibn Rabee Al-Amriy na
Hilaal Ibn Umayyah Al-Waaqifiy”. Wakanitajia watu wawili wema walio shiriki
katika vita vya Badri, ambao mimi nina kigezo chema kwao. Basi nikashikilia
msimamo wangu pale walipo nitajia watu hao.
IV.
Kuadabisha na
kunyoosha:
Akazidi kusema: “Na Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akakataza watu kuongea nasi, sisi watu watatu miongoni mwa walio
bakia nyuma wasende pamoja naye vitani. Basi watu wakatuepuka na
kutubadilikia mpaka nikaoina mbaya ardhi ile ikawa kama si ile ardhi
niijuayo, tukakaa katika hali hiyo ya mtengo kiasi cha siku khamsini. Ama
wale wenzangu wawili, wao wakajisalimisha wakakaa majumbani mwao, hawakutoka
kabisa. Ama mimi ndiye niliye kuwa kijana kati yao na mwenye moyo thabiti,
basi nikawa natoka nahudhuria swala ya jamaa pamoja na waislamu. Na
nikizunguka masokoni, basi hapana mtu ye yote anaye nisemesha. Na
nikimuendea Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ninamsalimia naye akiwa
katika kitako chake baada ya swala. Nikijiambia moyoni: Je, ameitukutisha
midomo yake kuitikia salamu yangu au la. Kisha huswali Sunnah karibu naye
huku nikimtazama kwa wizi, ninapoa anza kuswali huniangalia na nikigeukia
upande wake hukengeuka nami. Hata kilipo repa kitambo cha kukatwa pande na
watu, nikaenda nikauparamia ukuta wa nyumba ya Abu Qataadah. Huyu ni binamu
yangu na aliye kipenzi mno kwangu, nikamtolea salamu, basi wallah
hakunijibu, nikamwambia: Ewe Abu Qataadah, ninakuapia kwa Allah, hivi unajua
kwamba mimi ninampenda Allah na Mtume wake? Akanyamaza kimya asinijibu kitu,
nikarudia tena nikamuapia, akanyamaza kimya. Nikamuapia na kurudia mara ya
tatu, ndipo akasema: “Allah na Mtume wake ndio wajuao zaidi (ukweli wa hayo
uyasemayao)”. Macho yangu yakafurika machozi furi furi, nikarudi nyuma
nikaparamia ukuta nikaondoka zangu”.
V.
Warumi wajaribu
kuitumia fursa hii kumfarakanisha Mtume na maswahaba wake:
Anasema Ka’ab: “Basi wakati mmoja nikiwa natembea
sokoni Madinah, tahamaki huyo ni Mnabati miongoni mwa Manabati wa Shamu
walio kuja kuuza chakula Madinah, akiuliza: “Ni nani atakaye nifahamisha
Ka’ab Ibn Maalik?”, watu wakaniashiria mimi. Hata alipo nijia akanipa waraka
kutoka kwa mfalme wa Ghassaan, nikausoma na ndani yake mliandikwa: “Ama
baad, hakika imetufikia khabari kwamba mtu wako (Muhammad) amekukata pande.
Na wala Allah hakukuweka kwenye nchi ya udhalili wala mapuuzo, basi njoo
kwetu tutakuliwaza”. Nikajisemea nilipo kwisha isoma: Na hili tena ni balaa
jingine! Nikaenda nikaitia kwenye tanuri la moto nikaichoma. Hata zilipo
pita siku arobaini katika zile siku khamsini, tahamaki huyoo ni mjumbe wa
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-ananijia. Alipo fika akasema:
“Hakika Mtume wa Allah anakuamuru ujitenge na mkeo”. Nikauliza: Nimtaliki au
nifanyeje? Akajibu: “Hapana (usimtaliki), bali jitenge naye usimkurubie”. Na
akawatumia ujumbe kama huo wale wenzangu wawili. Nikamwambia mke wangu:
Nenda kwenu, ukae huko mpaka Allah alihukumu suala hili”.
Ka’ab anasema: “Mke wa Hilaal Ibn Umayyah akamuendea Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Ewe Mtume wa Allah! Hakika
Hilaal Ibn Umayyah ni mtu mzima asiye weza kujihudumia mwenyewe na wala hana
khadimu (mtumishi). Basi je, unaona vibaya mimi kumuhudumia yeye?” Mtume
akajibu: “Hapana (sioni vibaya), lakini asikukurubie (kimwili)”. Akasema:
“Wallah, hakika yeye hana nguvu ya lo lote. Wallah, amekuwa akilia tangu
lilivyo kuwa suala lake hili hadi hii leo”. Mmoja wa watu wangu akaniambia:
“Lau ungeli mtaka idhini Mtume wa Allah kwa mkeo, kwani amempa idhini mke wa
Hilaal Ibn Umayyah amtumikie”. Nikasema: Wallah, simtaki idhini Mtume wa
Allah kwa mke wangu, ninajuaje ataniambia nini nitakapo mtaka idhini na
ilhali mimi ni kijana?”
|