Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

SIRA YA MTUME (SAW)  

"BILA SHAKA MNAO MFANO MWEMA KWA MTUME WA MWENYEZI MUNGU…"Al-qur-an (33:21)

SOMO LA PILI

 

i) HALI YA KIDINI KATIKA BARA ARABU KABLA YA UISLAMU

Kabla ya kudhihiri kwa Uislamu Bara arabu halikuwa na dini moja bali lilisheheni dini nyingi. Baadhi ya wakazi wake walikuwa wakifuata dini ya Nabii Musa nao ni mayahudi na wengine waliifuata dini ya Nabii Isa, nao ni Manasara. Mbali na hawa walikuwepo pia waliokuwa wakiyaabudia masanamu. Qur-ani Tukufu imeyataja baadhi ya masanamu yaliyofanywa miungu kama vile Laata,Uzzah, Yaghuuth, Yauuqa na Nasrah. Kadhalika lilikuwepo kundi dogo lililokuwa likifuata dini ya haki likimuabudu mola wa haki kupitia mafundisho yaliyoletwa na Nabii Ibrahimu kutoka kwa Mwenyezi mungu.

Mwenyezi Mungu Mtukufu alipompa utume Muhammad na kumpa kazi nzito na jukumu kubwa la kutangaza dini ya Kiislamu aliinuka na kuanza kuwalingania watu wamuabudu Mungu mmoja asiye na mshirika na waache kuyaabudu masanamu waliyoyatengeneza wao wenyewe. Jawabu la Maquraysh lilikuwa ni kumkadhibisha Mtume na kumpinga vikali sana. Isitoshe walimuadhibu adhabu kali sana kila aliyemuamini na kumfuata Mtume ili iwe ni onyo kwa wengine. Hawakukomea hapo tu bali waliwazuia watu kuonana na kumsikiliza Mtume lakini kwa sababu ya subira, jihadi, imani yake na msaada wa Mwenyezi Mungu alifanikiwa kuwashinda maadui wa Uislamu na kuieneza dini ya Mwenyezi Mungu miongoni mwa Waarabu na watu wa mataifa mengine.

ii) IBADA YA MASANAMU

Kabla ya Uislamu waarabu walizama mno katika ibada ya masanamu mpaka wakaijaza Al-Kaaba masanamu ambayo idadi yake ilifikia masanamu mia tatu na sitini (360). Kila kabila lilikuwa na sanamu lake pekee na kila kaya/familia ilikuwa na sanamu malum kwa ajili ya familia hiyo tu. Mtu alipotaka kusafiri, alilichukua safarini sanamu moja ilikufanikiwa safarini na walikuwa wakiyatakasa na kuyatukuza masanamu haya kiasi cha kuyatolea Qurubaani na dhabihu (sadaka za kuteketeza). Waarabu walipokuwa wakitaka ushauri katika mambo yao mfano ndoa, biashara au safari basi uliendea "Hubal" sanamu lililokuwa ndani ya Al-kaaba wakampa ngamia na dir-ham mia mshika kete ambazo moja ilikuwa imeandikwa juu yake maneno"Mungu wangu amenikataza" na ya pili "Mungu wangu ameniamrisha" ya tatu "Naam/Ndiyo" ya nne "Hapana". Jumla kete zilikuwa ni saba, mshika kete huzizungusha na kuzichanganya kisha akaitoa moja na kilichoandikwa juu yake ndio huwa amri iliyotoka kwa Mungu sanamu.



Forum | Guestbook | Tuandikie |